Index

Back Top Print

[AR - BE - CS - DE - EN - ES - FR - IT - HU - LA - LV - PT - SW - ZH]

 

Konstitusio ya kidogma
juu ya Fumbo la Kanisa

Paulo Askofu
Mtumishi wa watumishi wa Mungu
pamoja na Mababa wa Mtaguso mkuu
ataka haya yakumbukwe daima

 

Sura ya Kwanza

FUMBO LA KANISA

Kanisa ni sakramenti katika Kristo

1. MWANGA WA MATAIFA (Lumen Gentium) ndiye Kristo. Ndiyo maana Mtaguso huu Mkuu, uliokusanyika katika Roho Mtakatifu, watamani mno kuwaangaza watu wote kwa mng’ao wake Kristo ung’arao juu ya uso wa Kanisa, kwa njia ya kuitangaza Injili kwa kila kiumbe (taz. Mk 16:15). Katika Kristo Kanisa ni kama sakramenti au ishara na chombo cha kuwaunganisha watu kiundani na Mungu na kuleta umoja kati ya wanadamu wote. Kwa hiyo [Mtaguso huu], ukiendeleza mafundisho ya Mitaguso iliyotangulia, unadhamiria kuwaeleza kinaganaga zaidi waamini wake na ulimwengu wote pia, maumbile yake na utume wake kwa ajili ya watu wote. Mazingira ya nyakati hizi yanafanya wajibu huu wa Kanisa uwe wa sharti zaidi sasa hivi, ili watu wote wanaozidi kuunganika siku za leo kwa vifungo vya kijamii, kiteknolojia na kiutamaduni, wapate kuufikia pia umoja kamili ndani ya Kristo.

Azimio la wokovu la Mungu Baba kwa ajili ya ulimwengu wote

2. Baba wa milele aliumba ulimwengu kwa azimio la hiari na la siri lenye hekima na wema, akaamua kuwainua wanadamu hadi kuwashirikisha uhai wake wa kimungu. Na pindi wanadamu walipoanguka katika Adamu, hakuwaacha kabisa, bali aliwapatia sikuzote misaada ya wokovu kwa kumtazamia Kristo Mkombozi “ambaye yu mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” (Kol 1:15). Maana wale wote walio wateule wake tangu milele, Mungu Baba “aliwajua, akawachagua wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi” (Rum 8:29). Tena, [Baba] aliazimia kuwakusanya [wote] wamwaminio Kristo katika Kanisa takatifu, lililoashiriwa (praefigurata) tangu mwanzo wa ulimwengu, na kutayarishwa kwa namna ya ajabu katika historia ya taifa la Israeli na katika agano la kale[1]. Katika nyakati za mwisho [Kanisa hilo] liliwekwa na kudhihirishwa kwa mmiminiko wa Roho Mtakatifu, na tena mwishoni mwa karne litakamilishwa kwa utukufu. Hapo, kama walivyoandika Mababa watakatifu wa Kanisa, wote wenye haki, kuanzia Adamu, “na tangu Abili hata mteule wa mwisho”[2], watakusanyika aliko Baba ndani ya Kanisa zima (Ecclesia universali).

Utume na kazi ya Mwana

3. Basi akaja Mwana ametumwa na Baba, naye Baba ndiye aliyetuteua katika Yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, akatangulia kutuchagua ili tufanywe wanawe; kwa maana ilimpendeza Baba kuvijumlisha vitu vyote katika Yeye (taz. Efe 1:4-5 na 10). Hivyo Kristo, ili kuyatimiza mapenzi ya Baba, akauzindua ufalme wa mbinguni hapa duniani, akatufunulia mafumbo yake Baba, akafanya ukombozi kwa utii wake. Kanisa, ambalo ndilo ufalme wa Kristo uliopo tangu sasa kati yetu katika fumbo, linakua wazi hapa duniani kwa uwezo wa Mungu. Mwanzo na kukua kwa Kanisa vimeonyeshwa kwa ishara za damu na maji zilizotoka katika ubavu uliochomwa wa Yesu msulibiwa (taz. Yn 19:34); vivyo hivyo vimebashiriwa na maneno ya Bwana yahusuyo kifo chake msalabani, “Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu” (Yn 12:32). Kila mara inapoadhimishwa altareni sadaka ya msalaba – ambayo kwayo “Kristo Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka” (1Kor 5:7) – kazi ya ukombozi yatekelezwa. Pamoja na hayo, kwa sakramenti ya mkate wa Ekaristi hudokezwa na kuundwa umoja wa waamini walio mwili mmoja katika Kristo (taz. 1Kor 10:17). Watu wote wanaitwa katika umoja huo na Kristo aliye nuru ya ulimwengu; nasi tunatoka kwake Yeye, tunaishi kwa ajili yake, na kumwelekea Yeye.

Roho Mtakatifu hulitakatifuza Kanisa

 4. Pale ilipotimilika kazi Baba aliyomkabidhi Mwana afanye duniani (taz. Yn 17:4), basi Roho Mtakatifu akatumwa siku ya Pentekoste ili kulitakatifuza Kanisa siku hadi siku, na waamini wapate njia ya kumkaribia Baba kwa Kristo katika Roho mmoja (taz. Efe 2:18). Huyo ndiye Roho wa uzima au chemchemi ya maji yabubujikiayo uzima wa milele (taz. Yn 4:14; 7:38-39). Kwa njia yake Baba anawahuisha wanadamu, walio wafu kwa sababu ya dhambi, mpaka atakapofufua ndani ya Kristo [pia] miili yao iliyo katika hali ya kufa (taz. Rum 8:10-11). Roho hukaa ndani ya Kanisa na ndani ya mioyo ya waamini kama katika hekalu (taz. 1Kor 3:16; 6:19); naye huomba ndani yao na kushuhudia ya kuwa walifanywa kuwa wana (taz. Gal 4:6; Rum 8:15-16 na 26). Naye huliongoza Kanisa kwenye kweli yote (taz. Yn 16:13), hulifanya kuwa moja katika ushirika na huduma, na kulifadhili vipawa mbalimbali vya kihierarkia na vya kikarama, ambavyo kwavyo huliongoza na kulipamba kwa matunda yake (taz. Efe 4:11-12; 1Kor 12:4; Gal 5:22). Kwa nguvu ya Injili hulitia tena Kanisa ujana wake, hulitengeneza upya daima na kuliongoza lipate kuunganika kikamilifu na Bwanaarusi wake[3]. Maana Roho na Bibiarusi wamwambia Bwana Yesu, “Njoo!” (taz. Ufu 22:17).

Hivyo Kanisa zima ulimwenguni linajionyesha kuwa “taifa lililokusanywa na umoja wa Baba, wa Mwana na wa Roho Mtakatifu”[4].

Ufalme wa Mungu

5. Fumbo la Kanisa takatifu linajidhihirisha katika kuanzishwa kwake lenyewe. Maana Bwana Yesu alianzisha Kanisa lake kwa kuihubiri habari njema, yaani ujio wa ufalme wa Mungu, ulioahidiwa tangu karne nyingi katika Maandiko: “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia” (Mk 1:15; taz. Mt 4:17). Ufalme huo unang’aa wazi mbele ya watu katika Neno la Kristo, katika matendo yake na uwepo wake. Neno la Bwana linafananishwa na mbegu iliyopandwa shambani (taz. Mk 4:14): wanaolisikiliza kwa imani na kuhesabiwa katika kundi dogo la Kristo (taz. Lk 12:32) wameupokea ufalme wenyewe wa Mungu. Halafu mbegu hiyo, kwa nguvu yake yenyewe, ikamea na kukua hata wakati wa mavuno (taz. Mk 4:26-29). Hata miujiza ya Yesu yathibitisha ya kuwa ufalme umekwisha fika duniani: “Ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia” (Lk 11:20; taz. Mt 12:28). Lakini kwanza kabisa ufalme wajionyesha katika nafsi ya Kristo mwenyewe aliye Mwana wa Mungu na Mwana wa Adamu, ambaye alikuja “kutumika na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi” (Mk 10:45).

Na hatimaye Yesu alipofufuka, baada ya kufa msalabani kwa ajili ya wanadamu, alijidhihirisha ya kuwa amewekwa kuwa Bwana na Kristo na Kuhani milele (taz. Mdo 2:36; Ebr 5:6; 7:17-21), akawamwagia wanafunzi wake Roho Mtakatifu aliyeahidiwa na Baba (taz. Mdo 2:33). Hivyo Kanisa ambalo lilijaliwa vipaji vyema vya Mwanzilishi wake na kushika kwa uaminifu amri zake za upendo, unyenyekevu na kujitolea, lakabidhiwa utume wa kuutangaza ufalme wa Kristo na wa Mungu, na kuusimika kati ya mataifa. Nalo Kanisa hapa duniani li chipukizi na chanzo cha ufalme huo. Wakati linapokua polepole lautazamia kwa shauku ufalme mkamilifu, na kwa nguvu zake zote latumaini na kutamani kujiunga na Mfalme wake katika utukufu.

Mifano ya Kanisa

6. Katika Agano la kale ufunuo wa ufalme wa Mungu umetolewa mara nyingi kwa njia ya mifano. Vivyo hivyo sasa maumbile ya ndani ya Kanisa hujidhihirisha kwetu kwa ishara mbalimbali, zitokanazo na maisha ya wachungaji na wakulima, kama vile na kazi ya kujenga, au na maisha ya familia na arusi. Na ishara hizo zimewahi kutayarishwa katika vitabu vya Manabii.

Hivyo Kanisa ni zizi, ambalo mlango wake mmoja tu na wa lazima ndiye Kristo (taz. Yn 10:1-10). Nalo ni pia kundi la kondoo, ambalo Mungu mwenyewe alihubiri tangu zamani ya kwamba atakuwa mchungaji wake (taz. Isa 40:11; Eze 34:11nk). Kondoo wake, ijapokuwa wanachungwa na wanadamu, huongozwa na kulishwa na Kristo mwenyewe aliye Mchungaji mwema na Mkuu wa wachungaji (taz. Yn 10:11; 1Pet 5:4), ambaye aliutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo (taz. Yn 10:11-15).

Kanisa ni ardhi iliyolimwa, ni shamba la Mungu (taz. 1Kor 3:9). Katika shamba hilo mzeituni ule wa zamani hukua, ambao shina lake takatifu ni Mababu, na ndani yake upatanisho wa Wayahudi na wa Mataifa umeletwa na utaendelea kuletwa (taz. Rum 11:13-26). Mzeituni huu ulipandwa na Mkulima wa mbinguni kama shamba la mizabibu lililoteuliwa (taz. Mt 21:33-43//; Isa 5:1nk). Kristo ndiye mzabibu wa kweli anayeyajalia matawi, yaani sisi, uhai na uwezo wa kuzaa; nasi, kwa njia ya Kanisa, twakaa ndani yake, na pasipo yeye hatuwezi kufanya neno lolote (taz. Yn 15:1-5).

Mara nyingi zaidi Kanisa huitwa jengo la Mungu (taz. 1Kor 3:9). Bwana mwenyewe alijifananisha na jiwe walilokataa waashi, nalo lakini limekuwa jiwe kuu la pembeni (taz. Mt 21:42//; Mdo 4:11; 1Pet 2:7; Zab 118:22). Na Kanisa lilijengwa na Mitume juu ya msingi huo (taz. 1Kor 3:11), na kutoka kwake lapata uimara na muungano. Jengo hilo huelezwa kwa majina mbalimbali: nyumba ya Mungu (taz. 1Tim 3:15), inamokaa familia yake, maskani ya Mungu katika roho (taz. Efe 2:19-22), “maskani ya Mungu pamoja na wanadamu” (Ufu 21:3). Na hasa laitwa hekalu takatifu, ambalo ishara zake ni mahali patakatifu palipojengwa kwa mawe, ambalo limesifiwa na Mababa watakatifu, na katika Liturujia hufananishwa kwa haki na Mji mtakatifu, ndio Yerusalemu mpya[5]. Maana ndani yake sisi tumejengwa hapa duniani kama mawe yaliyo hai (taz. 1Pet 2:5). Mji huo mtakatifu Yohane anautazama, wakati ulimwengu unapofanywa upya, kama ulioshuka kutoka mbinguni kwa Mungu, nao umewekwa tayari kama Bibiarusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe (Ufu 21:1nk).

Hatimaye Kanisa huitwa pia “Yerusalemu ya juu” na “mama yetu” (Gal 4:26; taz. Ufu 12:17), na kuelezwa kama Bibiarusi asiye na mawaa wa Mwanakondoo asiye na mawaa (taz. Ufu 19:7; 21:2 na 9; 22:17). Kristo “alilipenda ...akajitoa kwa ajili yake, kusudi alitakase” (Efe 5:25-26), akaliunganisha naye kwa agano lisilovunjika, daima “analilisha na kulitunza” (Efe 5:29). Basi alipokwisha kulitakasa alitaka liunganike naye na kumtii katika upendo na uaminifu (taz. Efe 5:24); hatimaye akalijaza vipaji vya mbinguni hata milele ili sisi tupate kuujua upendo wa Mungu na wa Kristo kwa ajili yetu, upitao kila ufahamu (taz. Efe 3:19). Wakati Kanisa linaposafiri hapa duniani mbali na Bwana (taz. 2Kor 5:6), hujiona kuwa ni mgeni, hata likatafute na kuyazingatia yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu, ambapo uhai wa Kanisa umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu, mpaka [Kanisa] litakapofunuliwa pamoja na Bwana arusi wake katika utukufu (taz. Kol 3:1-4).

Kanisa ni mwili wa Kristo

7. Mwana wa Mungu, katika hali ya kibinadamu aliyofungamana nayo, aliposhinda mauti kwa kifo chake na ufufuko wake, alimkomboa mwanadamu, akamgeuza kuwa kiumbe kipya (taz. Gal 6:15; 2Kor 5:17). Maana kwa kuwashirikisha Roho wake, anawafanya ndugu zake waitwao kutoka katika mataifa yote kuwa mwili wake katika fumbo.

Ndani ya mwili huo uhai wa Kristo hutiwa katika waamini, ambao kwa njia ya sakramenti wanaunganishwa, kwa jinsi ya siri na ya kweli, na Kristo aliyeteswa na kutukuzwa[6]. Maana kwa ubatizo tumefananishwa na Kristo: “Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja” (1Kor 12:13). Katika ibada hii takatifu ushirikiano wetu na kifo cha Kristo na ufufuko wake huonyeshwa kwa ishara na kutekelezwa: “Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake”; na “kama tulivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika tutaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake” (Rum 6:4-5). Kwa kushiriki kweli mwili wa Bwana katika kumega mkate wa Ekaristi, twainuliwa hadi tuufikie ushirikiano naye na kati yetu, “Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja” (1Kor 10:17). Hivyo sisi sote tumekuwa viungo vya mwili ule (taz. 1Kor 12:27), “na sisi tu viungo, kila mmoja kwa mwenzake” (Rum 12:5).

Kama vile viungo vyote vya mwili wa kibinadamu, ijapo ni vingi, ni mwili mmoja, vivyo hivyo na waamini katika Kristo (taz. 1Kor 12:12). Hata katika kujenga mwili wa Kristo kuna tofauti za viungo na za kazi zake. Roho ni mmoja agawiaye karama zake mbalimbali kwa ajili ya manufaa ya Kanisa, kadiri ya utajiri wake mwenyewe na hitaji la huduma. Neema waliyopewa Mitume ni bora zaidi kati ya karama hizo, na Roho mwenyewe aliwatiisha chini ya mamlaka yao pia wale waliojaliwa karama za pekee (taz. 1Kor 14). Roho huyohuyo akiunganisha katika umoja mwili huu, kwa njia yake mwenyewe, kwa uweza wake na kwa muungano wa ndani wa viungo vyake, hutengeneza na kuchochea umoja kati ya waamini. Kwa hiyo kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho (taz. 1Kor 12:26).

Kichwa cha mwili huo ndiye Kristo. Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, na katika yeye vitu vyote viliumbwa. Yeye amekuwako kabla ya vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye. Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha Kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote (taz. Kol 1:15-18). Kwa ukuu wa uweza wake atawala juu ya vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani, na kwa ukamilifu wake upitao vyote na kwa utendaji wake aujaza mwili wote kwa utajiri wa utukufu wake (taz. Efe 1:18-23)[7].

Viungo vyote lazima viundwe ili kufanana na Kristo, hata yeye aumbike ndani yao (Gal 4:19). Kwa sababu hiyo sisi, tuliopata kufanana naye, tuliokufa pamoja naye na kufufuliwa pamoja naye, tumeingizwa katika mafumbo ya maisha yake, hata tutakapotawala pamoja naye (taz. Flp 3:21; 2Tim 2:11; Efe 2:6; Kol 2:12; n.k.). Nasi tungali wasafiri bado hapa duniani, tunapofuata nyayo zake katika dhiki na dhuluma, tunaunganishwa na mateso yake kama vile mwili unavyounganika na kichwa, na tunateswa pamoja naye ili tupate kutukuzwa pamoja naye (taz. Rum 8:17).

“Kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu” ( Kol 2:19). Yeye katika mwili wake, yaani Kanisa, anagawa daima karama za huduma. Nasi kwa msaada wa karama hizi tunatumikiana sisi kwa sisi kwa nguvu yake mwenyewe, ili tuokoke, na tukiushika ukweli katika mapendo tukue hata tumfikie yeye katika yote, aliye kichwa chetu (taz. Efe 4:11-16).

Aidha ili tufanywe wapya daima ndani yake (taz. Efe 4:23), alitushirikisha Roho wake ambaye ni mmoja na yuleyule katika kichwa na katika viungo. Naye Roho huuhuisha na kuungamanisha na kuusukuma mwili wote hivi kwamba kazi yake ilifananishwa na Mababa watakatifu na kazi itendayo roho ndani ya mwili wa mtu, ambayo ndiyo asili ya uzima wake[8].

Kristo analipenda Kanisa kama Bibiarusi wake, akawa mfano wa mume anayempenda mke wake kama mwili wake mwenyewe (taz. Efe 5:25-28). Kwa upande wake Kanisa hukitii kichwa chake (taz. Efe 5:23-24). Maadamu “katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu kwa jinsi ya kimwili” (Kol 2:9), basi utimilifu wake hulijaza Kanisa, lililo mwili wake na utimilifu wake, kwa vipaji vyake vya kimungu (taz. Efe 1:22-23), ili lipate kuuelekea na kuufikia utimilifu wote wa Mungu (taz. Efe 3:19).

Kanisa lionekanalo na lisiloonekana

8. Kristo, aliye mshenga pekee, aliliweka duniani Kanisa lake takatifu, lililo jumuiya ya imani, matumaini na mapendo, kama muundo (compaginem) unaoonekana; na daima hulilisha[9] na kwa njia yake hueneza kwa watu wote ukweli na neema. Jamii iliyoundwa na viungo vya kihierarkia na mwili wa fumbo la Kristo; kusanyiko linaloonekana na jumuiya ya kiroho; Kanisa lililopo duniani na Kanisa lililokwisha pata urithi wa mema mbinguni; mambo hayo yasihesabiwe kuwa ni mambo mawili tofauti, bali ni jambo moja tu, changamano linalounganisha sehemu moja ya kibinadamu na sehemu nyingine ya kimungu[10]. Kwa hiyo kwa ulinganifu ulio mzuri Kanisa hufananishwa na fumbo la Neno lililofanyika mwili. Maana, kama vile maumbile [ya kibinadamu] yaliyotwaliwa na Neno wa Mungu na kuunganika naye kwa njia isiyotengeka yanavyomtumikia kama chombo cha wokovu chenye uhai, vivyo hivyo muundo wa kijamii wa Kanisa unamtumikia Roho wa Kristo anayeuhuisha, kwa ajili ya kuukuza mwili (taz. Efe 4:16)[11].

Hilo ndilo Kanisa pekee la Kristo tunalolikiri katika kanuni ya imani kwamba ni moja, takatifu, katoliki na la mitume[12]. Mwokozi wetu, baada ya ufufuko wake, alilikabidhi kwa Petro ili alilishe (taz. Yn 21:17); akamwagiza yeye na mitume wengine walieneze na kuliongoza (taz. Mt 28:18 n.k.); akaliweka kwa nyakati zote kama nguzo na msingi wa kweli (taz. 1Tim 3:15). Kanisa hilo, lililoundwa na kupangwa kama jamii katika ulimwengu huu, linaendelea kuwepo (subsistit) katika Kanisa katoliki, linalotawaliwa (gubernata) na Halifa wa Petro na Maaskofu katika ushirika naye[13]. Lakini pia nje ya muundo huu unaoonekana, hupatikana mambo mengi ya kutakatifuza na ya ukweli, ambayo, kama vipaji vilivyo mali ya Kanisa la Kristo, husukuma kwenye umoja wa kikatoliki.

Kama vile Kristo alivyotimiza kazi yake ya ukombozi katika hali ya umaskini na madhulumu, vivyo hivyo Kanisa laitwa kushika njia hiyohiyo ili kuwashirikisha watu matunda ya wokovu. Yesu Kristo “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu...alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa” (Flp 2:6-7); na kwa ajili yetu “ingawa alikuwa tajiri, akajifanya maskini” (2Kor 8:9). Vilevile Kanisa, ingawa linahitaji misaada ya wanadamu kwa kutekeleza utume wake, halikuwekwa ili kutafuta utukufu wa kidunia, bali kusudi lifahamishe [pote] unyenyekevu na roho ya kujihinisha (abnegationem), hata kwa kutoa mfano wake lenyewe. Kristo alitumwa na Baba “kuwahubiri maskini habari njema...kuwaponya waliovunjika moyo” (Lk 4:18), na “kutafuta na kuokoa kilichopotea” (Lk 19:10). Vivyo hivyo Kanisa huwahurumia kwa mapendo yake wanaotaabika kwa udhaifu wa kibinadamu; zaidi hutambua katika maskini na wateswa sura ya Mwasisi wake aliyekuwa naye maskini na mteswa; tena hujishughulisha kuinua umaskini wao, na hunuia kumtumikia Kristo ndani yao. Kristo aliye “mtakatifu, asiye na uovu, asiye na waa lolote” (Ebr 7:26), hakujua dhambi (taz. 2Kor 5:21), bali alikuja tu “ili afanye suluhu kwa dhambi za watu” (taz. Ebr 2:17). Lakini Kanisa, ambalo huwakumbatia wakosefu ndani yake, na wakati uleule ni takatifu na linahitaji kutakaswa, haliachi kamwe kutubu na kujitengeneza upya.

