HALMASHAURI YA KIPAPA
KWA AJILI YA MAZUNGUMZANO NA DINI MBALIMBALI
UJUMBE KWA AJILI YA KUMALIZA RAMADHANI
‘Id al-Fitri 1433 H. / 2012 A.D.
Malezi ya vijana Wakristo na Waislamu kwa ajili ya haki na amani
Wapendwa marafiki Waislamu,
1. Adhimisho la ‘Id al-Fitr’ ambalo linahitimisha mwezi wa Ramadhani, linatupa
hapa katika Halmashauri ya Kipapa kwa ajili ya Mazungumzano na Dini Mbalimbali
furaha ya kuwaletea salamu za upendo.
Tunafurahi pamoja nanyi kwa ajili ya muda huu wa upendeleo unaowapa fursa ya
kuzamisha utii kwa Mungu, kwa kufunga na matendo mengine ya ibada, tunu ambazo
hata kwetu zinathaminiwa.
Ndiyo sababu, mwaka huu, imeonekana kwetu inafaa kulenga fokasi ya tafakari ya
pamoja juu ya elimu ya vijana Wakristo na Waislamu kwa ajili ya haki na amani,
tunu ambazo hazitenganishwi na tunu za ukweli na uhuru.
2. Ikiwa kazi ya malezi imekabidhiwa kwa jamii nzima, kama mnavyofahamu, kwanza
kabisa, na kwa namna ya pekee, ni kazi ya wazazi na, pamoja nao, familia, shule
na vyuo vikuu, bila kusahau juu ya wale walio na wajibu kwa ajili ya maisha ya
imani, utamaduni, jamii, na uchumi, na ulimwengu wa mawasiliano.
Ni utendaji ambao ni mzuri na mgumu: kuwasaidia watoto na vijana kugundua na
kuendeleza rasilmali ambazo kwazo Muumba aliwajalia wawe nazo na kujenga
uwajibikaji katika mahusiano ya kibinadamu. Tukirejea juu ya kazi ya walezi,
Baba Mtakatifu Papa Benedikto XVI, hivi karibuni alithibitisha kwamba: “Kwa
sababu hiyo, leo kuliko wakati mwingine wowote, tunawahitaji mashuhuda wa kweli,
na si watu wanaoangalia tu sheria na matukio... Shahidi ni mtu yule ambaye
kwanza anaishi maisha anayowashauri wengine,” (”Ujumbe kwa ajili ya Siku ya
Ulimwengu ya Amani” 2012). Pamoja na hayo, tukumbuke pia kwamba vijana wenyewe
wanao wajibu pia kwa ajili ya malezi yao na kwa ajili ya malezi kwa ajili ya
haki na amani.
3. Awali ya yote, haki inapambanuliwa kwanza kabisa kwa utambulisho wa mwanadamu,
akiangaliwa katika ujumla wake woe; haiwezi kushushwa kwa viwango vyake vya
kubadilishwa au kugawanywa. Tusisahau kwamba jema la wote haliwezi kupatikana
bila mshikamano na upendo wa kidugu! Kwa waumini, haki halisi, inapokuwa katika
urafiki na Mungu , inazamisha mahusiano yote mengine: na mtu mwenyewe, na wengine na pamoja na uumbaji wote. Zaidi ya hayo, wanakiri kwamba haki ina
chanzo chake katika ukweli kwamba watu wote wameumbwa na Mungu na wanaitwa kuwa
wamoja, familia moja. Mtazamo huo wa vitu, pamoja na heshima kuu kwa akili na
uwazi kwa yaliyo ya juu, unawasukuma wanaume na wanawake wote wenye mapenzi mema,
ukiwaalika kupatanisha haki na wajibu.
4. Katika ulimwengu wetu uliojeruhiwa, kuwalea vijana kwa ajili ya amani kuna
umuhimu unaozidi kuongezeka. Kujiingiza sisi wenyewe kwa namna inayofaa, hali ya
kweli ya amani lazima ieleweke: kwamba haibaki tu katika maana finyu ya kutokuwa
na vita, au katika uwiano kati ya nguvu mbili zinazopingana, kwa wakati moja na
mara moja ni zawadi kutoka kwa Mungu na juhudi za mwanadamu kuitafuta bila
kukoma. Ni tunda la haki na tokeo la upendo. Ni muhimu kwamba waumini wakati
wote ni watendaji katika jumuiya zao wanamokuwamo: kwa kuishi huruma, mshikamano,
ushirikiano na udugu, wanaweza kwa hakika kuchangia kwa kuleta matokeo
yanayotakiwa katika kushughulikia changamoto kubwa za leo: makuzi ya kimapatano,
maendeleo kamilifu, kuzuia na kupatanisha magomvi, kutaja angalau machache.
5. Kwa kuhitimisha, tunapenda kuwahimiza vijana Waislam na Wakristo wasomaji wa
Ujumbe huu kujenga ukweli na uhuru, kusudi wawe wapiga mbiu kweli wa haki na
amani na wajenzi wa utamaduni unaoheshimu hadhi na haki za kila raia.
Tunawaalika kuwa na uvumilivu na ushupavu unaotakiwa kutekeleza mawazo haya,
kamwe bila kukimbilia maafikiano yenye mashaka, njia za mkato danganyifu au
mbinu zinazoonyesha heshima kidogo tu kwa mwanadamu. Wanaume na wanawake pekee
wanaoamini kwa unyofu mahitaji haya wataweza kujenga jamii ambamo haki na amani
zitakuwa ni za uhakika.
Mwenyezi Mungu ajaze utulivu na matumaini, mioyo, familia na jumuiya za wale
wanaolea hamu ya kuwa ‘ vyombo vya amani’!
Sikukuu njema kwenu nyote!
Kutoka Vatican 3 Agosti 2012
Jean-Louis Cardinal Tauran
Raisi
Askofu Mkuu Pier Lui Celata
Katibu
PONTIFICAL COUNCIL
FOR INTERRELIGIOUS DIALOGUE
00120 Vatican City
Telephone: 0039.06.6988 4321 / 06.6988 3648
Fax: 0039.06.6988 4494
E-mail: dialogo@interrel.va
|