Kanisa “linaendelea mbele katika kuhiji kwake katikati ya madhulumu ya ulimwengu na faraja za Mungu”[14], likitangaza msalaba na mauti ya Bwana hata ajapo (taz. 1Kor 11:26). Kwa uwezo wa Bwana aliyefufuka linapata nguvu ya kuzishinda, kwa saburi na upendo, taabu na shida za ndani na za nje, na ya kuufunulia ulimwengu, kwa uaminifu, fumbo la Bwana, ingawa bado lipo katika kivuli, mpaka mwisho wa nyakati litakapodhihirishwa katika ukamilifu wa mwanga wake.

Sura ya Pili

TAIFA LA MUNGU

Agano jipya na taifa jipya

9. Kila wakati na katika kila taifa mtu amchaye Mungu na kutenda haki hukubaliwa na yeye (taz. Mdo 10:35). Lakini ilimpendeza Mungu kuwatakatifuza na kuwaokoa watu, siyo mmoja mmoja na pasipo muungano kati yao, bali kwa kuwaunda kama taifa moja, lenye kumjua katika ukweli na kumtumikia kitakatifu. Kwa hiyo alijichagulia watu wa Israeli kuwa taifa lake, akafunga agano na taifa hilo, akalifundisha polepole kwa kujidhihirisha katika historia yake yeye mwenyewe na kufunulia kusudio la mapenzi yake, naye akaliweka wakfu kwa ajili yake. Lakini hayo yote yalitokea kama matayarisho na mfano wa lile agano lililo jipya na kamilifu ambalo lilitakiwa kufungwa katika Kristo, na wa ule ufunuo mtimilifu wa kuletwa na Neno wa Mungu mwenyewe aliyejifanya mwili. “Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda... Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu... Watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao, hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema Bwana” (Yer 31:31-34). Kristo aliliweka agano hilo jipya, yaani Agano Jipya katika damu yake (taz. 1Kor 11:25), akiwaita watu kutoka Wayahudi na mataifa, ili waungane siyo kwa kadiri ya mwili, bali katika Roho, na wawe taifa jipya la Mungu. Maana wamwaminio Kristo waliozaliwa mara ya pili, si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika, kwa Neno la Mungu lenye uzima (taz. 1Pet 1:23), si kwa mwili, bali kwa maji na kwa Roho Mtakatifu (taz. Yn 3:5-6); hawa walifanywa kuwa “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu... waliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu” (1Pet 2:9-10).

Kichwa cha taifa hili la kimasiya ni Kristo, “ambaye alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili tupate kuhesabiwa haki” (Rum 4:25). Naye sasa atawala kwa utukufu mbinguni, baada ya kupata jina lipitalo kila jina. Taifa hilo, hali yake ni heshima na uhuru wa watoto wa Mungu, ambao ndani ya mioyo yao Roho Mtakatifu hukaa kama katika hekalu lake. Sheria yake ni amri mpya ya kupendana kama Kristo mwenyewe alivyotupenda (taz. Yn 13:34). Na hatimaye kikomo chake ndicho ufalme wa Mungu, ulioanzishwa duniani na Mungu mwenyewe, na unaopaswa kupanuliwa zaidi hata utimizwe naye mwisho wa nyakati, Kristo atakapofunuliwa, aliye uhai wetu (taz. Kol 3:4), na “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu” (Rum 8:21). Kwa hiyo taifa hili la kimasiya, ijapo kwa kweli halijawachukua ndani yake watu wote, na mara nyingi huonekana kuwa kundi dogo tu, lakini ni mbegu thabiti sana ya umoja, tumaini na wokovu kwa jamii nzima ya wanadamu. Nalo limewekwa na Kristo katika ushirika wa maisha, wa upendo na wa ukweli, likatwaliwa naye kuwa chombo cha ukombozi wa watu wote, likatumwa ulimwenguni mwote kuwa nuru ya ulimwengu na chumvi ya dunia (taz. Mt 5:13-16).

Kama vile taifa la Israeli kadiri ya mwili lenye kutangatanga jangwani, lilivyoitwa Kanisa la Mungu (taz. Neh 13:1; Hes 20:4; Kum 23:1nk), vivyo hivyo taifa jipya la Israeli lenye kusafiri wakati huu likiutafuta mji ujao na udumuo (taz. Ebr 13:14), huitwa Kanisa la Kristo (taz. Mt 16:18). Kristo alilinunua kwa damu yake mwenyewe (taz. Mdo 20:28), akalijaza Roho wake, akalijalia misaada inayofaa kwa ajili ya umoja uonekanao na wa kijamii. Mungu alikusanya kusanyiko la wenye kumtazama kwa imani Yesu aliye mtendaji wa wokovu na asili ya umoja na amani; naye akawaweka kuwa Kanisa ili Kanisa hilo liwe, kwa ajili ya wote na kwa kila mmoja, sakramenti inayoonekana ya umoja huu uletao wokovu[15]. Kanisa, likitakiwa kuenea mahali pote, huingia katika historia ya watu, lakini wakati huohuo linavuka mipaka ya nyakati na ya mataifa. Kanisa hilo likisafiri katika majaribu na dhiki hutiwa nguvu na uwezo wa neema ya Mungu iliyoahidiwa na Bwana, lisije likatindikiwa uaminifu kamili kwa ajili ya udhaifu wa kibinadamu, bali lidumu kuwa Bibiarusi stahivu wa Bwana wake; wala lisiache kujitengeneza upya kwa msaada wa Roho Mtakatifu, hadi liifikie, kwa njia ya msalaba, nuru isiyojua kuchwa.

Ukuhani wa waamini wote

10. Kristo Bwana ndiye Kuhani Mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu (taz. Ebr 5:1-5), alilifanya taifa hili jipya kuwa “ufalme na makuhani kwa Mungu Baba yake” (Ufu 1:6; taz. 5:9-10). Maana, kwa kuzaliwa mara ya pili na kupakwa mafuta ya Roho Mtakatifu, waliobatizwa wanawekwa wakfu kuwa makao ya kiroho na ukuhani mtakatifu, ili kutoa dhabihu za kiroho kwa njia ya matendo yote ya kila mkristo, na kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita watoke gizani na waingie katika nuru yake ya ajabu (taz. 1Pet 2:4-10). Kwa hiyo wanafunzi wote wa Kristo, wakidumu katika kusali na kumsifu Mungu pamoja (taz. Mdo 2:42-47), wajitoe wenyewe wawe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu (taz. Rum 12:1); tena wamshuhudie Kristo popote duniani na wamjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini la uzima wa milele lililo ndani yao (taz. 1Pet 3:15).

Ukuhani wa waamini wote na ukuhani wa kidaraja au wa kihierarkia, ingawa huhitilafiana kadiri ya kiini chake na siyo kadiri ya cheo tu, huelekezana kati yake kwa sababu zote mbili, na kila mmoja kwa namna yake, hushiriki ukuhani mmoja wa Kristo[16]. Kuhani wa kidaraja, kwa mamlaka takatifu aliyo nayo, hulea na kuliongoza taifa la kikuhani, huadhimisha sadaka ya Ekaristi katika nafsi ya Kristo na kuitolea kwa Mungu kwa jina la taifa lote. Waamini wanashiriki sadaka ya Ekaristi kwa nguvu ya ukuhani wao wa kifalme[17], watekeleza ukuhani huo kwa kupokea sakramenti, kusali na kutoa shukrani, kwa ushuhuda wa maisha matakatifu, kwa kujikana na kwa upendo wenye utendaji.

Kutekelezwa kwa ukuhani wa waamini wote katika sakramenti

11. Tabia takatifu ya jumuiya ya kikuhani inatekelezwa, pamoja na muundo wake wenye utaratibu, kwa njia ya sakramenti na fadhila. Waamini, waliofanywa kuwa viungo vya Kanisa kwa ubatizo, kwa muhuri (charactere) wa ubatizo wameteuliwa na wameagizwa kutoa ibada ya dini ya kikristo, na maadamu walizaliwa upya kuwa watoto wa Mungu, yawapasa kuikiri mbele ya watu imani waliyoipokea kwa Mungu kwa njia ya Kanisa[18]. Kwa sakramenti ya kipaimara waunganishwa na Kanisa kikamilifu zaidi na kujaliwa nguvu ya pekee ya Roho Mtakatifu; kwa hiyo wanawajibika zaidi kuieneza na kuitetea imani kwa neno na kwa matendo, kama mashahidi wa kweli wa Kristo[19]. Wakishiriki sadaka ya Ekaristi, iliyo chemchemi na kilele cha maisha yote ya kikristo, wanamtolea Mungu dhabihu ya kimungu na kujitoa wenyewe pamoja nayo[20]. Hivyo wote, kwa kutoa sadaka au kwa kupokea Komunyo takatifu, wanatenda kazi yao katika Liturujia, wala si wote sawasawa, bali kila mmoja kwa namna yake. Tena wakiimarishwa kwa kula mwili wa Kristo katika kusanyiko (synaxi) takatifu, wadhihirisha wazi umoja wa taifa la Mungu, ambao huonyeshwa kwa jinsi ifaayo na kufanyizwa kwa namna ya ajabu kwa sakramenti hii tukufu sana.

Wanaoijongea sakramenti ya kitubio hupokea humo kutoka huruma ya Mungu ondoleo la makosa yaliyotendwa dhidi yake, na papo hapo hupatanishwa na Kanisa, ambalo dhambi yao imelijeruhi, na ambalo kwa mapendo, mfano na sala huhangaikia wongofu wao. Kwa mpako mtakatifu wa wagonjwa na sala ya mapadre, Kanisa lote linawakabidhi wagonjwa kwa Bwana aliyeteswa na kutukuzwa, ili awainue na kuwaokoa (taz. Yak 5:14-16); waama linawasihi hasa wajiunge kwa hiari na mateso na kifo cha Bwana (taz. Rum 8:17; Kol 1:24; 2Tim 2:11-12; 1Pet 4:13), ili walifaidie taifa la Mungu. Tena, wale miongoni mwa waamini wanaopokea Daraja takatifu, wanawekwa kwa jina la Kristo kulichunga Kanisa kwa Neno la Mungu na neema yake. Na hatimaye, wakristo wafunga ndoa, ambao kwa nguvu ya sakramenti yao ya ndoa waisharisha na kulishiriki fumbo la umoja na la upendo wenye kuzaa kati ya Kristo na Kanisa (taz. Efe 5:32), wanasaidiana kuufikia utakatifu katika maisha ya ndoa na katika kuwapokea na kuwalea watoto wao; kwa hiyo katika hali na hadhi ya maisha yao wana karama yao ya pekee ndani ya taifa la Mungu[21]. Maana katika ndoa hii hutokea familia ambayo ndani yake wanazaliwa raia wapya wa jamii ya kibinadamu, ambao kwa neema ya Roho Mtakatifu wanafanywa kuwa watoto wa Mungu kwa ubatizo, ili kuliendeleza taifa lake Mungu karne kwa karne. Katika familia, iliyo kama Kanisa la kinyumbani, yawapasa wazazi kuwa watangazaji wa kwanza wa imani kwa ajili ya watoto wao, kwa neno na mfano wao, na kusaidia wito maalum wa kila mmoja, na kwa uangalifu wa pekee hasa ule wito mtakatifu.

Kwa kuimarika na misaada ya wokovu mingi namna hii na ya ajabu, waamini wote wa kila hali na hadhi wanaitwa na Bwana, kila mmoja kwa njia yake, kwenye ukamilifu wa utakatifu kama Baba mwenyewe alivyo mtakatifu.

Hisia ya imani na karama katika taifa la Mungu

12. Taifa takatifu la Mungu laishiriki pia kazi ya unabii wa Kristo, linapoueneza ushuhuda wake ulio hai hasa kwa njia ya maisha ya imani na upendo, na kumpa Mungu dhabihu ya sifa, tunda la midomo iliungamayo jina lake (taz. Ebr 13:15). Waamini wote waliopakwa mafuta na Yeye aliye Mtakatifu (taz. 1Yoh 2:20 na 27) hawawezi kukosa katika mambo ya imani; nao hudhihirisha tabia yao hiyo ya pekee, isiyo ya dunia hii, kwa njia ya utambuzi wa imani (sensu fidei) ya taifa lote, pale ambapo “kuanzia maaskofu hadi waamini walei wa mwisho”[22] wanaonyesha makubaliano (consensum) ya wote kuhusu mambo ya imani na ya adili. Maana kwa hisia hiyo ya imani iliyoamshwa na kutegemezwa na Roho wa ukweli, taifa la Mungu, chini ya uongozi wa Majisterio takatifu linayoifuata kwa uaminifu, hulipokea si neno la wanadamu, bali hakika Neno la Mungu (taz. 1The 2:13). Tena huishika daima “imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu” (Yda 3), na kwa hukumu iliyo nyofu huipenya kwa undani zaidi na kuitia kikamilifu katika maisha yake.

Na Roho Mtakatifu mwenyewe, licha ya kutakatifuza taifa la Mungu na kuliongoza na kulipamba kwa fadhila mbalimbali kwa njia ya sakramenti na huduma, atoa pia karama za pekee miongoni mwa waamini wa kila hadhi kwa “kumgawia kila mtu peke yake karama zake kama apendavyo yeye” (1Kor 12:11); na kusudi lake ndilo kuwafanya wafae na kuwa tayari kuzishika kazi na huduma mbalimbali zenye kuleta manufaa kwa ajili ya matengenezo ya Kanisa na maongezo yake, kadiri ilivyoandikwa, “Kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana” (1Kor 12:7). Karama hizo zisizo za kawaida au zile za kawaida ambazo zimesambazwa kwa kiasi kikubwa, hazina budi kupokelewa kwa shukrani na faraja, maadamu ni zenye kufaa sana na kusaidia kwa mahitaji ya Kanisa. Lakini karama hizi zisizo za kawaida zisiombwe bila uchaji, wala matunda ya kazi za kitume yasitumainiwe kwa ujuvi kutokana nazo. Lakini kuamua uhalisi wake na matumizi yake yenye utaratibu ni juu ya wale wanaosimamia katika Kanisa, ambao yawapasa hasa siyo kumzimisha Roho, bali kujaribu mambo yote na kulishika lililo jema (taz. 1The 5:12 na 19-21). 

Kuenea kwa taifa pekee la Mungu popote duniani

13. Watu wote waitwa kuliingia taifa jipya la Mungu. Kwa hiyo taifa hili, likiendelea kuwa moja na pekee, inabidi lienee ulimwenguni pote na kwa karne zote, ili litimizwe azimio la mapenzi ya Mungu, ambaye awali aliumba maumbile ya kibinadamu kuwa kitu kimoja, akaamua kuwakusanya watoto wake waliotawanyika ili wawe wamoja (taz. Yn 11:52). Kwa kusudi hilo Mungu akamtuma Mwanae, aliyemweka kuwa mrithi wa yote (taz. Ebr 1:2), ili awe Mwalimu, Mfalme na Kuhani wa watu wote, kichwa cha taifa jipya na la popote duniani la watoto wa Mungu. Ndiyo sababu Mungu akamtuma pia Roho wa Mwanae, aliye Bwana na Mleta uzima, ambaye ndiye asili ya muungano na umoja kwa Kanisa zima na kwa waamini wote na kwa kila mmoja wao, katika fundisho la Mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali (taz. Mdo 2:42).

Hivyo taifa lile moja la Mungu lipo sasa katika mataifa yote ya dunia, maadamu Mungu hutwaa katika mataifa raia wake, walio raia wa ufalme ambao kwa maumbile yake si wa kidunia, bali wa kimbingu. Kwa hiyo waamini wote waliotawanyika ulimwenguni washirikiana wao kwa wao katika Roho Mtakatifu, na hivyo “yule akaaye Rumi ajua kuwa Wahindi ni viungo vyake”[23]. Lakini, maadamu ufalme wa Kristo si wa ulimwengu huu (taz. Yn 18:36), Kanisa au taifa la Mungu liletalo ufalme huu, halilinyimi taifa lolote chochote cha mali yake ya kidunia, bali kinyume chake husaidia na kupokea uwezo, utajiri na desturi vya mataifa, kwa kadiri vilivyo vyema, na katika kuvipokea huvitakasa, huviimarisha na kuviinua. Maana lakumbuka kwamba linapaswa kukusanya pamoja na Mfalme yule aliyepewa mataifa kuwa urithi wake (taz. Zab 2:8), nayo mataifa yanaleta vipawa vyao na sadaka zao katika mji wake (taz. Zab 72:10; Isa 60:4-7; Ufu 21:24). Tabia hii, ya kuenea pote duniani, ilipambayo taifa la Mungu ndiyo kipaji cha Bwana mwenyewe, na kwa njia yake Kanisa katoliki, kwa mafanikio na bila kukoma, laelekea kuwajumlisha wanadamu wote pamoja na mema yao yote chini ya Kristo aliye kichwa, katika umoja wa Roho wake[24].

Kwa nguvu ya ukatoliki (catholicitatis) huu kila sehemu huvipeleka vipaji vyake yenyewe kwa sehemu nyingine na kwa Kanisa lote, hivi kwamba sehemu zote pamoja, na kila moja pia, hukithiri kwa kushirikiana zenyewe kwa zenyewe na kufanya juhudi ili kupata ukamilifu katika umoja. Tokea hapo yajiri kuwa taifa la Mungu, licha ya kujikusanya kutoka katika mataifa mbalimbali, ndani yake lenyewe pia linajipanga kwa madaraja mbalimbali. Kwa maana kati ya viungo vyake kuna utofauti wa kazi, kwani wengine wanatumikia kwa huduma takatifu kwa ajili ya manufaa ya ndugu zao, au tena kuna utofauti wa hali na mpango wa maisha, kwani wengi katika hali ya kitawa wanawachochea ndugu kwa mfano wao wakinuia kuufikia utakatifu kwa njia nyembamba zaidi. Hivyo katika ushirika wa kikanisa yapo pia kwa halali Makanisa maalum (Ecclesiae particulares) yashikayo mapokeo yao yenyewe, bila kuathiri mamlaka kuu ya Kiti cha Petro kinachosimamia ushirika wote wa mapendo[25], hulinda tofauti za haki zilizopo, na wakati uleule huangalia ili yaliyo ya pekee yasidhuru umoja bali yautumikie zaidi. Na hatimaye, kutokana na hayo, vinakuwepo vifungu vya ushirika wa kindani kati ya sehemu mbalimbali za Kanisa kuhusu utajiri wa kiroho, wafanyakazi wa kitume na misaada ya kidunia. Kwa maana viungo vya taifa la Mungu vyaitwa kushirikiana katika mema, na maneno haya ya Mtume Paulo yahusu pia kila Kanisa, “Kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana, kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu” (1Pet 4:10).

Hivyo watu wote waitwa kwenye umoja huu wa kikatoliki wa taifa la Mungu, ambao huashiria na kuhamasisha amani timilifu. Na katika umoja huo kwa namna mbalimbali huhusianishwa au hukusudiwa kuingia waamini wakatoliki na hata wengine wamwaminio Kristo, na hatimaye pia watu wote wanaoitwa kwa neema ya Mungu kupata wokovu.

Waamini wakatoliki

14. Mtaguso huu mtakatifu huwaangalia kwanza waamini wakatoliki. Ukijitegemeza juu ya Maandiko Matakatifu na Mapokeo, [Mtaguso] hufundisha kuwa Kanisa hili linalohiji hapa duniani, ni la lazima kwa kupata wokovu. Maana Kristo peke yake ndiye Mshenga na njia ya wokovu, yeye ambaye yupo hapa kwa ajili yetu katika mwili wake, ulio Kanisa. Na Yeye mwenyewe alisisitiza kwa maneno wazi ulazima wa imani na ubatizo (taz. Mk 16:16; Yn 3:5), na papo hapo akathibitisha ulazima pia wa Kanisa, ambamo watu wanaingia kwa ubatizo kama kwa mlango. Kwa sababu hiyo, hawawezi kuokoka watu wale ambao, ingawa wanajua ya kwamba Kanisa katoliki limeasisiwa na Mungu kwa njia ya Yesu Kristo kama la lazima, wanakataa au kuingia ndani ya Kanisa au kudumu ndani yake.

Basi wanaingizwa kikamilifu katika jumuiya ya Kanisa wale ambao, wakiwa na Roho wa Kristo, wanakubali muundo wake mzima na njia zote za wokovu lilizopewa. Tena, katika mpangilio wake uonekanao, wanaunganika na Kristo – aliongozaye Kanisa kwa njia ya Baba Mtakatifu na Maaskofu – kwa vifungo vya ungamo la imani, sakramenti, uongozi wa Kanisa na ushirika. Lakini yule ambaye hadumu katika upendo na akaa ndani ya Kanisa kwa ‘mwili’ na si kwa ‘moyo’, ijapo ameingizwa katika Kanisa, hataokoka[26]. Basi, watoto wote wa Kanisa wakumbuke kuwa hali yao bora hutokana siyo na mastahili yao, bali na neema ya pekee ya Kristo. Ikiwa hawaiitikii neema hiyo kwa wazo, kwa neno na kwa tendo, sio tu hawataokoka, bali pia watahukumiwa kwa ukali zaidi[27].

Wakatekumeni ambao, wakiongozwa na Roho Mtakatifu, wanatamani kwa mapenzi dhahiri kuingizwa katika Kanisa, waunganishwa nalo kwa tamaa hiyo yenyewe, naye Mama Kanisa huwakumbatia tayari kama [wana] wake kwa upendo na matunzo.

Kanisa na wakristo wasio wakatoliki

15. Kanisa lajua kwamba limeunganika kwa sababu nyingi na wale waliobatizwa, ambao wamepewa heshima ya jina la wakristo, ingawa hawakiri imani iliyo kamili, au hawatunzi umoja wa ushirika chini ya Halifa wa Petro[28]. Kwa maana wapo wengi ambao huyaheshimu Maandiko Matakatifu kama kanuni ya imani na ya maisha, huonyesha juhudi ya kweli ya kidini, na kumwamini kwa upendo Mungu Baba Mwenyezi na Kristo aliye Mwana wa Mungu na Mwokozi[29]. Tena walitiwa muhuri wa ubatizo, ambao kwa njia yake wameunganishwa na Kristo, na zaidi wazikubali sakramenti nyingine pia na kuzipokea katika Makanisa yao au jumuiya za kikanisa. Wengi miongoni mwao wanao pia Uaskofu, huadhimisha Ekaristi Takatifu na kuwa na moyo wa ibada kwa ajili ya Bikira Mama wa Mungu[30]. Aidha kuna ushirika wa sala na fadhila nyingine za kiroho, na zaidi kuna hali ya umoja wa kweli katika Roho Mtakatifu, kwa kuwa Roho kwa nguvu yake iletayo utakatifu hutenda kazi pia ndani yao kwa njia ya vipawa na neema, tena baadhi yao akawatia nguvu hadi kumwaga damu yao. Hivyo Roho huchochea ndani ya wanafunzi wa Kristo hamu na matendo ili wote, kadiri ilivyopangwa na Kristo, wajiunge kwa amani katika kundi moja chini ya mchungaji mmoja[31]. Mama Kanisa hakomi kusali, kutumaini na kutenda ili kupata jambo hilo, tena huwasihi wanawe wajitakase na kujitengeneza upya, ili ishara ya Kristo ing’ae wazi zaidi juu ya uso wa Kanisa.

Kanisa na wasio wakristo

16. Hatimaye wale ambao hawajapokea Injili huhusiana na taifa la Mungu kwa njia mbalimbali[32]. Kwanza kabisa taifa lile, lililopewa maagano na ahadi, ambalo katika hilo alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili (taz. Rum 9:4-5). Hilo ndilo taifa lililo penzi kwa ajili ya Mababa zake, kwa habari ya kule kuchaguliwa, kwa sababu karama za Mungu hazina majuto, wala mwito wake (taz. Rum 11:28-29). Lakini mpango wa wokovu huwakumbatia pia wanaomtambua Muumba, na kati yao wa kwanza Waislamu: hao wakiri ya kuwa wanashika imani ya Ibrahimu, na pamoja nasi wanamwabudu Mungu mmoja, mwenye huruma, atakayewahukumu watu siku ya mwisho. Naye Mungu mwenyewe hayupo mbali na wengine wanaomtafuta katika vivuli na sanamu Mungu asiyejulikana, kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote (taz. Mdo 17:25-28), naye ndiye Mwokozi anayetaka watu wote waokolewe (taz. 1Tim 2:4). Kwa maana wanaweza kupata wokovu wa milele wale ambao, bila hatia, hawaifahamu Injili ya Kristo wala Kanisa lake, lakini hata hivyo wanamtafuta Mungu kwa moyo mnyofu, na kwa mvuto wa neema wanajitahidi kutimiza kwa matendo yao mapenzi ya Mungu wanayotambua kwa njia ya sauti ya dhamiri[33]. Maongozi ya Mungu hayakatai kuwapa misaada inayohitajika kwa ajili ya wokovu wale ambao, bila hatia yao, hawajaufikia ufahamu wazi wa Mungu, nao wanajitahidi, kwa neema ya Mungu, kuishi maisha manyofu. Kwa maana lolote lililo jema na la kweli lipatikanalo kati yao, lahesabiwa na Kanisa kuwa kama matayarisho ya Injili[34], na limetolewa na Yule amwangazaye kila mtu ili mwishowe apate uzima. Lakini mara nyingi wanadamu, wakidanganywa na Ibilisi, walipotea katika mawazo yao, wakaibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakiabudu kiumbe badala ya Muumba (taz. Rum 1:21 na 25). Au tena wakiishi na kufa pasipo Mungu hapa duniani, wanaelekea mwishoni kukata tamaa. Kwa hiyo Kanisa, likikumbuka amri ya Bwana: “Hubirini Injili kwa kila kiumbe” (Mk 16:15), husitawisha kwa uangalifu mkuu misioni, kwa ajili ya utukufu wa Mungu na wokovu wa watu hawa wote.

Tabia ya kimisionari ya Kanisa

17. Maana kama Mwana alivyotumwa na Baba, Yeye naye aliwatuma Mitume (taz. Yn 20:21) akisema, “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari” (Mt 28:19-20). Kanisa limepokea kutoka kwa Mitume amri hii ya Kristo, yenye umuhimu, ya kuuhubiri ukweli wa wokovu, ili kuitimiza hata mwisho wa dunia (taz. Mdo 1:8). Nalo Kanisa lashika maneno ya Mtume kana kwamba ni yake lenyewe, “Ole wangu nisipoihubiri Injili!” (1Kor 9:16), kwa hiyo huendelea kuwatuma wamisionari bila kukoma mpaka Makanisa mapya (novellae Ecclesiae) yatakapokwisha wekwa tayari, nayo yenyewe yapate kuendeleza tendo la uinjilishaji. Maana Kanisa huongozwa na Roho Mtakatifu kushiriki kazi ili kutimiliza azimio la Mungu aliyemweka Kristo kuwa asili ya wokovu kwa ulimwengu mzima. Kwa njia ya kuhubiri Injili Kanisa huwavuta wasikilizaji kuipokea na kuikiri imani, huwaandaa wapate ubatizo na kuwatoa katika utumwa wa upotovu, na kuwafanya kuwa viungo vya mwili wa Kristo, ili wakue ndani yake katika upendo hata ukamilifu. Matokeo ya kazi yake ni kwamba wema wowote upatikanao kuwa umepandwa katika moyo na nia za watu, na katika ibada na tamaduni za mataifa, zisipotee, bali ziponywe, ziinuliwe na kukamilishwa kwa ajili ya utukufu wa Mungu, aibu ya Shetani na heri ya mwanadamu. Kila mwanafunzi wa Kristo, kwa upande wake, huwajibika kuieneza imani[35]. Lakini, ijapo kila mmoja aweza kuwabatiza waaminio, ni juu ya padre tu kulitimiza jengo la Mwili kwa njia ya sadaka ya Ekaristi, akitekeleza maneno aliyoyasema Mungu kwa kinywa cha nabii, “Tokea maawio ya jua hata machweo yake jina langu ni kuu katika mataifa; na katika kila mahali unatolewa uvumba na dhabihu safi kwa jina langu” (Mal 1:11)[36]. Hivyo Kanisa husali na kutenda kazi pia ili ukamilifu wa ulimwengu wote uingizwe katika Taifa la Mungu, lililo Mwili wa Bwana na Hekalu la Roho Mtakatifu. Tena, ili katika Kristo, aliye kichwa cha wote, heshima yote na utukufu wote vitolewe kwa Muumba na Baba wa ulimwengu.

Sura ya Tatu

MUUNDO WA KIHIERARKIA WA KANISA

NA HASA UASKOFU

Utangulizi

18. Kristo Bwana, kusudi kulichunga na kuzidi kuliongeza Taifa la Mungu, aliweka katika Kanisa lake huduma mbalimbali, zinazolenga wema wa Mwili wote. Kwa maana wahudumu, waliopewa uwezo mtakatifu, wanawatumikia ndugu zao, ili wote walio watu wa Taifa la Mungu, na hivyo wamejaliwa heshima ya kweli ya kikristo, wakielekea shabaha ileile kwa hiari na kwa utaratibu, wakaufikie wokovu.

Sinodi hii takatifu hufuata nyayo za Mtaguso Mkuu wa Vatikani wa I, hufundisha na kutangaza pamoja nao ya kwamba Yesu Kristo, aliye Mchungaji wa milele, alijenga Kanisa takatifu, akawatuma Mitume kama Yeye mwenyewe alivyotumwa na Baba (taz. Yn 20:21), tena akataka waandamizi wao, yaani Maaskofu, wawe wachungaji wa Kanisa lake hata ukamilifu wa nyakati. Kusudi Uaskofu wenyewe uwe mmoja na usiogawanyika, akamweka Mt. Petro juu ya Mitume wengine, na katika yeye akatia chanzo na msingi udumuo na uonekanao wa umoja wa imani na wa ushirika[37]. Mtaguso Mtakatifu huwatolea tena waamini wote fundisho hilo la uanzishaji, udumifu, nguvu na tabia ya mamlaka tukufu ya Papa na ya Majisterio yake isiyoweza kukosa, ili liaminike kwa uthabiti. Tena, katika kuendelea kwa njia hiyohiyo, linaamua kukiri na kutangaza mbele ya wote fundisho juu ya Maaskofu walio waandamizi wa Mitume, ambao pamoja na mwandamizi wa Petro, aliye Wakili wa Kristo[38] na kichwa kionekanacho cha Kanisa zima, waiongoza nyumba ya Mungu aliye hai. 

Kuitwa na kuwekwa kwa Thenashara

19. Bwana Yesu, baada ya kumwomba Baba, aliwaita aliowataka mwenyewe, akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri ufalme wa Mungu (taz. Mk 3:13-19; Mt 10:1-42). Na Mitume hawa (taz. Lk 6:13) akawaweka wawe kama urika (ad modum collegii) au kundi la kudumu (coetus stabilis), ambalo kiongozi wake alimweka Petro, aliyemteua miongoni mwao (taz. Yn 21:15-17). Akawatuma kwanza kwa wana wa Israeli, kisha kwa mataifa yote (taz. Rum 1:16), ili, wakishiriki katika uwezo wake Yesu, wawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi wake, wawatakatifuze na kuwaongoza (taz. Mt 28:16-20; Mk 16:15; Lk 24:45-48; Yn 20:21-23), na hivyo walieneze Kanisa na kulichunga wakihudumia chini ya uongozi wa Bwana, siku zote hata ukamilifu wa dahari (taz. Mt 28:20). Nao walithibitishwa kikamilifu katika utume huo siku ya Pentekoste (taz. Mdo 2:1-36) kadiri ya ahadi ya Bwana, “Mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi” (Mdo 1:8). Aidha Mitume, wakihubiri kotekote Injili (taz. Mk 16:20), ipokelewayo na wasikilizaji kwa kazi ya Roho Mtakatifu, hulikusanya Kanisa lote ulimwenguni, ambalo Bwana aliasisi juu ya msingi wa Mitume na kulijenga juu ya Mt. Petro, kiongozi wao, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni (taz. Ufu 21:14; Mt 16:18; Efe 2:20)[39].

Maaskofu ni waandamizi wa mitume

20. Utume ule wa kimungu, uliokabidhiwa na Kristo kwa Mitume, utadumu hata mwisho wa nyakati (taz. Mt 28:20), maadamu Injili wanayopaswa kuipeleka (tradendum) ni, kwa ajili ya Kanisa, asili ya maisha yake sikuzote. Kwa sababu hiyo Mitume, katika jamii hii iliyopangwa kihierarkia, walijitahidi kuwaweka waandamizi.

Kwa maana, licha ya kuwa na wasaidizi katika huduma yao[40], waliwaachia wasaidizi wao wa karibu zaidi, kama wosia, wajibu wa kulitimiza na kuimarisha tendo lililoanzishwa nao[41], ili utume uliokabidhiwa kwao uendelezwe baada ya kifo chao. Wakasisitiza walitunze kundi lote, ambalo Roho Mtakatifu aliwaweka ndani yake wapate kulilisha Kanisa lake Mungu (taz. Mdo 20:28). Basi, wakawaweka watu hawa na baadaye wakaagiza kwamba watu wengine wenye kukubaliwa wapokee huduma yao baada ya kufa kwao[42]. Kati ya huduma mbalimbali zinazotekelezwa katika Kanisa tangu siku za kwanza, kama vile Mapokeo yashuhudiavyo, inashika nafasi ya kwanza kazi ya wale waliowekwa katika Daraja ya Uaskofu, ambao, kwa uandamizi unaoendelea tangu awali[43], wanayo matawi ya shina la Mitume[44]. Hivyo basi, Mt. Ireneus ashuhudiavyo, Mapokeo ya kitume hujidhihirisha[45] na kutunzwa[46] ulimwenguni mwote kwa njia ya wale waliosimikwa na Mitume kuwa Maaskofu na kwa njia ya waandamizi wao mpaka sasa.

Basi, Maaskofu wamekabidhiwa huduma ya jumuiya pamoja na msaada wa Mapadre na mashemasi[47], wakiliongoza kundi lake kwa niaba ya Mungu[48], ambalo wao ni wachungaji wake, wakiwa kama walimu wa mafundisho, makuhani wa ibada takatifu, wahudumu wa uongozi[49]. Aidha, kama vile udumuvyo wajibu uliokabidhiwa na Bwana kwa Petro tu, mkuu wa Mitume, unaotakiwa kupitishwa kwa waandamizi wake, vivyo hivyo hudumu wajibu wa Mitume wa kulichunga Kanisa, ambao inabidi utimizwe bila katizo na Daraja takatifu ya Maaskofu[50]. Kwa hiyo Mtaguso Mkuu mtakatifu hufundisha kwamba Maaskofu waliwekwa mahali pa Mitume kwa amri ya kimungu[51], ili wawe wachungaji wa Kanisa, ambao awasikilizaye wao amsikiliza Kristo, naye awakataaye wao amkataa Kristo na yule aliyemtuma Kristo (taz. Lk 10:16)[52]. Hali ya kisakramenti ya Uaskofu

21. Basi, katika nafsi za Maaskofu, wanaosaidiwa na mapadre, yupo katikati ya waamini Bwana Yesu Kristo, aliye Kuhani Mkuu. Maana wakati anapoketi kuume kwa Mungu Baba, haiachi jumuiya ya makuhani wake wakuu[53], bali kwanza kwa njia ya huduma yao mashuhuri huyatangazia mataifa yote neno la Mungu na kuwapa waamini sakramenti za imani bila kikomo. Tena kwa uangalifu wao wa kibaba (taz. 1Kor 4:15) huviunganisha viungo vipya na Mwili wake kwa kuvizaa upya kutoka juu. Mwishowe kwa hekima na busara yao hulielekeza na kuliongoza taifa la agano jipya katika safari yake ya kuelekea uheri wa milele. Wachungaji hawa, walioteuliwa ili kulichunga kundi la Bwana, ndio watumishi wa Kristo na mawakili wa siri za Mungu (taz. 1Kor 4:1); nao walikabidhiwa huduma ya kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu (taz. Rum 15:16; Mdo 20:24), na huduma ya Roho na ya haki katika utukufu (taz. 2Kor 3:8-9).

Kusudi wapate kutimiza kazi hizo kubwa namna hiyo, Mitume walitajirishwa na Kristo kwa mmiminiko wa pekee wa Roho Mtakatifu aliyewajilia (taz. Mdo 1:8; 2:4; Yn 20:22-23); nao wenyewe kwa kuwekea mikono yao waliwapa wasaidizi wao kipaji hicho cha Roho (taz. 1Tim 4:14; 2Tim 1:6-7), ambacho ndicho kimepitishwa mpaka kwetu kwa njia ya kuwekwa wakfu kwa Maaskofu[54]. Mtaguso mtakatifu unafundisha kwamba kwa kuwekwa wakfu kwa Maaskofu hujaliwa ukamilifu wa sakramenti ya upadre, yaani ukamilifu ule ambao, katika mapokeo ya kiliturujia ya Kanisa, na katika lugha ya Mababa wa Kanisa, huitwa ukuhani mkuu, ulio kilele cha huduma takatifu[55]. Uwakfu wa Maaskofu hukabidhi pia, pamoja na jukumu la kutakatifuza, majukumu ya kufundisha na ya kuongoza, ambayo lakini, kwa maumbile yake, yaweza kutekelezwa tu katika ushirika wa kihierarkia na kichwa na viungo vingine vya urika [huo]. Kwa maana kutokana na mapokeo, yajidhihirishavyo hasa katika ibada za kiliturujia na desturi za Kanisa la Mashariki na la Magharibi, huonekana wazi kwamba, kwa njia ya kuwekea mikono na kutaja maneno ya uwakfu, hujaliwa neema ya Roho Mtakatifu[56] na kutiwa muhuri (characterem) takatifu[57], kiasi kwamba Maaskofu, kwa namna bora na dhahiri, wanashika nafasi ya Kristo mwenyewe aliye Mwalimu, Mchungaji na Kuhani mkuu, na kutenda katika nafsi yake (in Eius persona)[58]. Tena ni juu ya Maaskofu, kwa njia ya sakramenti ya Daraja takatifu, kuwaingiza wateuliwa wapya katika umoja wa Maaskofu.

Urika wa Maaskofu na mkuu wake

22. Kama vile Mt. Petro na wale Mitume wengine wameunganika, kwa agizo la Bwana, katika urika mmoja tu wa kitume, kwa jinsi iliyo sawa (pari ratione), Baba Mtakatifu aliye mwandamizi wa Petro, na Maaskofu walio waandamizi wa Mitume, wanaungana pamoja. [Yapo mambo mawili] yaonyeshayo tabia na maumbile ya kiurika ya Daraja ya uaskofu: yaani nidhamu ya kale, ambayo kufuatana nayo Maaskofu wa ulimwengu mzima walishirikiana wao kwa wao na pamoja na Askofu wa Roma, katika kifungo cha umoja, upendo na amani[59]; na vilevile kukusanyika kwa Mitaguso[60] ili kuamua pamoja masuala yaliyo muhimu[61], baada ya kutia maanani na kuchunguza maoni ya wengi[62]. Tena Mitaguso ya Kanisa iadhimishwayo katika mfululizo huthibitisha kwa udhahiri maumbile hayo, ambayo imekwisha kudokezwa pia na desturi iliyopo tangu zamani ya kuwashirikisha Maaskofu wengi katika kumwinua mteuliwa mpya kwenye Daraja ya ukuhani mkuu. Basi, mmoja hufanywa mshiriki wa Umoja wa Maaskofu kwa nguvu ya uwakfu wa kisakramenti (vi sacramentalis consecrationis) na kwa ushirika wa kihierarkia (hierarchica communione) pamoja na Kichwa cha Urika [huo] (Collegii Capite) na viungo vyake.

Urika wa Maaskofu hauwezi kuwa na mamlaka usipounganika na Baba Mtakatifu, aliye mwandamizi wa Petro, naye ndiye kichwa chake, ambaye mamlaka ya ukuu wake hudumu kabisa juu ya wote, wachungaji kwa waamini. Kwa maana Baba Mtakatifu, kwa nguvu ya wadhifa wake kama Wakili wa Kristo na Mchungaji wa Kanisa lote, ana mamlaka katika Kanisa, iliyo kamili, ya juu kabisa na iwahusuyo wote (plenam, supremam et universalem potestatem), ambayo anaweza kuyatimiza kwa uhuru. Urika wa Maaskofu (Ordo Episcoporum) ni urithi wa urika wa Mitume katika kufundisha na katika uongozi wa kichungaji; na ndani yake umoja wa Mitume huendelezwa katika nyakati. [Urika huo wa Maaskofu] pamoja na Kichwa chake aliye Baba Mtakatifu, na kamwe pasipo yeye, una mamlaka ya juu kabisa na kamili juu ya Kanisa lote[63]. [Mamlaka hiyo] yaweza kutekelezwa tu kwa idhini ya Baba Mtakatifu. Bwana alimweka Simoni Petro tu kuwa mwamba na mshika ufunguo wa Kanisa (taz. Mt 16:18-19), akamweka kuwa Mchungaji wa kundi lake zima (taz. Yn 21:15nk); lakini wadhifa wa kufunga na kufungua aliopewa Petro (taz. Mt 16:19), ulikabidhiwa pia kwa Urika wa Mitume uliounganika na mkuu wake (taz. Mt 18:18; 28:16-20)[64]. Urika huo maadamu umeundwa na wengi, huonyesha hali ya Taifa la Mungu ya kuwa la namna nyingi na la ulimwengu mzima; maadamu ulikusanyika chini ya kiongozi mmoja tu, huonyesha umoja wa kundi la Kristo. Ndani yake Maaskofu, wakiheshimu kwa uaminifu mamlaka na ukuu wa mkuu wao, hutumia mamlaka yao wenyewe kwa ajili ya mema ya waamini wao, na zaidi, ya Kanisa zima, ambalo Roho Mtakatifu huzidi kuimarisha muundo wake wenye utaratibu na upatano wake. Mamlaka kuu juu ya Kanisa lote uliyopewa Urika huo wa Maaskofu hutekelezwa kwa jinsi iliyo rasmi katika Mitaguso Mikuu. Hakuna Mtaguso Mkuu usipothibitishwa au walau kukubaliwa na mwandamizi wa Petro; tena ni haki ya Kuhani Mkuu wa Roma kuiitisha Mitaguso hii, kuiongoza na kuiidhinisha[65]. Mamlaka hiyohiyo ya Urika [wa Maaskofu] yaweza kutekelezwa na Maaskofu walioko pande zote za dunia wakishirikiana na Baba Mtakatifu, ilimradi mkuu wa Urika awe amewaita kutenda kiurika, au walau aidhinishe au kukubali kwa hiari tendo la pamoja la Maaskofu waliotawanyika, ili lipate kuwa kweli tendo la kiurika (actus collegialis).

Mahusiano ya Maaskofu ndani ya urika wao

23. Umoja wa kiurika huonekana pia katika mahusiano ya kila Askofu na Makanisa faridi na Kanisa lote zima. Kuhani Mkuu wa Roma, kama mwandamizi wa Petro, ni chanzo na msingi udumuo na uonekanao wa umoja wa Maaskofu na wa kundi la waamini[66]. Maaskofu, kila mmoja peke yake, ni chanzo na msingi uonekanao wa umoja katika Makanisa yao faridi[67], yaliyowekwa kwa mfano wa Kanisa lote zima, na katika hayo na kutokana na hayo lipo Kanisa katoliki lililo moja na pekee[68]. Kwa sababu hiyo kila Askofu huwakilisha Kanisa lake mwenyewe, na Maaskofu wote pamoja na Baba Mtakatifu, huwakilisha Kanisa lote katika kifungo cha amani, upendo na umoja.

Maaskofu wote, kila mmoja wao, waliowekwa juu ya Makanisa faridi, wanatumia madaraka yao ya kichungaji juu ya sehemu ya taifa la Mungu waliyokabidhiwa, si juu ya Makanisa mengine wala juu ya Kanisa zima. Lakini Maaskofu, maadamu ni viungo vya Umoja wa Maaskofu na waandamizi halali wa Mitume, kwa mpango na agizo la Kristo, wanapaswa, kila mmoja, kulishughulikia Kanisa lote[69]. Shughuli hiyo, ijapo haitekelezwi kwa mamlaka ya kisheria, lakini huchangia sana katika kuleta manufaa ya Kanisa zima. Kwa maana Maaskofu wote huwajibika kukuza na kuhifadhi umoja wa imani na nidhamu iliyo moja kwa Kanisa lote; tena huwafundisha waamini wawe na upendo kwa Mwili wote wa fumbo wa Kristo, hasa kwa viungo vilivyo maskini, vyenye kuteswa na kuudhiwa kwa ajili ya haki (taz. Mt 5:10). Mwishowe huwajibika kuendeleza utendaji wowote unaohusu Kanisa lote, hasa kusudi imani ipate kukua na mwanga wa ukweli kamili uwazukie watu wote. Aidha, ni kweli kwamba [Maaskofu], wakiongoza vizuri kila mmoja Kanisa lake kama sehemu ya Kanisa zima, wanachangia kwa manufaa ustawi wa Mwili wote wa fumbo, ambao ni mwili unaofanywa na Makanisa pia[70].

Juhudi ya kutangaza Injili popote duniani ni juu ya Umoja wa Wachungaji, ambao Kristo aliwapa amri wote kwa pamoja, akiweka wajibu ulio wa pamoja, kama vile Baba Mtakatifu Selestino alivyowasisitizia Mababa wa Mtaguso wa Efeso[71]. Hivyo Maaskofu, kila mmoja kwa upande wake, kwa kadiri utekelezaji wa wajibu wao wa pekee uwawezeshavyo, wanapaswa kushirikiana katika kazi wao kwa wao na pamoja na Halifa wa Petro, ambaye alikabidhiwa kwa namna ya pekee jukumu kuu la kueneza jina la Kristo[72]. Kwa hiyo inabidi [Maaskofu] watoe watenda kazi wa mavuno na pia misaada ya kiroho na ya kimwili, kwa nguvu zao zote kwa ajili ya misioni, au moja kwa moja wao wenyewe, au katika kuuchochea ushirikiano wenye bidii wa waamini. Hatimaye Maaskofu, wakifuata mfano mstahiki wa zamani, katika ushirika wa upendo usio na mipaka, watoe kwa moyo msaada wa kidugu kwa Makanisa mengine, hasa yale yaliyo jirani zaidi au maskini zaidi.

Kwa Maongozi ya Mungu imetokea kwamba baadhi ya Makanisa yaliyoasisiwa mahali mbalimbali na Mitume na waandamizi wao, katika mwenendo wa karne yalijiweka katika makundi mengi yenye kuunganika kwa utaratibu. Makundi hayo, wakati unapohifadhiwa umoja wa imani na muundo pekee wa kimungu wa Kanisa zima, yanatumia nidhamu, mazoea ya kiliturujia na urithi wa kiteolojia na wa kiroho yao yenyewe. Baadhi yao, hasa Makanisa ya zamani ya kipatriarka, kama mama katika imani, yamezaa mengine yaliyo kama binti zao, nayo hufungamana mpaka siku ya leo kwa kifungo cha upendo katika maisha ya kisakramenti na kwa kuheshimiana katika haki zao na wajibu zao[73]. Utofauti huo wa Makanisa mahalia yaliyo na umoja kati yao waonyesha kwa udhahiri zaidi ukatoliki wa Kanisa lisilogawanyika. Vivyo hivyo Mabaraza ya Maaskofu siku hizi yanaweza kusaidia kwa njia nyingi na zenye kuzaa matunda, ili roho ya umoja ipate kuwa na matokeo yaonekanayo.   

Huduma ya Maaskofu

24. Maaskofu, kwa kuwa ni waandamizi wa Mitume, wakabidhiwa na Bwana, aliyepewa mamlaka yote mbinguni na duniani, utume wa kuyafundisha mataifa yote na kuihubiri Injili kwa kila kiumbe, ili watu wote wapate wokovu kwa njia ya imani, ubatizo na kuzishika amri (taz. Mt 28:18-20; Mk 16:15-16; Mdo 26:17nk). Ili wapate kuutimiza utume huo Kristo Bwana aliwaahidia Mitume Roho Mtakatifu, na siku ya Pentekoste alimtuma kutoka mbinguni, ili kwa nguvu ya Roho huyo wapate kuwa mashahidi wake mpaka mwisho wa dunia, mbele ya mataifa, jamii za watu na wafalme (taz. Mdo 1:8; 2:1nk; 9:15). Wajibu huo Bwana alioukabidhi kwa wachungaji wa taifa lake ni utumishi wa kweli, ambao katika Maandiko Matakatifu huitwa kwa neno lenye maana “diakonia” au huduma (taz. Mdo 1:17 na 25; 21:19; Rum 11:13; 1Tim 1:12).

Utume wa kikanisa (missio canonica) wa Maaskofu waweza kufanyika kadiri ya desturi halali, zisizokanushwa na mamlaka ya juu kabisa ya Kanisa yanayolihusu Kanisa lote zima, au kwa sheria ziwekwazo au kukubaliwa na mwenye mamlaka hiyohiyo, au moja kwa moja na Halifa wa Petro mwenyewe. Ikiwa huyo anapinga au anakataa ushirika wa kitume, Maaskofu hawawezi kukubaliwa kwenye madaraka[74]

Jukumu la kufundisha

25. Kati ya majukumu ya Maaskofu yaliyo muhimu zaidi, kuhubiri Injili hushika nafasi ya kwanza[75]. Maana Maaskofu ndio watangazaji wa imani wawaletao wanafunzi wapya kwa Kristo, na walimu halisi waliojaliwa mamlaka ya Kristo, ambao wanawahubiria watu waliokabidhiwa kwao imani. Imani hiyo inawapasa kuishika na kuiishi katika mwenendo wao. Tena, wanaieleza imani hiyo katika mwanga wa Roho Mtakatifu, wakitoa katika hazina ya Ufunuo vitu vipya na vya kale (taz. Mt 13:52), wakaufanya uzae matunda na wanalichunga kundi lao ili kufukuza makosa yanayolihatarisha (taz. 2Tim 4:1-4). Maaskofu wanaofundisha katika ushirika na Baba Mtakatifu, lazima waheshimiwe na wote kama mashahidi wa ukweli ulio wa kimungu na wa kikatoliki; aidha, waamini wapaswa kuukubali uamuzi wa Askofu wao, utolewao kwa jina la Kristo kuhusu imani na maadili, na kuambatana nao kwa roho ya utii wa kidini. Lakini utii huo wa kidini ulio wa utashi na wa akili inabidi wautoe kwa namna ya pekee kwa Majisterio halisi ya Baba Mtakatifu, hata wakati asiposema “ex cathedra”, ili Majisterio yake kuu ikubalike kwa heshima, na hukumu zitolewazo naye zipokelewe kwa moyo wa dhati, kadiri anavyojulisha nia na mapenzi yake, ambayo yanaonekana hasa kwa tabia ya hati, au kwa kurudiwa mara nyingi mafundisho yaleyale, au kwa namna ya kusema kwake.

Ingawa kila Askofu peke yake hana fadhila ya kutokosea (infallibilitas), lakini Maaskofu hutangaza fundisho la Kristo bila kukosa[76] pale ambapo, ijapo wametawanyika ulimwenguni, watunza kifungo cha ushirika kati yao na pamoja na Halifa wa Petro, katika mafundisho yao halisi kuhusu mambo ya imani na maadili, wanakubaliana juu ya fundisho (sententia) linalotakiwa kulipokea kama la kweli na la mwisho. Jambo hilo ni dhahiri zaidi wanapokusanyika katika Mtaguso Mkuu, nao ni walimu na waamuzi wa imani na maadili kwa ajili ya Kanisa lote, na maamuzimkataa (definitionibus) yao yapaswa yashikwe kwa utii na imani[77].

[Fadhila hii ya] kutokosea ambayo Mkombozi aliye Mungu alitaka Kanisa lake lijaliwe kila linapoamua kuhusu mafundisho ya imani na maadili, inaenea kadiri ya amana (depositum) ya Ufunuo wa Mungu ieneavyo, ambayo lazima itunzwe kwa uchaji na kuelezwa kwa uaminifu. Baba Mtakatifu wa Roma, aliye kichwa cha Urika wa Maaskofu, hujaliwa fadhila hiyo ya kutokosea, kwa nguvu ya wadhifa wake, wakati anapotangaza kwa mkataa (definitivo actu) fundisho kuhusu imani au maadili[78], hali akiwa mchungaji mkuu na mwalimu wa waamini wote, anayewaimarisha ndugu zake katika imani (taz. Lk 22:32). Kwa hiyo maamuzimkataa (definitiones) yake huitwa kwa haki [maamuzi] yasiyokosoleka (irreformabiles) kwa tabia yake yenyewe na siyo kwa kibali cha Kanisa, kwa kuwa yametangazwa kwa msaada wa Roho Mtakatifu, ulioahidiwa kwake katika nafsi ya Mtakatifu Petro. Kwa hiyo [maamuzi yake] hayahitaji idhini yoyote ya wengine wala haiwezekani kukata rufaa kwa baraza jingine. Kwa maana hapo Baba Mtakatifu hatoi hukumu zake kama mtu binafsi, bali anaeleza au kulinda mafundisho ya imani katoliki[79] kama mwalimu mkuu wa Kanisa zima aliyejaliwa katika nafsi yake karama ya kutokosea iliyo ya Kanisa lenyewe. [Karama hii ya] kutokosea iliyoahidiwa kwa Kanisa imo pia katika Umoja wa Maaskofu unapotekeleza Majisterio kuu pamoja na Halifa wa Petro. Ukubali wa Kanisa hauwezi kukosekana kwa maamuzimkataa haya kwa sababu ya tendo la Roho Mtakatifu mwenyewe lenye kutunza na kuendeleza kundi lote la Kristo katika umoja wa imani[80].

Baba Mtakatifu wa Roma na Umoja wa Maaskofu pamoja naye wanapoelezea fundisho fulani, wanalitoa kadiri ya Ufunuo wenyewe, ambao wote wanatakiwa kuukubali na kuufuata. Ufunuo huo, kwa njia ya Maandiko [Matakatifu] au ya Mapokeo hurithishwa kikamilifu na uandamizi halali wa Maaskofu (per legitimam Episcoporum successionem), na kwanza na uangalizi wa Baba Mtakatifu mwenyewe, tena hutunzwa kitakatifu na kuelezwa kiaminifu katika Kanisa kwa mwanga wa Roho wa ukweli[81]. Baba Mtakatifu na Maaskofu, kwa sababu ya wadhifa wao na umuhimu wa jambo lenyewe, wanajitahidi kwa bidii na kwa njia zifaazo, ili kuuchunguza Ufunuo huo barabara na kuueleza inavyofaa[82]; ila hawapati ufunuo mpya wa hadhara kana kwamba unaihusu amana ya kimungu ya imani[83].

Jukumu la kutakatifuza

26. Askofu, aliyepewa ukamilifu wa sakramenti ya Daraja takatifu, ndiye “wakili wa neema ya ukuhani mkuu”[84], hasa katika Ekaristi anayotolea mwenyewe au kuagiza itolewe[85], na kwa njia ya hiyo Kanisa daima huishi na kukua. Kanisa hilo la Kristo limo kweli ndani ya jumuiya za mahali za waamini zilizo halali, ambazo, zikiunganika na wachungaji wao, zaitwa nazo pia, katika Agano Jipya, Makanisa[86]. Maana hayo, katika mahali pao, ndilo Taifa jipya lililoitwa na Mungu katika Roho Mtakatifu na uthibitifu mwingi (taz. 1The 1:5). Ndani yao kwa njia ya kuhubiri Injili ya Kristo waamini wanakusanywa, na fumbo la Karamu ya Bwana laadhimishwa, “ili kwa mwili na damu ya Bwana udugu wa Mwili wote ufungamanishwe”[87]. Katika kila jumuiya inayoshiriki altare, chini ya huduma takatifu ya Askofu[88], hutolewa ishara ya mapendo yale na “umoja ule wa Mwili wa fumbo, ambao pasipo huo, haiwezekani kuwepo wokovu”[89]. Katika jumuiya hizo, ingawa mara nyingi ni ndogo na maskini, au zimetawanyika kama uamishoni, yumo Kristo, ambaye kwa nguvu zake, Kanisa lililo moja, takatifu, katoliki na la Mitume launganishwa[90]. Kwa maana, “ushirika wa mwili na damu ya Kristo haufanyi lolote jingine zaidi ya kwamba sisi tunageuzwa kuwa kile tunachopokea”[91].

Aidha, kila adhimisho halali la Ekaristi lasimamiwa na Askofu anayekabidhiwa wajibu wa kumtolea Mungu Mtukufu ibada ya dini ya kikristo na kuipanga kadiri ya amri za Bwana na sheria za Kanisa, zinazoainishwa zaidi, kwa habari ya Jimbo lake, na uamuzi wake mwenyewe.

Hivyo Maaskofu, kwa njia ya sala na kazi kwa ajili ya watu, wamimina ukamilifu wa utakatifu wa Kristo kwa namna mbalimbali na kwa wingi. Kwa huduma ya Neno wawashirikisha waaminio uweza wa Mungu uuletao wokovu (taz. Rum 1:16), na kwa njia ya sakramenti, ambazo kwa mamlaka yao wanapanga utoaji wake wenye utaratibu na matunda[92], wawatakatifuza waamini. Wao wenyewe wasimamia utoaji wa ubatizo, ambao kwao unajaliwa ushirika katika ukuhani wa kifalme wa Kristo. Nao ni wahudumu halisi (ministri originarii) wa kipaimara, watoaji wa Daraja takatifu, wapangao utaratibu wa nidhamu ya kitubio, na kwa juhudi wawaonya na kuwafundisha watu wao ili washike nafasi zao kwa imani na uchaji katika Liturujia na hasa katika sadaka takatifu ya Misa. Mwisho inawapasa kuwasaidia kwa mfano wa mtindo wa maisha yao wale wanaowasimamia, wakiiepusha mienendo yao na mabaya, na kuigeuza kuwa mizuri, iwezekanavyo kwa msaada wa Mungu, ili wachungaji wapate kuufikia uzima wa milele, pamoja na kundi lililokabidhiwa kwao[93].

Jukumu la kuongoza

27. Maaskofu huyaongoza Makanisa faridi waliyokabidhiwa kama mawakili na wajumbe wa Kristo[94], kwa mashauri, maonyo na mifano, na pia kwa mamlaka na uwezo mtakatifu, ambao lakini hawautumii ila kwa kulijenga kundi lao katika ukweli na utakatifu, wakikumbuka kuwa aliye mkubwa na awe kama aliye mdogo, na mwenye kuongoza kama yule atumikaye (taz. Lk 22:26-27). Uwezo huo, wanaotumia wenyewe kwa jina la Kristo, ni halisi, wa kawaida na wa kujitegemea, ingawa mwishowe utekelezaji wake waongozwa na mamlaka kuu ya Kanisa, na waweza kutiwa mipaka fulani kwa ajili ya manufaa ya Kanisa au ya waamini. Kwa nguvu ya uwezo huu Maaskofu wanayo haki takatifu na wajibu mbele ya Mungu wa kutoa sheria na hukumu kwa waliowekwa chini yao, na wa kusimamia yale yahusuyo utaratibu wa ibada na wa utume.

Nao wanakabidhiwa kwa ukamilifu huduma ya kichungaji, yaani utunzaji wa kundi lao wa daima na wa kila siku, wala wasihesabiwe kuwa mawakili wa Mababa Watakatifu wa Roma, kwa sababu wanatumia uwezo ulio wao wenyewe na huitwa kweli wasimamizi wa watu wanaowaongoza[95]. Mamlaka yao hayaondolewi na mamlaka kuu ya Kanisa zima, bali, kinyume chake, huthibitishwa, huimarishwa na hulindwa nayo[96], kwa maana Roho Mtakatifu hutunza bila hitilafu muundo wa uongozi uliowekwa na Kristo Bwana katika Kanisa lake.

Askofu, aliyetumwa na Baba wa nyumba kuiongoza familia yake, aweke mbele ya macho mfano wa Mchungaji Mwema asiyekuja kutumikiwa, bali kutumika (taz. Mt 20:28; Mk 10:45) na kuutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo (taz. Yn 10:11). Yeye, aliyetwaliwa katika wanadamu na kuwa katika hali ya udhaifu, aweza kuwachukulia wasiojua na wenye kupotea (taz. Ebr 5:1-2). Asikatae kuwasikiliza walio chini yake anaowatunza kama watoto wake wa kweli na kuwaonya wamsaidie kwa bidii. Kwa vile atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya roho zao (taz. Ebr 13:17), afanye juhudi kwa ajili yao, kwa sala, mahubiri, na matendo yote ya mapendo, pia kwa ajili ya wale wasio bado wa kundi lile moja, ambao awaone kama watu waliokabidhiwa kwake katika Bwana. Naye, kwa kuwa huwiwa na wote, kama Mtume Paulo awe tayari kuihubiri Injili kwa wote (taz. Rum 1:14-15) na kuwahimiza waamini wake wawe na utendaji wa kitume na wa kimisioni. Na waamini kwa upande wao yawapasa kuambatana na Askofu kama Kanisa na Yesu Kristo, na kama Yesu Kristo na Mungu Baba, ili yote yaunganishwe katika umoja[97] na kuzidi kwa wingi kwa ajili ya utukufu wa Mungu (taz. 2Kor 4:15).

Mapadre: mahusiano yao na Kristo, na Maaskofu, na umoja wa mapadre na Taifa la kikristo

28. Kristo, ambaye Baba alimtakasa, akamtuma ulimwenguni (taz. Yn 10:36), kwa njia ya Mitume wake aliwashirikisha katika uwakfu na utume wake waandamizi wao, yaani Maaskofu[98], ambao waliwakabidhi kihalali watu wengine katika Kanisa wadhifa wa huduma yao kwa daraja mbalimbali. Hivyo huduma ya kikanisa iliyoasisiwa na Mungu hutekelezwa katika daraja mbalimbali na wale waitwao tangu zamani Maaskofu, Mapadre, Mashemasi[99]. Mapadre, ingawa hawana kilele cha ukuhani, na katika kutumia uwezo wao wapo chini ya Maaskofu, lakini waunganika nao katika heshima ya kikuhani[100], na kwa nguvu ya Daraja takatifu[101], kwa mfano wa Kristo aliye Kuhani mkuu na wa milele (taz. Ebr 5:1-10; 7:24; 9:11-28), wawekwa wakfu, kama makuhani wa kweli wa Agano Jipya, kwa ajili ya kuihubiri Injili, kuwachunga waamini na kuadhimisha ibada kwa Mungu[102]. Wakishiriki kazi ya Mpatanishi, aliye mmoja, Kristo (taz. 1Tim 2:5), katika daraja ya huduma yao, wawahubiria wote Neno la Mungu. Nao hutekeleza jukumu lao tukufu hasa katika ibada au kusanyiko la Ekaristi, ambapo wakitenda katika nafsi ya Kristo[103], na kulitangaza fumbo lake, huunganisha matoleo ya waamini na sadaka ya Kichwa chao, na katika sadaka ya Misa huidhihirisha na kuitekeleza[104], hata Bwana ajapo (taz. 1Kor 11:26), sadaka ile ya Agano Jipya iliyo moja, yaani sadaka ya Kristo, aliyejitoa nafsi yake mara moja tu kwa Mungu Baba kuwa sadaka isiyo na mawaa (taz. Ebr 9:11-28). Tena, kwa ajili ya waamini watubu au wagonjwa, hutimiza kwa nguvu yote huduma ya upatanisho na faraja, na kumtolea Mungu Baba mahitaji na sala za waamini (taz. Ebr 5:1-4). Wakiitekeleza huduma ya Kristo aliye Mchungaji na Kichwa, kwa kadiri ya mamlaka yao[105], huikusanya familia ya Mungu kama jumuiya ya ndugu iliyopenywa na roho ya umoja[106], na kwa njia ya Kristo katika Roho huiongoza kwa Mungu Baba. Katikati ya kundi lao humwabudu katika roho na kweli (taz. Yn 4:24). Hatimaye hujitaabisha kwa kuhutubu na kufundisha (taz. 1Tim 5:17), wakisadiki waliyoyasoma na kuyatafakari katika sheria ya Bwana, wakifundisha waliyosadiki na kuyafuata waliyofundisha[107].

Mapadre, washiriki wenye busara wa Daraja ya Uaskofu[108], na msaada na chombo chake, waitwao kutumikia taifa la Mungu, wanakuwa umoja, au presbiterio (presbyterium), pamoja na Askofu wao[109], ijapokuwa umoja huu una wadhifa mbalimbali. Katika kila jumuiya ya waamini ya mahali [mapadre hao] wanafanya kwa namna fulani awepo Askofu, ambaye wanashirikiana naye kwa roho pana na yenye tumaini, na wanashika, kwa kiasi fulani, majukumu yake na uangalizi wake na kuzitekeleza kwa juhudi za kila siku. Nao, chini ya mamlaka ya Askofu, hutakatifuza na kuongoza fungu la kundi la Bwana walilokabidhiwa, hulifanya Kanisa lote zima lionekane wazi mahali pao na kutenda kazi ifaayo hata Mwili mzima wa Kristo ujengwe (taz. Efe 4:12). Wakiangalia daima mema ya wana wa Mungu wajitahidi kuchangia matendo yao katika kazi ya uchungaji ya Jimbo zima, na zaidi, ya Kanisa lote. Kwa sababu ya ushirikiano huo katika ukuhani na utume, Mapadre wamkiri kweli Askofu kama baba yao na kumtii kwa heshima. Na Askofu awahesabu Mapadre, walio wasaidizi wake, kama wana na rafiki, kama vile Kristo anavyowaita wanafunzi wake si tena watumwa, bali rafiki (taz. Yn 15:15). Kwa sababu ya Daraja yao na huduma yao Mapadre wote wa kijimbo na wa kitawa, washirikishwa katika umoja wa Maaskofu, na kadiri ya wito wao na neema waliyopewa, wahudumia mema ya Kanisa zima.

Kwa nguvu ya upadirisho mtakatifu na ya utume ulio sawasawa Mapadre wote hufungamana katika udugu wa ndani, unaopaswa kujionyesha kwa hiari na kwa moyo katika kusaidiana katika mambo ya kiroho na ya kimwili, ya kichungaji na ya binafsi, katika mikutano na katika ushirikiano wa maisha, wa kazi na wa upendo.

Kama baba katika Kristo wawaangalie waamini wao waliowazaa kiroho kwa Ubatizo na mafundisho (taz. 1Kor 4:15; 1Pet 1:23). Wakijifanya kwa moyo vielelezo vya kundi lao (taz. 1Pet 5:3) waongoze na kuitumikia jumuiya yao ya mahali, ili yenyewe istahili kuitwa kwa jina lile ambalo kwalo taifa lile lililo moja na zima la Mungu lasifiwa, yaani Kanisa la Mungu (taz. 1Kor 1:2; 2Kor 1:1; n.k.). Wakumbuke katika mwenendo na uangalizi wao wa kila siku kuwaonyesha waamini na wasio waamini, wakatoliki na wasio wakatoliki, sura ya huduma ya kweli ya kikuhani na ya kichungaji, na ya kwamba inawapasa kuwashuhudia wote ukweli na uzima, na kama wachungaji wema, kuwatafuta pia wale (taz. Lk 15:4-7) ambao, ijapokuwa walibatizwa katika Kanisa katoliki, waliacha kupokea sakramenti, au hata kukosa imani.

Kwa kuwa siku hizi wanadamu wanazidi kufungamana wao kwa wao katika maisha ya kiraia, ya kiuchumi na ya kijamii, yawapasa Mapadre, kwa kuunganisha juhudi na kazi zao chini ya uongozi wa Maaskofu na wa Baba Mtakatifu, waondoshe kila sababu ya mfarakano (dispersionis), kusudi wanadamu wote waongozwe kwenye umoja wa familia ya Mungu.

Mashemasi

29. Kwenye daraja iliyo chini katika Hierarkia wapo Mashemasi, ambao wamewekewa mikono “siyo kwa ajili ya ukuhani, bali kwa utumishi”[110]. Kwa maana, wakiwa wamethibitika kwa neema ya sakramenti wanalitumikia taifa la Mungu katika ushirika na Askofu na umoja wa Mapadre wake, katika huduma (diaconia) ya liturujia, ya Neno na ya upendo. Ni wajibu wa Shemasi, kadiri atakavyokabidhiwa na mamlaka halali, kutoa Ubatizo rasmi, kuitunza Ekaristi na kuigawa, kuisimamia Ndoa na kuibariki kwa jina la Kanisa, kuwapelekea Komunyopamba walio katika hatari ya kufa, kuwasomea waamini Maandiko Matakatifu, kuwafundisha na kuwaonya watu, kuongoza ibada na sala za waamini, kugawa visakramenti, kuongoza ibada ya maziko na mazishi. Mashemasi, waliowekwa kwa matendo ya huruma na ya usimamizi, walikumbuke onyo la Mt. Polikarpo, “Wawe na huruma, wenye bidii, wakienenda katika ukweli wa Bwana, aliyejifanya mtumishi wa wote”[111].

Maadamu wajibu hizo zilizo za lazima sana kwa maisha ya Kanisa zinaweza kutekelezeka kwa shida katika nchi nyingi kadiri ya utaratibu wa sasa wa Kanisa la Roma, kwa siku za mbele Ushemasi unaweza tena kuwekwa kama Daraja halisi na ya kudumu ya Hierarkia. Ni juu ya Mabaraza halali ya Maaskofu ya nchi mbalimbali kwa kibali cha Baba Mtakatifu mwenyewe, kuamua kama inafaa na katika mahali gani Mashemasi wa namna hii waasisiwe kwa huduma ya kiroho. Kwa idhini ya Askofu wa Roma Ushemasi huu waweza kutolewa kwa wanaume wa umri wa kukomaa kutosha pia wakiishi katika ndoa, na vilevile kwa vijana wafaao ambao sheria ya useja lazima kwao idumu kuwa na nguvu.

Sura ya Nne

WALEI

Walei katika Kanisa

30. Mtaguso Mkuu, ukiisha kueleza majukumu ya Hierarkia unafurahi kuelekeza moyo kwenye hali ya waamini wakristo wenye kuitwa walei, ingawa yote yaliyosemwa juu ya Taifa la Mungu huwahusu walei, sawasawa kama watawa na wakleri. Lakini mambo mengine huwahusu kwa namna ya pekee walei, wanaume kwa wanawake, sababu ya hali yao na utume wao. Misingi ya mambo hayo inatakiwa kuchunguzwa kinaganaga zaidi, sababu ya mazingira ya pekee ya siku hizi. Maana wachungaji wenye Daraja takatifu wanajua sana jinsi walei wanavyosaidia usitawi wa Kanisa lote. Maana wachungaji wanajua kwamba hawakuasisiwa na Kristo ili wajitwalie peke yao utume wote wenye wokovu ambao Kanisa liliupokea kwa ajili ya ulimwengu, bali kwamba huduma yao tukufu ndiyo kuwachunga waamini na kutambua huduma zao na karama zao ili wote, kila mmoja kadiri ya kipaji chake, wasaidiane kwa pamoja katika kazi moja. Kwa maana yatupasa sisi sote “tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikamanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo” (Efe 4:15-16).

Tabia na utume wa walei

31. Kwa jina la walei humaanishwa hapa waamini wote isipokuwa wale wenye Daraja takatifu, na wenye hali ya kitawa iliyokubaliwa na Kanisa. Yaani, waamini ambao kwa vile walipata kuwa viungo vya mwili wa Kristo kwa ubatizo, na kufanywa kuwa Taifa la Mungu na kushirikishwa kwa namna yake katika huduma ya kikuhani, ya kinabii na ya kifalme ya Kristo, watekeleza, kadiri ya uwezo wao, utume wa Taifa lote la kikristo katika Kanisa na katika ulimwengu.

Tabia ya kidunia ndiyo tabia halisi na pekee ya walei. Maana wenye Daraja takatifu, ingawa mara nyingine waweza kuyashughulikia mambo ya kidunia, hata kufanya kazi ya kidunia, lakini kwa sababu ya wito wao wa pekee waelekezwa kimsingi na hasa (precipue et ex professo) ili kutimiza huduma takatifu; na watawa, kwa hali yao, watoa ushuhuda mwangavu na bora wa kwamba ulimwengu hauwezi kugeuzwa na kutolewa kwa Mungu pasipo roho ya heri nane. Ni juu ya walei, kutokana na wito wao, kuutafuta ufalme wa Mungu wakiyashughulikia mambo ya dunia na kuyaelekeza kadiri ya Mungu. Wanaishi ulimwenguni, yaani katika kazi zozote na shughuli za kidunia na katika mazingira ya kawaida ya maisha ya kifamilia na ya kijamii, ambayo maisha yao yamefungamanishwa nayo. Hapo wanaitwa na Mungu kusaidia kuutakatifuza ulimwengu, kama kutoka kwa ndani, mithili ya chachu, katika kuyatimiza majukumu yao wenyewe, wakiongozwa na roho ya kiinjili, na hivyo wamdhihirishe Kristo kwa wengine, waking’aa hasa kwa ushuhuda wa maisha yao, imani, matumaini na mapendo. Kwa hiyo yawahusu hao kwa namna ya pekee kuyaangaza na kuyapanga mambo yote ya kidunia, ambayo wamefungamana nayo, hili daima yafanyike na kukua kadiri ya Kristo na kuwa kwa sifa ya Muumba na Mkombozi.

Hadhi ya walei katika Taifa la Mungu

32. Kwa asasi ya Mungu Kanisa takatifu lapangwa na kuongozwa kwa namna mbalimbali ajabu. “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake” (Rum 12:4-5).

Basi, Taifa teule la Mungu ni moja tu: “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja” (Efe 4:5); hadhi moja ya viungo kwa kuzaliwa upya katika Kristo, neema moja ya kuwa watoto, wito mmoja wa kuwa wakamilifu, wokovu mmoja, tumaini moja na upendo usiogawanyika. Basi katika Kristo na katika Kanisa haiko tofauti mintarafu jamaa au taifa, hali ya kijamii au jinsia, kwa kuwa “hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa “mmoja” katika Kristo Yesu” (Gal 3:28; taz. Kol 3:11).

Basi, ingawa ndani ya Kanisa sio wote wanaoshika njia ileile, lakini wote waitwa kuwa watakatifu na wamepata imani ileile katika haki ya Mungu (taz. 2Pet 1:1). Ijapo wengine kwa mapenzi ya Kristo waliwekwa kuwa walimu, mawakili wa mafumbo na wachungaji kwa ajili ya wengine, lakini upo kati ya wote usawa wa kweli kuhusu hadhi na utendaji wa pamoja wa waamini wote kwa ajili ya kuujenga Mwili wa Kristo. Tofauti iliyowekwa na Bwana kati ya wenye Daraja takatifu na wengine wa Taifa la Mungu, inaleta yenyewe muungano kwa kuwa wachungaji na waamini wengine wamefungamana wao kwa wao kwa sababu kila mmoja anamhitaji mwenzake. Wachungaji wa Kanisa, wakiufuata mfano wa Bwana, watumikiane wao kwa wao na wawatumikie waamini; nao waamini wafanye kazi kwa juhudi pamoja na wachungaji na walimu. Hivyo katika kutofautiana wote wanaushuhudia umoja wa ajabu katika Mwili wa Kristo: kwa maana utofauti wenyewe wa neema, huduma na utendaji unawakusanya watoto wa Mungu katika umoja, kwa kuwa “kazi hizi zote huzitenda Roho huyu mmoja, yeye yule” (1Kor 12:11).

Kwa hiyo walei, kama vile kwa hisani ya Mungu wanaye kama ndugu Kristo, ambaye ijapokuwa ni Bwana wa vyote hakuja kutumikiwa bali kutumika (taz. Mt 20:28), vivyo hivyo wanao kama ndugu zao wale wenye Daraja takatifu ambao wanaichunga familia ya Mungu wakifundisha, wakitakatifuza na kuiongoza kwa mamlaka ya Kristo, ili amri mpya ya upendo itimizwe na wote. Mtakatifu Augustino aeleza hayo vizuri sana: “Ikiwa kunanitisha [kujitambua] mimi ni nani kwa ajili yenu, kunanifariji [kujitambua] mimi ni nani pamoja nanyi. Maana kwa ajili yenu, mimi ni Askofu; pamoja nanyi, mimi ni mkristo. Lile ni jina la wajibu, hili ni la neema; lile ni jina la hatari, hili ni la wokovu”[112].

Utume wa walei

33. Walei, waliokusanyika katika Taifa la Mungu na kuwekwa katika Mwili mmoja wa Kristo chini ya kichwa kimoja, wawao wote waitwa, kama viungo vyenye uhai, kutolea nguvu zao zote walizopewa na ufadhili wa Muumbaji na neema ya Mkombozi, ili kulikuza Kanisa na kulitakatifuza daima.

Utume wa walei ndio kushiriki utume wa Kanisa lenyewe uletao wokovu; na kuutimiza utume huo ni agizo ambalo wote wanapewa na Mungu mwenyewe kwa njia ya Ubatizo na Kipaimara. Kwa sakramenti, hasa kwa Ekaristi takatifu, mapendo kwa Mungu na kwa watu, yaliyo roho ya utume wote, yanashirikishwa na kulishwa. Lakini walei waitwa kwa namna ya pekee kuonyesha uwepo wa Kanisa na utendaji wake mahali pale na katika mazingira yale ambamo lenyewe haliwezi kuwa chumvi ya dunia, isipokuwa kwa njia yao tu[113]. Hivyo kila mlei, kwa sababu ya vipaji vyenyewe alivyopewa, anakuwa shahidi na wakati huohuo chombo hai cha utume wa Kanisa lenyewe “kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo” (Efe 4:7).

Licha ya utume huo uwahusuo moja kwa moja waamini wakristo wote, walei wanaweza kuitwa kwa njia mbalimbali kuushiriki kwa karibu zaidi utume wa Hierarkia[114], kadiri ya mfano wa wanaume na wanawake wale waliomsaidia Mtume Paulo katika kuishindania Injili, na kutenda kazi katika Bwana (taz. Flp 4:3; Rum 16:3nk). Aidha wana uwezo wa kuwekwa na Hierarkia ili kutimiza kazi kadhaa za Kanisa kwa ajili ya shabaha ya kiroho.

Basi, walei wote wametwishwa mzigo wenye heshima wa kufanya kazi ili azimio la wokovu la Mungu liwafikie zaidi na zaidi watu wote wa nyakati zote na wa mahali pote duniani. Kwa sababu hiyo wafunguliwe kila njia ili wao nao wapate kushiriki kwa bidii tendo la wokovu la Kanisa kadiri ya nguvu zao na mahitaji ya nyakati.

Jukumu ya kikuhani na ya kiibada

34. Yesu Kristo, aliye Kuhani mkuu na wa milele, akitaka kuendeleza ushuhuda wake na huduma (servitium) yake kwa njia ya walei pia, huwahuisha kwa Roho wake na kuwahimiza bila kukoma watimize tendo lolote lililo jema na kamili.

Kwa maana hao aliowaunganisha kwa ndani na maisha yake na huduma yake akawajalia pia sehemu ya jukumu lake la kikuhani ili watimize ibada ya kiroho, ili Mungu atukuzwe na watu waokolewe. Kwa sababu hiyo walei, maadamu wametunukiwa kwa Kristo (Christo dicati) na kupakwa Roho Mtakatifu, kwa namna ya ajabu waitwa na kufundishwa ili Roho azae kila siku matunda mengi sana ndani yao. Kwa maana matendo yao yote, sala zao na shughuli zao za kitume, maisha yao ya ndoa, na ya familia, kazi zao za kila siku, burudani za roho na za mwili, kama zikitimilizwa katika Roho, na hata taabu za maisha, zikichukuliwa kwa uvumilivu, zinageuka kuwa dhabihu za roho zinazokubaliwa na Mungu kwa njia ya Yesu Kristo (taz. 1Pet 2:5). Katika adhimisho la Ekaristi dhabihu hizo zatolewa kwa uchaji wote kwa Baba pamoja na sadaka ya Mwili wa Bwana. Hivyo walei pia, huku wakitenda kazi kila mahali katika utakatifu kama waabudu, wauweka wakfu kwa Mungu ulimwengu wote.

Jukumu la kinabii na ushuhuda

35. Kristo, aliye Nabii mkuu, alitangaza ufalme wa Baba kwa ushuhuda wa maisha yake na kwa nguvu ya neno, naye hutimiza kazi yake ya kinabii hadi ufunuo mkamilifu wa utukufu wake, si kwa njia ya Hierarkia peke yake, inayofundisha kwa jina na uwezo wake, bali pia kwa njia ya walei. Kwa sababu hiyo huwaweka walei kuwa mashahidi wake na kuwapa utambuzi wa imani (sensu fidei) na neema ya Neno (taz. Mdo 2:17-18; Ufu 19:10) ili nguvu ya Injili ing’ae katika maisha ya kila siku, ya kifamilia na ya kijamii. Nao wanajionyesha kuwa wana wa ahadi, wakiwa wamethibitika katika imani na matumaini, wakiukomboa wakati wa sasa (taz. Efe 5:16; Kol 4:5) na kungojea kwa saburi utukufu ujao (taz. Rum 8:25). Na matumaini haya wasiyafiche moyoni mwao, bali wayaonyeshe katika miundo ya maisha ya kidunia, wakiongoka daima na kushindana “juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya” (Efe 6:12).

Kama vile sakramenti za Sheria Mpya, zinazolisha maisha na utume wa waamini hudokeza mbingu mpya na nchi mpya (taz. Ufu 21:1), vivyo hivyo walei huwa watangazaji wenye nguvu wa imani ya mambo yatarajiwayo (taz. Ebr 11:1), ikiwa hawasiti kuunganisha ungamo la imani na maisha kadiri ya imani. Kuhubiri Injili, yaani kumtangaza Kristo kwa ushuhuda wa maisha na kwa neno, hupata tabia maalum na nguvu ya pekee kwa sababu hutekelezwa katika hali za kawaida za dunia.

Katika jukumu hilo hali ile ya maisha iliyotakatifuzwa na sakramenti maalum, yaani maisha ya ndoa na ya kifamilia, huonekana kuwa na thamani kubwa. Humo mna utekelezaji na shule bora ya utume wa walei, ambapo dini ya kikristo hupenya mpango wote wa maisha na kuugeuza zaidi siku kwa siku. Humo watu wa ndoa wana wito wao maalum wa kushuhudiana wao kwa wao na kwa watoto imani na upendo wa Kristo. Familia ya kikristo hutangaza kwa sauti kubwa nguvu za Ufalme wa Mungu zilizopo sasa, pamoja na matumaini ya uzima wa heri ujao. Hivyo kwa mfano na ushuhuda wake huuhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi na kuwaangaza wautafutao ukweli.

Basi walei, hata wanaposhughulikia mambo ya kidunia, waweza na kupaswa kutekeleza utendaji bora kwa ajili ya uinjilishaji wa ulimwengu. Hata kama baadhi yao wanatoa huduma takatifu fulani kadiri ya uwezo wao kama mawakili, wenye Daraja wakikosekana au wakizuiwa kwa madhuluma, au ikiwa wengi kati yao wanatumia nguvu zao zote katika kazi ya kitume, lakini inawapasa wote kusaidia kazi ya kueneza Ufalme wa Kristo duniani na kuukuza. Kwa hiyo walei wajitahidi kwa bidii kuufahamu zaidi na zaidi ukweli uliofunuliwa, na kumsihi Mungu kwa ari awajalie kipaji cha hekima.

Jukumu ya kifalme

36. Kristo, aliyekuwa mtii hata mauti na kwa hiyo Baba alimwadhimisha mno (taz. Flp 2:8-9), akaingia katika utukufu wa ufalme wake. Vitu vyote vimetiishwa chini yake mpaka atakapojitiisha yeye mwenyewe na kuvitiisha viumbe vyote kwa Baba, ili kwamba Mungu awe yote katika yote (taz. 1Kor 15:27-28). Naye aliwashirikisha wanafunzi wake uwezo huu ili nao pia wawekwe katika uhuru wa kifalme na washinde ndani yao wenyewe utawala wa dhambi kwa kujikana wenyewe na kwa utakatifu wa maisha yao (taz. Rum 6:12), na zaidi, wakimtumikia Kristo katika watu wengine, kwa unyenyekevu na saburi wawapeleke ndugu zao kwa Mfalme yule, ambaye kumtumikia yeye ndiko kutawala. Kwa maana Bwana anapenda kuueneza ufalme wake kwa njia pia ya walei waamini, yaani ufalme “wa kweli na uzima, ufalme wa utakatifu na wa neema, ufalme wa haki, mapendo na amani”[115]; katika ufalme huo viumbe vyenyewe vitatolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu (taz. Rum 8:21). Wanafunzi wamepewa yakini ahadi kuu na amri kuu, yaani “vyote ni vyenu, nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu” (1Kor 3:21 na 23).

Basi, yawapasa waamini kutambua maumbile halisi ya viumbe vyote, thamani yake na mpango wake unaoielekea sifa ya Mungu, na kusaidiana wao kwa wao kuishi maisha matakatifu zaidi pia kwa njia ya matendo ya kidunia, ili ulimwengu upenywe na Roho wa Kristo ili ufanikiwe kufikia kikomo chake katika haki, upendo na amani. Katika kuutimiza wajibu huu kwa ajili ya wote, walei wanashika nafasi ya kwanza. Kwa hiyo, kwa ustadi wao katika maarifa ya kidunia na kwa utendaji wao ulioinuliwa kwa ndani na neema ya Kristo, wachangie kwa bidii matendo yao ili mema yaliyoumbwa yasitawishwe kwa kazi ya kibinadamu, kwa ufundi na maarifa kwa ajili ya manufaa ya watu wote kabisa, kadiri ya mpango wa Muumbaji na mwanga wa Neno lake. Tena mema hayo yagawanyike kati ya watu kwa haki inavyofaa na, kwa namna yake, yasaidie maendeleo ya watu wote katika uhuru wa kibinadamu na wa kikristo. Hivyo Kristo kwa njia ya viungo vya Kanisa ataiangaza zaidi na zaidi jamii nzima ya kibinadamu kwa mwanga wake uletao wokovu.

Aidha, yawapasa walei, kwa kuunganisha nguvu zao, waponye taasisi na hali za maisha za ulimwengu, ikiwa zinachochea dhambi katika desturi, hivi kwamba hizo zote ziweze kufuata kanuni za haki na kurahisisha kutenda fadhila badala ya kuwa kizuizi. Kwa kufanya hivyo watapenyeza thamani ya kimaadili katika utamaduni na kazi za binadamu. Kwa namna hiyo shamba la dunia laandaliwa vizuri zaidi kwa ajili ya mbegu iliyo Neno la Mungu, na pamoja na hayo, milango ya Kanisa itakuwa ni wazi zaidi, ili tangazo la amani liuingie ulimwengu.

Kwa ajili ya mpango wa wokovu waamini wajifunze kwa uangalifu kutofautisha kati ya haki na wajibu ambao wanazo, maadamu wameunganika na Kanisa, na zile ziwapasazo kama washiriki wa jamii ya kibinadamu. Wajibidishe kuzioanisha kati yao, wakikumbuka kwamba katika mambo yote ya kidunia yawabidi kuongozwa na dhamiri ya kikristo, kwa sababu hakuna utendaji wa kibinadamu, hata katika mambo ya kidunia, uwezao kuondolewa katika utawala wa Mungu. Katika nyakati zetu inatakiwa hasa kwamba utofautishaji huu pamoja na ulinganifu huu zing’ae kwa namna iliyo dhahiri zaidi iwezekanavyo katika mwenendo wa waamini, ili utume wa Kanisa uweze kuzikabili kikamilifu hali za pekee za ulimwengu wa sasa. Kwa maana, kama vile lazima kukubali ya kwamba mji wa kidunia, ushughulikiao kwa haki mambo ya kidunia, huongozwa na kanuni zake, vivyo hivyo hukataliwa kwa haki mafundisho yale mabaya yatakayo kuijenga jamii bila kuijali dini na kuupinga uhuru wa dini wa raia, na kuuangamiza[116].

Mahusiano na Hierarkia

37. Walei, kama vile waamini wakristo wote, wana haki ya kupokea kwa wingi, kutoka kwa wachungaji wenye Daraja takatifu, mema ya kiroho ya Kanisa, hasa misaada ya Neno la Mungu na ya sakramenti[117]. Basi, wawajulishe wachungaji mahitaji yao na matakwa yao kwa uhuru na matumaini yanavyowapasa watoto wa Mungu na ndugu katika Kristo. Kwa kadiri ya elimu, umahiri na ubora walivyo navyo, wanayo haki, pengine hata wajibu, ya kuyaeleza maoni yao juu ya yale yahusuyo manufaa ya Kanisa[118]. Ikiwa inafaa, hilo litendeke kwa njia ya taasisi zilizopangwa na Kanisa kwa ajili hiyo, na daima [litendeke] katika ukweli, uthabiti na busara, kwa heshima na mapendo kwa wale wanaowakilisha nafsi ya Kristo kutokana na huduma zao takatifu.

Walei, kama vile waamini wakristo wote, washike kwa utii wa kikristo na kwa moyo yale ambayo wachungaji wenye Daraja takatifu, walio mawakili wa Kristo, wanayaamuru kama walimu na viongozi katika Kanisa. Hivyo wanaufuata mfano wa Kristo ambaye, kwa utii wake hata mauti aliwafungulia watu wote njia yenye heri ya uhuru wa watoto wa Mungu. Wala wasiache kuwaombea viongozi wao kwa Mungu, maana wao wanakesha kwa ajili zetu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha, wala si kwa kuugua (taz. Ebr 13:17).

Na wachungaji wenye Daraja takatifu watambue na kukuza hadhi na madaraka ya walei katika Kanisa; watumie kwa moyo mashauri yao yenye busara, wawakabidhi kazi kwa huduma ya Kanisa huku wakiwaamini, wawaachie uhuru na nafasi ya utendaji, zaidi wawatie moyo ili waanzishe matendo kwa hiari yao pia. Kwa uangalifu katika Kristo na upendo wa kibaba wayafikirie makusudio, maombi na mapendekezo yatolewayo na walei[119]. Aidha, wachungaji wataukubali kwa heshima ule uhuru wa haki uwahusuo wote katika mji wa dunia hii.

Mema mengi yatarajiwa kwa ajili ya Kanisa kutokana na mahusiano haya ya karibu kati ya walei na wachungaji. Kwa njia hii hisia ya madaraka yao wenyewe yaimarika ndani ya walei, juhudi zachochewa na nguvu za walei zaunganika kwa urahisi zaidi na kazi ya wachungaji. Wachungaji nao, kwa msaada wa mang’amuzi ya walei, wanaweza kutoa hukumu yao kwa dhahiri na kwa kufaa zaidi katika mambo ya kiroho na ya kidunia; na hivyo Kanisa lote likithibitishwa na viungo vyake vyote, lipate kutimiza utume wake kwa ajili ya uzima wa ulimwengu kwa mafanikio makubwa zaidi.

Walei, roho ya ulimwengu

38. Kila mlei hupaswa kuwa mbele ya ulimwengu shahidi wa ufufuko na maisha ya Bwana Yesu na ishara ya Mungu aliye hai. Yawapasa wote kwa pamoja, na kila mmoja kwa upande wake, kuulisha ulimwengu matunda ya kiroho (taz. Gal 5:22) na kueneza ndani yake ile roho iwahuishayo maskini, wapole na wapatanishi, ambao Bwana aliwatangaza katika Injili kuwa wenye heri (taz. Mt 5:3-9). Kwa neno moja, “kama vile roho ilivyo mwilini, ndivyo wakristo wawe ulimwenguni”[120].

Sura ya Tano

WITO WA WATU WOTE KATIKA KANISA KUWA WATAKATIFU

Utakatifu katika Kanisa

39. Kanisa, ambalo fumbo lake laelezwa na Mtaguso Mkuu, huaminika kuwa daima takatifu. Kwa maana Kristo, Mwana wa Mungu, anayetangazwa pamoja na Baba na Roho Mtakatifu kwamba ni “peke yake mtakatifu”[121], amelipenda Kanisa kama Bibiarusi wake, akajitoa mwenyewe kwa ajili yake ili alitakatifuze (taz. Efe 5:25-26), akaliunganisha naye kama mwili wake, akalijazia kipaji cha Roho Mtakatifu, kwa utukufu wa Mungu. Kwa hiyo wote katika Kanisa, wawe watu wa hierarkia au wawe waongozwao nayo, waitwa kuwa watakatifu, kadiri anavyosema Mtume [Paulo], “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu” (1The 4:3; taz. Efe 1:4). Utakatifu huu wa Kanisa hujidhihirisha bila kukoma, tena ni lazima ujidhihirishe katika matunda ya neema anayozaa Roho ndani ya waamini. Hujieleza kwa njia mbalimbali katika kila mmoja mwenye kujitahidi kuufikia ukamilifu wa upendo katika hali yake ya kawaida ya maisha yake, akiwajenga wengine; kwa namna yake ya pekee hujionyesha katika kutimiza mashauri yaitwayo kwa kawaida ya kiinjili. Utekelezaji huo wa mashauri wanaojitwalia wakristo wengi kwa msukumo wa Roho Mtakatifu, au wenyewe peke yao au katika hali au mpango ulivyokubaliwa na Kanisa, huleta ulimwenguni, tena lazima ulete, ushuhuda na mfano bora wa utakatifu wake [Kanisa].

Wito wa watu wote kuwa watakatifu

40. Bwana Yesu, aliye mwalimu na mfano wa kimungu wa ukamilifu wote, aliwahubiria wanafunzi wake wote na kila mmoja peke yake wenye hali yoyote, utakatifu wa maisha ambao Yeye mwenyewe ndiye mwanzishaji na mtimilizaji wake, “Ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu” (Mt 5:48)[122]. Akawapelekea wote Roho Mtakatifu ili awasukume kwa ndani kumpenda Mungu kwa moyo wote, kwa roho yote, kwa ufahamu wote, na kwa nguvu zote (taz. Mk 12:30), na kupendana kama vile Kristo alivyowapenda (taz. Yn 13:34; 15:12). Wafuasi wa Kristo walioitwa na Mungu siyo kadiri ya matendo yao, bali kadiri ya azimio na neema yake na kuhesabiwa haki katika Bwana Yesu, katika ubatizo wa imani walifanywa kweli watoto wa Mungu na washiriki wa tabia ya Mungu, na hivyo watakatifu halisi. Kwa hiyo yawapasa, kwa msaada wa Mungu, kuushika na kuutimiliza katika maisha yao utakatifu huu waliopewa. Waonywa na Mtume waishi “kama iwastahilivyo watakatifu” (Efe 5:3), na “kwa kuwa wamekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, wajivike moyo wa rehema, utu mwema, unyenyekevu, upole, uvumilivu” (Kol 3:12), na wawe na matunda ya Roho ili wafanywe watakatifu (taz. Gal 5:22; Rum 6:22). Kwa kuwa twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi (taz. Yak 3:2) tunahitaji daima huruma ya Mungu na tunapaswa kusali kila siku, “Utusamehe madeni yetu” (Mt 6:12)[123].

Ni dhahiri kwa wote kwamba waamini wote wakristo wa hali yoyote au daraja lolote huitwa kufikia utimilifu wa maisha ya kikristo na ukamilifu wa upendo[124]: kwa utakatifu huu huhamasishwa kiwango cha maisha kiwafaacho zaidi wanadamu, hata katika jamii ya kidunia. Kwa lengo la kuufikia ukamilifu huo waamini watumie nguvu walizopata kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo, ili wakifuata nyayo zake na kufananishwa na mfano wake, wakiyatii mapenzi ya Baba katika mambo yote, wajitoe kwa moyo wote kwa ajili ya utukufu wa Mungu na huduma ya jirani. Hivyo utakatifu wa Taifa la Mungu utazidi kuzaa matunda tele, kama ilivyoonyeshwa wazi katika historia ya Kanisa kwa njia ya maisha ya watakatifu wengi.

Namna nyingi za kutekeleza utakatifu ulio mmoja

41. Katika aina na wajibu mbalimbali za maisha utakatifu mmoja husitawishwa na wote waongozwao na Roho wa Mungu na, wakiitii sauti ya Baba na kumwabudu Mungu Baba katika roho na kweli, wanamfuata Kristo aliye maskini, mnyenyekevu na mwenye kuchukua msalaba, ili wastahili kushiriki utukufu wake. Yampasa kila mmoja, kadiri ya vipawa vyake na majukumu yake, kuendelea mbele bila kusitasita katika njia ya imani iliyo hai, iamshayo matumaini na kutenda kwa mapendo.

Wachungaji wa kundi la Kristo wapaswa kwanza kabisa, kwa mfano wa Kuhani Mkuu na wa milele, Mchungaji na Mwangalizi (Episcopi) wa roho zetu, kutekeleza kwa utakatifu na shauku, kwa unyenyekevu na uthabiti huduma yao, ambayo ikiwa imetimizwa hivi, itakuwa njia bora ya kujitakatifuza wao wenyewe pia. Wameteuliwa kwa utimilifu wa ukuhani, na wanajaliwa neema ya kisakramenti ili watimize jukumu kamili la upendo wa kichungaji, katika kusali, kujitoa na kuhubiri, na kwa kila mtindo wa uangalizi na huduma ya kiaskofu[125], wasihofu kutoa uhai wao kwa ajili ya kondoo na, wakijifanya vielelezo kwa lile kundi (taz. 1Pet 5:3), walihamasishe Kanisa liufikie utakatifu mkubwa zaidi siku kwa siku, kwa mfano wao pia.

Mapadre, kwa kulandana na Daraja la Maaskofu, ambao ni taji lake la kiroho[126], huku wakishiriki neema ya huduma yao kwa njia ya Kristo, aliye Mshenga wa milele na pekee, wakue katika upendo wa Mungu na wa jirani kwa kutimiza wajibu wao kila siku, watunze kifungo cha ushirika kati ya mapadre, wajae mema yote ya kiroho na watoe kwa wote ushuhuda hai wa Mungu[127], huku wakiwaiga wale mapadre ambao, katika mkondo wa karne nyingi, walitoa mfano mwangavu wa utakatifu, katika huduma iliyokuwa mara nyingi nyenyekevu na iliyositirika. Sifa yao yadumu katika Kanisa la Mungu. Kutokana na wajibu wao, husali na kutoa sadaka kwa ajili ya watu wao na kwa ajili ya taifa lote la Mungu, kwa kufahamu wanayotenda na kuiga wanayoshika[128]. Badala ya kuzuiliwa na shughuli za kitume, na hatari na dhiki, kwa njia ya yayo hayo wakwee kwenye utakatifu wa juu zaidi, wakilisha na kuchochea utendaji wao kwa wingi wa kutafakari, kwa ajili ya faraja ya Kanisa zima la Mungu. Mapadre wote, na hasa waitwao wakleri wa Jimbo kwa hadhi ya pekee ya upadirisho wao, wakumbuke jinsi gani umoja mwaminifu na ushirikiano mkubwa na Askofu wao unavyosaidia utakatifu wao.

Wahudumu pia wa Daraja iliyo chini zaidi wanashiriki kwa namna ya pekee utume na neema ya ukuhani mkuu, na wa kwanza kati yao ni Mashemasi, ambao, kwa kuwa wanayatumikia mafumbo ya Kristo na ya Kanisa[129], wapaswa kujikinga na kila hatia ya uovu na kumpendeza Mungu na kutenda mema yote mbele ya watu (taz. 1Tim 3:8-10 na 12-13). Wakleri wanaoitwa na Bwana na kutengwa ili wawe fungu lake, chini ya uangalizi wa wachungaji wao, na wanaojiandaa kwa wajibu wa wahudumu, wanatakiwa kulinganisha akili zao na mioyo yao na [lengo] la uteule wao mtukufu, wakidumu katika kusali, wakiwa na juhudi katika upendo, wakitafakari mambo yoyote yaliyo ya kweli, yaliyo ya haki na yenye sifa njema, wakitekeleza yote kwa utukufu na heshima ya Mungu. Wanaunganika nao wale walei walioteuliwa na Mungu, ambao wanaitwa na Askofu kusudi wajitoe kabisa kwa matendo ya kitume na wanataabika katika shamba la Mungu wakizaa matunda mengi[130].

Watu wa ndoa na wazazi walio wakristo wapaswa, wakifuata njia yao wenyewe, kutegemezana kwa upendo mwaminifu katika neema kwa muda wote wa maisha yao. Wawafundishe watoto wao waliopokea kutoka kwa Mungu kwa upendo, katika mafundisho ya kikristo na fadhila za kiinjili. Hivyo wanatoa mfano wa upendo usiolegea na wenye ukarimu, wanajenga udugu wa mapendo na wanakuwa mashahidi na washiriki wa uzaaji wa Mama Kanisa, kama ishara na ushirika wa upendo ule, ambao kwao Kristo alimpenda Bibiarusi wake akajitoa kwa ajili yake[131]. Mfano wa aina hii unatolewa kwa namna nyingine na watu wajane na wasiofunga ndoa, [wanawake kwa wanaume], ambao wanaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kwa ajili ya utakatifu na utendaji wa Kanisa. Na wale wanaojishughulisha katika kazi zilizo mara nyingi zenye taabu, wapaswa kwa njia ya matendo ya kibinadamu kujikamilisha wenyewe, kuwasaidia raia, kuhamasisha jamii yote na viumbe vyote viifikie hali bora zaidi. Tena, kwa upendo wenye matendo, huku wakifurahi katika matumaini na kuchukuliana mizigo wao kwa wao, wapaswa kumwiga Kristo, ambaye mikono yake ilizoea kushika vyombo vya kazi na pamoja na Baba daima anatenda kazi kwa ajili ya wokovu wa watu wote; na kwa kazi yao ya kila siku waufikie utakatifu wa juu zaidi, hata ule wa kitume.

Na wale wanaolemewa na umaskini, udhaifu, maradhi na taabu mbalimbali au wanaoudhiwa kwa ajili ya haki, wajue kuwa wanaunganika kwa namna ya pekee na Kristo atesekaye kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu. Bwana katika Injili aliwatangaza kuwa wenye heri, na “Mungu wa neema yote, aliyetuita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, wakiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza na kuwathibitisha na kuwatia nguvu” (1 Pet 5:10).

Basi wakristo wote waamini katika hali, wajibu au mazingira ya maisha yao, na kwa njia ya mambo hayo yote, watatakatifuzwa zaidi na zaidi siku kwa siku ikiwa wanapokea yote kwa imani kutoka kwa mkono wa Baba wa mbinguni na kushirikiana na mapenzi ya Mungu, wakiwaonyesha wote, katika huduma hiyo ya kidunia, upendo ule ambao kwao Mungu aliupenda ulimwengu.

Njia za utakatifu

42. “Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake” (1Yoh 4:16). Mungu amemimina pendo lake katika mioyo yetu kwa njia ya Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi (taz. Rum 5:5); kwa sababu hiyo kipaji cha kwanza na cha lazima zaidi ni upendo, ambao kwao tunampenda Mungu kupita yote na jirani kwa ajili ya Mungu. Lakini kusudi upendo ukue rohoni kama mbegu nzuri na kuzaa matunda, yampasa kila mwamini kusikiliza kwa hamu Neno la Mungu, na kwa msaada wa neema yake kutimiza mapenzi yake kwa matendo, kushiriki mara kwa mara sakramenti, hasa Ekaristi na ibada takatifu, na kujitia kwa uthabiti katika kusali, kujinyima, kuwahudumia ndugu kwa bidii, na kutekeleza fadhila zote. Kwa maana upendo, ulio kifungo cha ukamilifu na utimilifu wa sheria (taz. Kol 3:14; Rum 13:10), huziongoza njia zote za kutakatifuza, huzikamilisha na kuzielekeza zifikie kikomo chake[132]. Kwa hiyo, upendo kwa Mungu na kwa jirani ndio muhuri aliotiwa kila mfuasi wa kweli wa Kristo.

Kwa kuwa Yesu, Mwana wa Mungu, amedhihirisha upendo wake kwa kutoa uhai wake kwa ajili yetu, hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kutoa uhai wake kwa ajili yake Yesu na ndugu zake (taz. 1Yoh 3:16; Yn 15:13). Tangu awali wakristo wengine waliitwa, tena wataitwa sikuzote, kutoa ushuhuda huu mkubwa sana mbele ya watu wote, hasa mbele ya wadhulumu. Kwa hiyo kifodini (martyrium) ambacho kwa njia yake mwanafunzi anafananishwa na mwalimu wake aliyekubali kwa hiari kufa kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu, na kulinganishwa naye katika kuimwaga damu, kinathaminiwa na Kanisa kuwa karama bora na uhakikisho mkuu wa upendo. Ingawa ni wachache wanaojaliwa [neema hii ya kifodini], lakini wote wanapaswa wawe tayari kumkiri Kristo mbele ya watu, na kumfuata katika njia ya msalaba kati ya madhulumu ambayo hayakosekani kamwe katika Kanisa.

Tena utakatifu wa Kanisa hutukuzwa kwa namna ya pekee kwa njia ya mashauri ya aina nyingi ambayo Bwana anawapa wafuasi wake katika Injili ili wayashike[133]. Bora katika hayo ni karama yenye thamani ya neema ya Mungu waliyojaliwa wengine na Baba (taz. Mt 19:11; 1Kor 7:7) ya kujiweka wakfu kwa Mungu tu katika ubikira au katika useja[134] kwa urahisi zaidi na kwa moyo usiogawanyika (taz. 1Kor 7:32-34). Kujinyima huko kikamilifu kwa ajili ya Ufalme wa mbinguni huheshimiwa daima na Kanisa kwa namna ya pekee kama ishara na msukumo wa mapendo na kama chemchemi maalum yenye uwezo wa kuzaa kiroho ulimwenguni.

Kanisa lakumbuka pia onyo la Mtume anayewahimiza waamini wawe na mapendo na kuwaonya kuwa na nia iyo hiyo ndani yao, ambayo ilikuwamo ndani ya Kristo Yesu “aliyejifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa… akawa mtii hata mauti” (Flp 2:7-8) na kwa ajili yetu “amekuwa maskini ingawa alikuwa tajiri” (2Kor 8:9). Ingawa yawapasa wanafunzi kuuiga daima na kuushuhudia upendo huu na unyenyekevu wa Kristo, Mama Kanisa hufurahi kuwa ndani yake kuna idadi kubwa ya wanaume na wanawake wanaofuata kujinyenyekesha kwake Mwokozi kwa karibu zaidi na kukuonyesha wazi zaidi, kwa kushika umaskini kwa uhuru wa wana wa Mungu na kukana mapenzi yao wenyewe. Yaani hao wajitiisha chini ya mtu kwa ajili ya Mungu, na hivi wanakwenda mbele zaidi ya kiasi kilichomo katika amri kuhusu ukamilifu, ili wafanane kikamilifu zaidi na Kristo aliye mtii[135].

Basi waamini wote waalikwa na kupasika kuuelekea utakatifu na ukamilifu kwa kadiri ya hali yao. Kwa hiyo wajitahidi wote kuliongoza pendohisia (affectus) lao inavyotakiwa, ili katika kutumia vitu vya kiulimwengu na kushikwa na tamaa ya mali iliyo kinyume na roho ya umaskini wa kiinjili, wasije wakazuiliwa kuyaelekea mapendo kamili. Kwa maana Mtume aonya, “Wale wautumiao ulimwengu huu [wawe] kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita” (1Kor 7:31)[136].

Sura ya Sita

WATAWA

Mashauri ya kiinjili katika Kanisa

43. Mashauri ya kiinjili ya usafi wa moyo uliowekwa wakfu kwa Mungu, umaskini na utii, yaliyo na misingi juu ya maneno na mifano ya Bwana na kupendekezwa na Mitume, Mababa, Walimu na Wachungaji wa Kanisa, ni kipaji cha Mungu ambacho Kanisa limepewa na Bwana wake na kukitunza daima kwa neema yake. Mamlaka ya Kanisa, chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu, yalifanya bidii kuyafafanua [mashauri hayo], kuratibisha utekelezaji wake na kuasisi, kutokana nao, miundo thabiti ya maisha. Basi ikawa kama ilivyo katika mti uliopandwa na mbegu ya Mungu na kutoa matawi katika shamba la Bwana kwa namna za ajabu nyingi, ziliongezeka njia mbalimbali za maisha ya upweke na ya pamoja, na familia mbalimbali, zinazositawi kwa ajili ya manufaa ya washiriki wake, na kwa ajili ya wema wa Mwili wote wa Kristo[137]. Kwa maana familia hizo huwapatia washiriki wake misaada ya uthabiti mkubwa wa mwenendo wa maisha, ya mafundisho yakubalikayo kwa kuufikia ukamilifu, ya ushirika wa kidugu katika utumishi wa kiaskari wa Kristo, ya uhuru uimarishwao na utii, kusudi waweze kutimiza salama nadhiri zao za kitawa (professionem religiosam) na kuzitunza kwa uaminifu na kuendelea kwa furaha ya kiroho katika njia ya mapendo[138].

Tukizingatia mfumo wa kimungu na wa kihierarkia wa Kanisa, hali hiyo ya kitawa haiko kati ya hali ya kikleri na ya kilei, bali katika makundi haya mawili waamini kadha wa kadha huitwa na Mungu ili wajaliwe kipaji hiki cha pekee katika maisha ya Kanisa, na kuusaidia, kila mmoja kwa namna yake, utume wa Kanisa uletao wokovu[139].

Maumbile na umuhimu wa hali ya kitawa

44. Kwa nadhiri, au vifungo vingine vitakatifu vinavyofanana nazo kwa jinsi zake, ambazo mwamini ajilazimisha kwa hizo kuyashika yale mashauri matatu ya kiinjili yaliyotajwa hapo juu, yeye ajitoa kabisa kwa Mungu aliye mpendwa wake kupita yote, hata awekwe kwa huduma na heshima ya Mungu kwa hadhi mpya na ya pekee. Kwa ubatizo amefia dhambi na kuwekwa wakfu kwa Mungu, lakini kusudi aweze kuzalisha matunda tele zaidi ya neema ya ubatizo, kwa uprofesi (professione) wa mashauri ya kiinjili katika Kanisa ananuia kuopolewa na mapingamizi yawezayo kumzuia kuwa na ari ya upendo na ukamilifu wa ibada kwa Mungu, naye ajiweka wakfu kwa undani zaidi kwa utumishi wa Mungu[140]. Uwakfu huu utazidi kuwa mkamilifu kwa kadiri vitakavyokuwa imara na thabiti vifungo vimwonyeshavyo Kristo afungamanaye kwa namna isiyotanguka na Kanisa aliye Bibiarusi wake.

Kwa kuwa mashauri ya kiinjili, kwa njia ya upendo yanaouelekezea[141], yawaunganisha kwa namna ya pekee wale wanaozitimiza na Kanisa na fumbo lake, maisha yao ya kiroho yapaswa kutolewa pia kwa ajili ya manufaa ya Kanisa zima. Unatokana na hayo wajibu wao wa kufanya kazi, kadiri ya nguvu zao na aina ya wito wao, kwa ajili ya kupandikiza na kuthibitisha Ufalme wa Kristo katika roho za watu, kwa sala na matendo, na kuueneza katika nchi zote. Kwa sababu hiyo Kanisa huhifadhi na kusimamia tabia ya pekee ya mashirika mbalimbali.

Basi uprofesi wa mashauri ya kiinjili unaonekana kuwa kama ishara inayoweza na kupaswa kuwavuta kwa namna ya kufaa wanakanisa wote watimize kwa juhudi wajibu za wito wa kikristo. Maana, kwa kuwa taifa la Mungu halina mji udumuo hapa duniani, bali hutafuta ule ujao, hali ya kitawa iwafanyayo wale waliyoishika kuwa huru zaidi na shughuli za kidunia, hudhihirisha kwa ajili ya waamini wote uwepo wa mema ya mbinguni yaliyopo tayari katika ulimwengu huu; na huushuhudia uzima mpya na wa milele unaopatikana kwa njia ya ukombozi wa Kristo, na kutangaza ufufuko ujao na utukufu wa Ufalme wa mbinguni. Hali ya kitawa huiga pia kwa uaminifu zaidi, na daima huonyesha katika Kanisa, hali ile ya maisha aliyotwaa Mwana wa Mungu alipoingia ulimwenguni ili kuyafanya mapenzi ya Baba, na aliyoipendekeza kwa wanafunzi wake waliomfuata. Hatimaye, huonyesha kwa namna ya pekee Ufalme wa Mungu unavyoinuka juu ya mambo yote ya dunia, na yalivyo madai yake makuu; na kudhihirisha kwa ajili ya watu wote ubora wa ukuu wa uweza wake Kristo Mtawala, na uwezo usio na mipaka wa Roho Mtakatifu atendaye kazi kwa ajabu katika Kanisa.

Basi hali hiyo [ya maisha] inayoundwa kwa uprofesi wa mashauri ya kiinjili, ingawa haingii katika muundo wa kihierarkia wa Kanisa, lakini inahusu kwa hakika maisha yake na utakatifu wake.

Mamlaka ya Kanisa na hali ya kitawa

45. Kwa kuwa wajibu wa Hierarkia ya Kanisa ni kulichunga taifa la Mungu na kuliongoza kwenye malisho mema (taz. Eze 34:14), inaipasa kuratibisha kwa hekima kwa njia ya sheria zake utekelezaji (praxim) wa mashauri ya kiinjili ambayo kwa njia yake ukamilifu wa mapendo kwa Mungu na kwa jirani huchochewa kwa namna ya pekee[142]. Nayo pia ikifuata kwa usikivu misukumo ya Roho Mtakatifu, hupokea kanuni zilizotolewa na wanaume na wanawake mashuhuri, na zikiisha pangwa hata zaidi, hutoa idhini kwa uthabiti. Kwa mamlaka yake yenye uangalizi na utunzo huzisimamia pia mashirika yaliyoasisiwa popote duniani ili kujenga Mwili wa Kristo, yapate kukua na kusitawi kadiri ya roho ya waanzishaji.

Kwa lengo la kusaidia zaidi mahitaji ya kundi zima la Bwana, shirika lolote la kitawa (perfectionis Institutum), na wanashirika wake mmoja mmoja, huweza kuondolewa kutoka kwa mamlaka ya wakuu wa mahali, kwa idhini ya Baba Mtakatifu kwa sababu ya ukuu wake juu ya Kanisa lote, na kuwekwa chini yake tu, kwa ajili ya mafaa ya wote[143]. Vilevile huweza kuachiliwa au kuwekwa (relinqui aut committi) chini ya mamlaka ya [Maaskofu wao wakuu waitwao] Mapatriarka. Wanashirika wenyewe, katika kutimiza wajibu wao kwa akili ya Kanisa kulingana na aina yao ya pekee ya maisha, wapaswa kuwaheshimu na kuwatii Maaskofu, kadiri ya sheria za Kanisa, kwa sababu ya mamlaka yao ya kichungaji juu ya Makanisa [yao] faridi na kwa ajili ya umoja na ulinganifu (concordiam) uhitajikao katika kazi ya kitume[144].

Kanisa kwa idhini yake haliinui tu nadhiri za kitawa kuwa na hadhi ya hali ya kikanuni (ad status canonici dignitate), lakini kwa adhimisho lake la kiliturujia huziweka katika hali ya uwakfu kwa Mungu. Kwa maana Kanisa lenyewe, kwa mamlaka liliyokabidhiwa na Mungu, hupokea nadhiri za maprofesi (profitentium vota suscipit), huwaombea kwa sala ya hadharani [wajaliwe] misaada na neema ya Mungu, huwaweka mikononi mwa Mungu na kuwapa baraka ya kiroho, likiunganisha matoleo yao na sadaka ya Ekaristi.

Ukuu wa kujiweka wakfu kwa Mungu

46. Watawa wafanye bidii sana ili kwa njia yao wenyewe Kanisa limdhihirishe kwa uwazi zaidi siku kwa siku, kwa waamini na wasioamini, Kristo, ama [kama yuko katika hali ya] kutafakari mlimani, au akiuhubiria umati Ufalme wa Mungu, ama akiwaponya wagonjwa na wenye jeraha, au akiwaongoa wakosefu wazae matunda mema, au akiwabariki watoto na kuwatendea mema watu wote, akiyatii daima mapenzi ya Baba aliyemtuma[145].

Mwishowe wote wajue kwamba uprofesi wa mashauri ya kiinjili, ingawa unasababisha kuacha mambo yenye heshima yanayothamanika sana, lakini haupingi maendeleo ya kweli ya nafsi ya kibinadamu, bali kwa tabia yake huifaidia sana. Kwa maana mashauri haya, yakipokelewa kwa hiari kadiri ya wito wa kila mmoja, husaidia sana takaso la moyo na uhuru wa kiroho, huwasha daima moto wa mapendo na hasa huweza kumlinganisha mkristo na aina ile ya maisha ya kibikira na kimaskini aliyojichagulia Kristo Bwana na ambayo Mama yake Bikira aliifuata, kama ilivyothibitishwa na mifano ya waanzishaji (fundatorum) wengi watakatifu. Mtu yeyote asidhani kwamba watawa kwa kujiweka wakfu wamekuwa wageni kwa watu na wasiofaa katika mji wa kidunia. Kwa maana, ijapo wengine hawakai pamoja (non directe adsistunt) na watu wa wakati wao, lakini wanawakumbuka kwa namna ya kindani zaidi katika mtima wa Kristo, na kushirikiana nao kiroho ili jengo la mji wa kidunia liwe daima na msingi katika Bwana na kumwelekea Yeye, isije ikatokea kwamba wanafanya kazi bure waujengao[146].

Kwa sababu hiyo Mtaguso Mtakatifu huwathibitisha na kuwasifu wanaume na wanawake, ndugu wa kiume na ndugu wa kike, ambao monasterini au katika mashule na hospitali, au mishenini, kwa uaminifu mdumifu na mnyenyekevu katika uwakfu wao, wanampamba Bibiarusi wa Kristo na kuwahudumia watu wote kwa moyo na kwa namna nyingi.

Kuhimiza udumifu

47. Kila mmoja aitwaye kwa uprofesi wa mashauri, afanye juhudi kubwa ili kudumu na kuwa bora zaidi katika wito ule ambao Mungu alimwita, ili Kanisa lipate utakatifu mkubwa zaidi, na kwa ajili ya utukufu mwingi zaidi wa Utatu mmoja na usiogawanyika, ulio chemchemi na asili ya utakatifu wote katika Kristo na kwa njia ya Kristo.

Sura ya Saba

TABIA YA KIESKATOLOJIA YA KANISA LINALOSAFIRI

NA UMOJA NA KANISA LILILO MBINGUNI

Tabia ya kieskatolojia ya wito wetu

48. Kanisa, ambalo sisi sote twaitwa kwake katika Kristo Yesu na ndani yake tunapata utakatifu kwa neema ya Mungu, halitapata utimilifu wake isipokuwa katika utukufu wa mbinguni, hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote (taz. Mdo 3:21). [Na wakati huo], pamoja na jamii ya watu ulimwengu wote pia, ambao umeunganika kwa undani na mwanadamu (intime cum homine coniungitur), na kwa njia yake unafikilia shabaha yake, utajumlishwa (instaurabitur) kikamilifu katika Kristo (taz. Efe 1:10; Kol 1:20; 2Pet 3:10-13).

Kristo alipoinuliwa juu ya nchi aliwavuta wote kwake (taz. Yn 12:32); akiisha kufufuka katika wafu (taz. Rum 6:9) akamtuma ndani ya wanafunzi wake Roho wake mleta uzima, na kwa njia yake akauweka Mwili wake ulio Kanisa kuwa sakramenti ya wokovu kwa wote. Akikaa kuume kwa Baba, daima hutenda kazi ulimwenguni ili awaongoze wote kwenye Kanisa na kwa njia yake awaunganishe naye zaidi na, kwa kuwalisha Mwili wake na Damu yake mwenyewe, kuwashirikisha katika maisha ya utukufu wake. Basi kule kutengeneza upya tulikoahidiwa na tunakongojea, kumekwisha anza tayari katika Kristo, kunaendelezwa mbele kwa utume wa Roho Mtakatifu, na kudumu kwa njia yake katika Kanisa. Ndani yake [Kanisa] twafundishwa kwa imani maana ya maisha yetu ya muda, hadi tuimalize kwa tumai la mema yajayo, kazi tuliyokabidhiwa na Baba katika ulimwengu huu, na kutimiza wokovu wetu wenyewe (taz. Flp 2:12).

Basi, miisho ya zamani imekwisha kutufikia (taz. 1Kor 10:11), kufanywa upya kwa ulimwengu kumekwisha wekwa bila kutenguliwa, na kwa hakika kabisa kumeanza kuonjwa kweli toka sasa; kwa kweli Kanisa hata hapa duniani limepambwa utakatifu wa kweli ingawa si mkamilifu. Lakini mpaka hapo zitakapokuwepo mbingu mpya na dunia mpya ambamo haki yakaa ndani yake (taz. 2Pet 3:13), Kanisa linalosafiri, katika sakramenti zake na taasisi zake zilizo za wakati huu, linachukua sura ya ulimwengu huu unaopita na linaishi kati ya viumbe ambavyo vinaugua na vina utungu hata sasa na vinatazamia kwa shauku nyingi kufunuliwa kwa wana wa Mungu (taz. Rum 8:19-22).

Tukiwa tumeunganishwa na Kristo katika Kanisa na kutiwa muhuri wa Roho Mtakatifu “aliye arbuni ya urithi wetu” (Efe 1:14), twaitwa kweli wana wa Mungu, na ndivyo tulivyo (taz. 1Yoh 3:1), lakini hatujafunuliwa bado pamoja na Kristo katika utukufu (taz. Kol 3:4) ambao ndani yake tutafanana na Mungu kwa maana tutamwona kama alivyo (taz. 1Yoh 3:2). Kwa hiyo, “wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana” (2Kor 5:6) na sisi wenyewe tulio na malimbuko ya Roho, sisi pia tunaugua katika nafsi zetu (taz. Rum 8:23) na tunatamani kwenda zetu tukae na Kristo (Flp 1:23). Upendo wenyewe hutubidisha tuishi zaidi kwa ajili yake Yeye aliyekufa na kufufuka (taz. 2Kor 5:15). Kwa hiyo twajitahidi kumpendeza Bwana katika yote (taz. 2Kor 5:9) na twazivaa silaha zote za Mungu tupate kuweza kuzipinga hila za shetani na kushindana siku ya uovu (taz. Efe 6:11-13). Kwa kuwa hatujui siku wala saa yatupasa kukesha daima kama Bwana anavyotuonya ili, ikishamalizika safari iliyo moja tu ya maisha yetu duniani (taz. Ebr 9:27), tustahili kuingia pamoja naye katika karamu ya arusi na kuhesabiwa miongoni mwao waliobarikiwa [na Mungu] (taz. Mt 25:31-46) na wala asituamuru kama watumwa wabaya na walegevu (taz. Mt 25:26) kwenda katika moto wa milele (taz. Mt 25:41) na katika giza la nje ambako “ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno” (Mt 22:13 na 25:30). Kwa maana, kabla ya kutawala pamoja na Kristo mtukufu, sisi sote tutadhihirishwa “mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya” (2Kor 5:10), na mwisho wa dunia “watatoka, wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu” (Yn 5:29; taz. Mt 25:46). Basi tukiyahesabu “mateso ya wakati huu wa sasa kuwa si kitu kama utukufu ule utakaofunuliwa kwetu” (Rum 8:18; taz. 2Tim 2:11-12), kwa imani thabiti twalitazamia “tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu Mkuu na Mwokozi wetu” (Tit 2:13), “atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu” (Flp 3:21), na atakayekuja “ili kutukuzwa katika watakatifu wake, na kustaajabiwa katika wote waliosadiki” (2The 1:10).

Ushirika wa Kanisa la mbinguni na Kanisa linalosafiri

49. Mpaka Bwana atakapokuja katika utukufu wake na malaika wote pamoja naye (taz. Mt 25:31), na vitu vyote kutiishwa chini ya miguu yake baada ya kubatilishwa mauti (taz. 1Kor 15:26-27), wanafunzi wake wengine husafiri duniani, wengine walioaga dunia hii hutakaswa, na wengine wanatukuzwa wakimtazama katika nuru timilifu Mungu huyu mmoja katika nafsi tatu, jinsi alivyo[147]Lakini sisi sote, ingawa kwa hatua na namna mbalimbali, tunashirikiana katika upendo uleule wa Mungu na jirani na kumwimbia Mungu wetu utenzi uleule wa utukufu. Kwa maana wale wote walio wa Kristo, walio na Roho wake, waungamanishwa katika Kanisa moja na kushikanishwa katika Yeye (taz. Efe 4:16). Kwa hiyo, umoja wa wale wanaosafiri duniani na wa ndugu waliolala katika amani ya Kristo haukatiki hata kidogo, kinyume chake, kadiri ya imani ya daima ya Kanisa [umoja huo] huimarishwa kwa kubadilishana mema ya kiroho[148]. Hivyo wale walio mbinguni, kwa kuwa wameunganika na Kristo kwa undani zaidi, wanaliimarisha Kanisa lote katika utakatifu kwa uthabiti zaidi, wanakuza ibada zinazotolewa nalo kwa Mungu hapa duniani na kusaidia kulijenga zaidi na zaidi kwa njia mbalimbali (taz. 1Kor 12:12-27)[149]. Kwa maana, baada ya kupokelewa mbinguni na kukaa pamoja na Bwana (taz. 2Kor 5:8), kwa njia yake, pamoja naye na ndani yake, hawaachi kutuombea kwa Baba[150], wakimtolea mastahili yao waliyojipatia duniani kwa njia ya Kristo Yesu aliye Mpatanishi pekee kati ya Mungu na wanadamu (taz. 1Tim 2:5), kwa kumtumikia Bwana katika yote na kuyatimiliza katika miili yao yale yaliyopungua ya mateso ya Kristo kwa ajili ya mwili wake, yaani, Kanisa (taz. Kol 1:24)[151]. Hivyo udhaifu wetu husaidiwa sana na juhudi yao ya kidugu.

Mahusiano kati ya Kanisa linalosafiri duniani na Kanisa la mbinguni

50. Kanisa la wale wanaosafiri, huku likiufahamu vizuri ushirika huu wa Mwili mzima wa Fumbo wa Yesu Kristo, tangu awali ya dini ya kikristo lilikuza kwa heshima kubwa ukumbusho wa marehemu[152] na, kwa sababu “ni wazo takatifu na la kicho kufanya upatanisho kwa wafu ili wafunguliwe dhambi zao” (taz. 2Mak 12:46), likatolea maombezi kwa ajili yao. Kanisa limesadiki daima kwamba mitume na mashahidi wa Kristo, waliotoa ushuhuda mkubwa wa imani na mapendo kwa kumwaga damu yao, wameunganika nasi kwa namna ya pekee katika Kristo; likawaheshimu kwa upendo wa pekee pamoja na Bikira Maria Mwenye heri na malaika watakatifu[153] na kuwaomba kwa uchaji msaada wa maombezi yao. Baadaye wamehesabika pamoja nao wengine pia walioiga kwa karibu zaidi ubikira na umaskini wa Kristo[154], na mwishowe wengine ambao utimizaji wao bora wa fadhila za kikristo[155] na karama za Mungu ziliwapendekeza kwa waamini hata wawaheshimu kwa utauwa na kuwaiga[156].

Kwa maana tukiangalia maisha ya wale waliomfuata Kristo kiaminifu, tunahimizwa upya kuutafuta Mji ule ujao (taz. Ebr 13:14 na 11:10), na pamoja na hayo twafundishwa njia salama kabisa ya kuufikia, kati ya mabadiliko ya ulimwengu, umoja kamili na Kristo, ndio utakatifu, kila mmoja kadiri ya wito wake na hali yake[157]. Katika maisha ya wale wanaobadilishwa wafanane kikamilifu zaidi na mfano wa Kristo (taz. 2Kor 3:18), ijapo wanashiriki hali yetu ya kibinadamu, Mungu huwadhihirishia watu wazi uwepo wake na uso wake. Ndani yao Yeye mwenyewe husema nasi na kutuonyesha alama ya Ufalme wake[158], ambao tunavutwa kwake kwa nguvu, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii (taz. Ebr 12:1) na kuwa na ushuhuda wa namna hii wa ukweli wa Injili.

Lakini hatuheshimu kumbukumbu ya watakatifu wa mbinguni kwa sababu ya mfano [wao] tu, bali zaidi ili umoja wa Kanisa zima katika Roho [Mtakatifu] uimarishwe kwa zoezi la mapendo ya kidugu (taz. Efe 4:16). Kwani, kama vile ushirika kati ya [wakristo] wasafirio [duniani] unavyotusogeza karibu zaidi na Kristo, vivyo hivyo umoja na watakatifu unatuunganisha na Kristo, ambaye kwake yeye, kama Chemchemi na Kichwa, hutoka neema zote na uzima wenyewe wa taifa la Mungu[159]. Kwa hiyo yafaa kabisa tuwapende rafiki hawa wa Yesu Kristo na warithi pamoja naye, walio ndugu na wafadhili wetu wakuu, na tumshukuru Mungu ipasavyo kwa ajili yao[160] na “tuwasihi sana na kuyakimbilia maombezi yao, nguvu zao na msaada wao ili tujaliwe na Mungu fadhili zake kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo, Bwana wetu aliye peke yake Mkombozi wetu na Mwokozi wetu”[161]. Kwa maana kila kielezo halisi cha upendo wetu kwa ajili ya watakatifu, kadiri ya tabia yake, humwelekea Kristo na kutekelezwa kwake yeye aliye “taji la watakatifu wote”[162], na kwa njia yake kwa Mungu aliye wa ajabu katika watakatifu wake na kutukuzwa ndani yao[163].

Umoja wetu na Kanisa la mbinguni hutimizwa kwa njia bora tunapoadhimisha sifa ya Mungu Mwenyezi kwa shangwe moja, hasa katika Liturujia takatifu, ambamo uwezo wa Roho Mtakatifu hutenda kazi ndani yetu kwa ishara za sakramenti[164], na sisi sote, watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa tulionunuliwa kwa damu ya Kristo (taz. Ufu 5:9), tuliokusanyika katika Kanisa moja, twamtukuza Mungu aliye Mmoja na Utatu Mtakatifu kwa wimbo mmoja wa sifa. Kwa hiyo katika kuadhimisha sadaka ya Ekaristi tunaunganika sana na ibada ya Kanisa la mbinguni tukishirikiana nalo, na tukimheshimu na kumkumbuka kwanza Maria mtukufu Bikira daima, na pia Yusufu mwenye heri, na Mitume na mashahidi wenye heri na watakatifu wote[165].

Maagizo ya kichungaji ya Mtaguso Mkuu

51. Mtaguso huu Mtakatifu huipokea kwa utauwa mkubwa imani hii stahivu ya mababa wetu mintarafu muungano wetu wenye uhai na ndugu ambao wapo katika utukufu wa mbinguni au wapo bado katika kutakaswa baada ya kufa kwao, na kukumbusha tena Maagizo ya Mtaguso wa pili wa Nikea[166], ya Mtaguso wa Florenzia[167] na Trento[168]. Pamoja na haya kwa bidii yake ya kichungaji unawaonya wote wanaohusika wajitahidi kuepuka au kusahihisha desturi mbaya, mambo yapitayo kiasi au yaliyo na mapungufu fulani, ambayo labda yameingia hapa na pale, na wayatengeneze upya yote, ili Kristo na Mungu wasifiwe kikamilifu zaidi. Wawafundishe waamini kwamba heshima ya kweli ya watakatifu (sanctorum cultum) hutegemea siyo wingi wa matendo mbalimbali ya nje, bali nguvu ya upendo wetu wenye utendaji, ambao kwao twatafuta, kwa manufaa yetu na ya Kanisa, “mfano katika maisha yao, urafiki kwa kuungana nao na msaada kwa njia ya maombezi yao”[169]. Kwa upande mwingine yapasa kuwafundisha waamini kwamba uhusiano wetu na wale [watakatifu] walio mbinguni, mradi umefahamika katika mwanga mkubwa zaidi wa imani, haupunguzi ibada ya kumwabudu Mungu Baba itolewayo kwake kwa njia ya Kristo katika Roho, bali kinyume chake huzidi kuisitawisha[170].

Kwa maana sisi sote tulio watoto wa Mungu na kuwa familia moja katika Kristo (taz. Ebr 3:6), tunaposhirikiana sisi kwa sisi katika kupendana na katika kutoa sifa moja kwa Utatu Mtakatifu, tunaitikia wito halisi wa Kanisa na kushiriki Liturujia ya utukufu kamili, tukiionja tangu sasa[171]. Kwa maana Kristo atakapotokea na wafu wakifufuka kwa utukufu, fahari ya Mungu itautilia nuru mji wa mbinguni na taa yake itakuwa ni Mwanakondoo (taz. Ufu 21:23). Ndipo Kanisa lote la watakatifu, katika heri kubwa ya mapendo, litakapomwabudu Mungu na “Mwanakondoo aliyechinjwa” (Ufu 5:12) likitangaza kwa sauti moja: “Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwanakondoo, hata milele na milele” (Ufu 5:13).

Sura ya nane

BIKIRA MARIA MWENYE HERI MAMA WA MUNGU

KATIKA FUMBO LA KRISTO NA LA KANISA

I. UTANGULIZI

52. Mungu mwenye fadhili na hekima tele, akitaka kuutimiza ukombozi wa ulimwengu, “ulipowadia utimilifu wa wakati alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke... ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana” (Gal 4:4-5). Naye “ameshuka toka mbinguni kwa ajili yetu sisi wanadamu na kwa ajili ya wokovu wetu, akapata mwili kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwake yeye Bikira Maria”[172]. Fumbo hili la wokovu la Mungu limefunuliwa kwetu na kuendelezwa katika Kanisa, ambalo Bwana ameweka kuwa mwili wake, na ndani yake waamini, wanaoambatana na Kristo aliye Kichwa [chao] na kushirikiana na watakatifu wake wote, wapaswa pia “kumheshimu kwanza Maria mtukufu daima Bikira, Mama wa Mungu na Bwana wetu Yesu Kristo”[173].

Maria na Kanisa

53. Bikira Maria, aliyepokea kwa ujumbe wa Malaika Neno wa Mungu moyoni mwake na mwilini mwake na kuuletea ulimwengu Uzima, anatambuliwa na kuheshimiwa kuwa kweli Mama wa Mungu na wa Mkombozi. Yeye aliyekombolewa kwa njia bora sana kwa kutazamiwa mastahili ya Mwanae, na kuunganika naye kwa kifungo imara kisichofungulika, amejaliwa cheo kikuu na hadhi ya kuwa Mzazi wa Mwana wa Mungu, na kwa sababu hiyo ndiye binti mpenzi wa Baba na hekalu la Roho Mtakatifu. Kwa ajili ya kipaji hiki cha neema kuu anavizidi sana viumbe vingine vyote vilivyo mbinguni na duniani. Pamoja na hayo anaonekana ameunganika, katika uzao wa Adamu, na watu wote wanaohitaji wokovu; na zaidi, yeye ni pia “mama kweli wa viungo (vya Kristo) ... kwa sababu … alishiriki kwa mapendo yake ili waamini wazaliwe katika Kanisa, ambao ndio viungo vya Kichwa hicho[174]. Kwa sababu hiyo husalimiwa kama kiungo kikuu na cha pekee cha Kanisa na mfano wake mtimilifu (typus) na kielelezo (exemplar) chake bora sana katika imani na katika mapendo; na Kanisa katoliki, likifundishwa na Roho Mtakatifu, humheshimu kwa upendo na heshima wa kimwana kama mama yake mpenzi sana.

Madhumuni ya Mtaguso Mkuu

54. Mtaguso Mkuu katika kutoa mafundisho mintarafu Kanisa ambamo Mkombozi Mungu hutenda wokovu, unanuia kueleza kwa uangalifu dhima ya Bikira Mwenye heri katika fumbo la Neno aliyefanyika mwili na la Mwili wake wa fumbo. Pia [unataka kufafanua] wajibu wa watu waliokombolewa kumhusu Mama wa Mungu (Deiparam), aliye mama wa Kristo na mama wa wanadamu, hasa wa waamini. Lakini Mtaguso hauna nia ya kutoa mafundisho yaliyotimilika juu ya Maria, wala kukata masuala yasiyoelezwa bado wazi na kazi ya wanateolojia. Kwa hiyo yanabaki halali (in suo iure) maoni yapendekezwayo katika shule katoliki mintarafu yule anayeshika katika Kanisa takatifu mahali pa kwanza baada ya Kristo, na pa karibu zaidi nasi[175].

II. DHIMA YA BIKIRA MARIA KATIKA MPANGO WA WOKOVU

Mama wa Masiya katika Agano la Kale

55. Maandiko Matakatifu ya Agano la Kale na ya Agano Jipya na Mapokeo ya kale yaonyesha wazi zaidi na zaidi dhima ya Mama wa Mwokozi katika mpango wa wokovu, na kuiweka mbele yetu tuifikirie. Vitabu vya Agano la Kale vyaeleza historia ya wokovu ambayo ndani yake hutayarishwa polepole ujio wa Kristo ulimwenguni. Maandiko hayo ya Kale, yanavyosomwa katika Kanisa na kufahamika katika mwanga wa ufunuo kamili wa baadaye, hatua kwa hatua yabainisha zaidi na zaidi sura ya yule mwanamke aliye Mama wa Mkombozi. Katika mwanga huu anabashiriwa kinabii katika ahadi ya ushindi juu ya nyoka waliyopewa wazazi wa kwanza baada ya kutenda dhambi (taz. Mwa 3:15). Vilevile yeye ni Bikira yule atakayepata mimba na kumzaa Mtoto mwanamume ambaye jina lake ataitwa Emanueli (taz. Isa 7:14; Mik 5:2-3; Mt 1:22-23). Yeye anashika nafasi ya kwanza miongoni mwa wanyenyekevu na maskini wa Bwana, ambao, kwa matumaini ya imani wanangojea na wanapata wokovu kwake. Hatimaye, kwa yeye, Binti mtukufu wa Sayuni aliye bora sana, baada ya kungojea ahadi kwa muda mrefu, nyakati zilitimia na mpango mpya wa wokovu ukawekwa, hapo Mwana wa Mungu alipotwaa maumbile ya kibinadamu kutoka kwake, ili amkomboe mwanadamu katika dhambi kwa mafumbo ya mwili wake.

Maria katika kutangazwa habari njema

56. Mungu wa huruma alitaka Umwilisho utanguliwe na ukubali wake yeye aliyeteuliwa tangu milele awe Mama, ili kama vile mwanamke alivyoshiriki kuileta mauti, kadhalika mwanamke asaidie kuuleta uzima. Hayo yamhusu kwa namna ya pekee Mama wa Yesu aliyeuzalia ulimwengu Uzima wenyewe, utengenezao yote upya, naye alitajirishwa na Mungu kwa karama zenye kustahili jukumu hili kubwa hivi. Kwa hiyo hatuwezi kushangaa ikiwa Mababa Watakatifu walizoea kumwita Mama wa Mungu kuwa “Mtakatifu kabisa”, bila doa lolote la dhambi, kama aliyetengenezwa na Roho Mtakatifu na kufanywa kuwa kiumbe kipya[176]. Hali amepambwa tangu nukta ya kwanza ya kutungwa kwake mimba kwa mng’aro wa utakatifu wa pekee kabisa, Bikira huyu wa Nazareti aliamkiwa na Malaika mhubiri (Angelo nuntiante), kwa amri ya Mungu, kuwa “amejaa neema” (gratia plena) (taz. Lk 1:28), naye akamjibu mjumbe wa mbinguni, “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana, na iwe kwangu kama ulivyosema” (Lk 1:38). Hivyo Maria, binti Adamu, kwa kulikubali Neno la Mungu amekuwa Mama wa Yesu, na akiyakumbatia kwa roho yake yote, na bila kushikwa na dhambi yoyote, mapenzi ya Mungu yenye wokovu, akajitoa kabisa kama mjakazi wa Bwana kwa ajili ya nafsi ya Mwanawe na kwa kazi yake, akilihudumia fumbo la ukombozi chini yake na pamoja naye, kwa neema ya Mungu Mwenyezi. Kwa hiyo Mababa Watukufu huona kwa haki kuwa Maria hakutumiwa na Mungu katika hali ya kutendwa tu, bali alishiriki kuleta wokovu wa binadamu kwa imani [yake] na utii [wake] wa hiari. Kwa maana, kama vile Mt. Ireneus asemavyo, yeye “kwa kutii amekuwa sababu ya wokovu kwa ajili yake na kwa ajili ya kizazi chote cha wanadamu”[177]. Ndiyo sababu, Mababa wa Kanisa wasio wachache hupenda kueleza katika mahubiri yao kwamba “fundo la kutotii kwa Hawa limefunguliwa kwa utii wa Maria; na kile ambacho Hawa bikira alifunga kwa kutosadiki kwake, Bikira Maria alikifungua kwa imani yake”[178]. Wakimfananisha [Maria] na Hawa, wanamwita Maria “Mama wa walio hai”[179], na mara nyingi wanatangaza, “Mauti kwa njia ya Hawa; kwa njia ya Maria uzima”[180].

Maria wakati wa utoto wa Yesu

57. Umoja huu wa Maria na Mwanawe katika kazi ya wokovu unaonekana tangu dakika ile Bikira alipotunga mimba Kristo mpaka kifo chake. Kwanza, Maria alipoondoka kwenda kwa haraka kumwamkia Elisabeti akasalimiwa naye kuwa mwenye heri kwa imani yake katika wokovu ulioahidiwa, na mtangulizi akaruka ndani ya tumbo la mama yake (taz. Lk 1:41-45); tena, wakati wa kuzaa, Mama wa Mungu alipowaonyesha wachungaji na mamajuzi kwa furaha Mwana wake mzaliwa wa kwanza, asiyepunguza ukamilifu wa ubikira wake, bali akautakatifuza[181]. Na alipomtolea Bwana hekaluni, pamoja na sadaka ya maskini, alimsikia Simeoni akiagua kwamba Mwanae atakuwa ishara itakayonenewa, na kwamba upanga utaingia moyoni mwake mama ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi (taz. Lk 2:34-35). Walipomkosa mtoto Yesu na kumtafuta kwa huzuni, wazazi wake wakamwona hekaluni akiyashughulikia yale yaliyo ya Baba yake, wala hawakuelewa na neno la Mwana. Lakini mama yake aliyaweka haya yote moyoni mwake akiyatafakari (taz. Lk 2:41-51).

Maria katika maisha ya hadharani ya Yesu

58. Katika maisha ya hadharani ya Yesu, mama yake alijionyesha tangu mwanzo kwa njia ya pekee katika arusi ya Kana ya Galilaya, aliposababisha kwa huruma yake chanzo cha ishara za Yesu aliye Masiya, kwa njia ya maombezi yake (taz. Yn 2:1-11). Wakati wa kuhubiri kwake Mwanae, alipokea maneno ambayo kwayo yeye, akiuinua Ufalme juu ya mahusiano na vifungo vya mwili na damu, alitangaza kuwa wenye heri wale wanaolisikia na kulitunza Neno la Mungu (taz. Mk 3:35; Lk 11:27-28), kama alivyofanya Maria kwa uaminifu (taz. Lk 2:19 na 51). Hivyo Bikira Maria pia aliendelea mbele katika safari ya imani, alihifadhi kwa uaminifu muungano wake na Mwanawe, mpaka kufika penye msalaba (taz. Yn 19:25), ambapo alisimama imara, kwa mpango wa Mungu; aliteswa kikatili pamoja na Mwanawe wa pekee, na alijiunganisha kwa moyo wake wa kimama na sadaka yake. Alikubali kwa upendo sadaka aliyojitoa yule dhabihu aliyemzaa mwenyewe. Mwishowe alikabidhiwa na Yesu mwenyewe akifa msalabani kama mama yake kwa mwanafunzi kwa maneno haya, “Mama, tazama mwanao” (taz. Yn 19:26-27)[182].

Maria baada ya kupaa kwake Bwana

59. Kwa kuwa ilimpendeza Mungu sakramenti ya wokovu wa wanadamu isidhihirishwe kitukufu kabla ya kumimina Roho aliyeahidiwa na Kristo, tunawaona Mitume kabla ya siku ya Pentekoste “wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake na Maria, Mama yake Yesu, na ndugu zake” (Mdo 1:14). Hata Maria aliomba kwa sala zake paji la Roho ambaye alimfunika tayari kama kivuli siku ya kutangazwa kwake. Mwishowe, Bikira asiye na doa, aliyekingiwa na kila doa la dhambi ya asili[183], akishamaliza mwendo wa maisha yake duniani, aliinuliwa katika utukufu wa mbinguni pamoja na mwili [wake] na pamoja na roho [yake][184]; akatukuzwa na Bwana kama Malkia wa ulimwengu, ili afananishwe kikamilifu zaidi na Mwanawe, aliye Bwana wa mabwana (taz. Ufu 19:16) na mshindi wa dhambi na mauti[185].

III. BIKIRA MWENYE HERI NA KANISA

Kristo aliye mpatanishi wa pekee na Maria

60. Mpatanishi wetu ni mmoja tu kadiri ya maneno ya Mtume, “Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu, ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote” (1Tim 2:5-6). Huduma ya kimama ya Maria kwa watu haiutilii giza upatanisho huu wa pekee wa Kristo, wala kuupunguza kwa namna yoyote ile, bali yaonyesha nguvu zake. Kwa kweli kila mvuto wa wokovu kwa upande wa Bikira Mwenye heri kwa watu hautoki katika lazima fulani bali katika mapenzi ya Mungu, na kububujika kutoka wingi wa mastahili ya Kristo. Una msingi wake katika upatanisho wake, na huutegemea kabisa, huchota toka humo nguvu yake yote, wala hauzuii kwa namna yoyote muungano wa moja kwa moja wa waamini na Kristo, bali unausaidia.

Maria anashiriki katika kazi ya ukombozi

61. Bikira Mwenye heri aliyeteuliwa tangu milele kuwa Mama wa Mungu, pamoja na [azimio la] umwilisho wa Neno wa Mungu, kwa mpango wa Maongozi ya Mungu amekuwa hapa duniani Mama Mtukufu wa Mkombozi aliye Mungu, mwenzi mwenye moyo mkuu kwa namna ya pekee kuliko wote, na mjakazi mnyenyekevu wa Bwana. Kwa kumtunga mimba na kumzaa Kristo, kwa kumlisha, kumtolea kwa Baba hekaluni, kwa kuteswa pamoja na Mwanae aliyekufa msalabani, alishiriki kwa namna iliyo ya pekee kabisa kazi ya Mwokozi kwa utii wake na imani, matumaini na mapendo yake yenye kuwaka, ili uzima wa kimungu utengenezwe upya katika roho [za wanadamu]. Kwa sababu hiyo amekuwa mama kwa ajili yetu katika mpango wa neema.

Mwombezi kwa ajili ya wokovu

62. Umama huu wa Maria katika mpango wa neema unadumu bila kukatizwa tangu nukta ile ya ukubali aliotoa kwa imani wakati wa tangazo [la kuzaliwa Bwana] na alioushikilia bila kusita chini ya msalaba, hadi ukamilifu wa milele wa wateule wote. Kwa kweli, akiwa amepalizwa mbinguni, hakuacha huduma hii ya wokovu, bali kwa njia ya maombezi yake ya namna nyingi anaendelea kupata kwa ajili yetu mapaji ya wokovu wa milele[186]. Kwa mapendo yake ya kimama, huwaangalia ndugu wa Mwanawe wanaohiji bado na kuishi katika hatari na taabu, mpaka watakapofikishwa kwenye makao yenye furaha. Kwa sababu hiyo, Bikira mwenye heri huombwa katika Kanisa kwa majina haya ya heshima: Mtetezi, Msaidizi, Mfadhili na Mpatanishi[187]. Lakini haya yaeleweke vizuri, ili kitu chochote kisipunguze au kuongeza hadhi na uwezo wa Kristo aliye Mpatanishi peke yake[188].

Kwa maana hakuna kiumbe chochote kiwezacho kulinganishwa na Neno aliyejifanya mwili na Mkombozi; lakini kama vile ukuhani wa Kristo unavyoshirikishwa kwa namna mbalimbali kwa wahudumu [watakatifu] na kwa watu waamini, na kama vile wema wa pekee wa Mungu unavyoenea kweli kwa namna mbalimbali katika viumbe, ndivyo upatanisho pekee wa Mkombozi hauzuii, bali unaamsha katika viumbe ushirikiano wa namna mbalimbali unaochotwa katika chemchemi moja tu.

Kanisa halisiti kuikiri wazi huduma hii ya Maria iliyowekwa chini [ya ile ya Kristo], huionja daima na kuikabidhi mioyoni mwa waamini, ili, wakitegemezwa na msaada huu wa kimama, waambatane kwa undani zaidi na Mpatanishi na Mkombozi.

Maria bikira na mama, mfano mtimilifu wa Kanisa

63. Bikira Mwenye heri, kwa kipaji na dhima ya umama wa kimungu unaomwunganisha na Mwanae Mkombozi, na kwa neema zake na huduma zake za pekee, ameunganika pia kwa undani na Kanisa. Mama wa Mungu ni kielezo (typus) cha Kanisa, kwa habari ya imani, mapendo na umoja kamili na Kristo, kama alivyowahi kufundisha Mt. Ambrosi[189]. Kwa maana katika fumbo la Kanisa ambalo pia laitwa kwa haki mama na bikira, Bikira Maria mwenye heri ametangulia kwa njia bora na ya pekee kutoa mfano wa kuwa bikira na kuwa mama[190]. Katika kuamini na kutii kwake alimzaa duniani Mwana mwenyewe wa Baba, asimjue mtu, akitiwa kivuli na Roho Mtakatifu, akiwa kama Hawa mpya asiyemwamini nyoka wa zamani, bali amwaminiye mjumbe wa Mungu kwa imani isiyochafuliwa na shaka lolote. Akamzaa Mwana ambaye Mungu alimweka [awe] mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi (taz. Rum 8:29), yaani waamini, ambao Maria anashiriki kwa upendo wa kimama katika kuzaliwa kwao na kulelewa kwao.

Kanisa bikira na mama

64. Hata Kanisa, kwa kuutazama utakatifu wenye siri wa Maria, na kuyaiga mapendo yake na kuyatimiza kiaminifu mapenzi ya Baba, kwa kulipokea Neno la Mungu kwa uaminifu, linakuwa pia mama; kwani kwa mahubiri na ubatizo linazaa watoto waliotungwa kwa [uwezo wa] Roho Mtakatifu na kuzaliwa kwa Mungu, kwa uzima mpya usiokufa. Nalo pia ni Bikira anayehifadhi kwa ukamilifu na usafi wa moyo ile imani aliyomwahidia Bwanaarusi wake, na kwa kumwiga Mama wa Bwana wake, kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, hutunza kibikira (virginaliter) imani kamili, tumaini thabiti na mapendo manyofu[191].

Kanisa linapaswa kuuiga utakatifu wa Maria

65. Kanisa limekwisha kuufikia, ndani ya nafsi ya Bikira mwenye heri sana ukamilifu unaoliweka kuwa bila waa wala kunyanzi (taz. Efe 5:27); ila waamini wa Kristo wanajibidisha bado kukua katika utakatifu wakishinda dhambi. Kwa sababu hiyo wayainua macho yao kwa Maria anayeng’aa mbele ya jumuiya ya wateule kama mfano wa fadhila. Kanisa likimfikiria yeye kwa utauwa na kumtazama katika mwanga wa Neno aliyefanyika mwili, hupenya kwa heshima na kwa undani zaidi fumbo kuu la umwilisho, na kupata kufanana zaidi na zaidi na Bwanaarusi wake. Maana Maria, aliyeingia kabisa ndani ya historia ya wokovu, anaunganisha ndani yake kwa namna fulani maazimio (placita) makuu ya imani na kuyaakisi kama kioo; hivyo, anapohubiriwa na kuheshimiwa, huwavuta waamini kwa Mwanawe, kwa sadaka yake na kwa upendo wa Baba. Nalo Kanisa, likiufuatia utukufu wa Kristo, lapata kufanana zaidi na zaidi na kielezo (typus) chake kitukufu, na kuendelea bila kukoma katika imani, matumaini na mapendo, likitafuta na kuyashika mapenzi ya Mungu katika yote. Kwa hiyo Kanisa, pia katika kazi yake ya kitume, linamtazama kwa haki yeye aliyemzaa Kristo ambaye alichukuliwa mimba kwa Roho Mtakatifu na kuzaliwa na Bikira, kusudi [halafu] azaliwe na kukua katika mioyo ya waamini kwa njia ya Kanisa. Bikira huyo alikuwa katika maisha yake kielezo cha ule upendo wa kimama ambao wapaswa kuwa nao rohoni wale wote wanaoshiriki katika kazi ya utume ya Kanisa ili watu wazaliwe upya.

IV. IBADA KWA BIKIRA MARIA KATIKA KANISA

Tabia na msingi wa ibada

66. Maria alitukuzwa kwa neema ya Mungu, baada ya Mwanawe, kupita malaika wote na wanadamu wote, kwa maana yeye ni Mama mtakatifu sana wa Mungu aliyeshiriki mafumbo ya Kristo. [Kwa sababu hiyo Bikira Maria] anaheshimiwa kwa haki na Kanisa kwa ibada ya pekee. Kwa kweli, tangu nyakati za kale zaidi, Bikira Mwenye heri anaheshimiwa kwa cheo cha “Deipara” [yaani “Mama wa Mungu”], nao waamini wanaukimbilia ulinzi wake, wakimwomba katika hatari zao zote na mahitaji yao[192]. Hasa tokea Mtaguso wa Efeso ibada ya taifa la Mungu kwa Maria imekua kwa njia ya ajabu katika kumheshimu na kumpenda, katika kumwomba na kumwiga, kadiri ya maneno yake mwenyewe yenye utabiri, “Vizazi vyote wataniita mbarikiwa, kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu” (Lk 1:48-49). Ibada hiyo, kama ilivyokuwa daima katika Kanisa, ingawa ni ya pekee kabisa, ni tofauti kimsingi na ibada ya kuabudu inayotolewa kwa Neno aliyejifanya mwili, pia kwa Baba na kwa Roho Mtakatifu; na ibada [kwa Maria] pia inaikuza [ibada ile ya kuabudu]. Aina mbalimbali za heshima kwa Mama wa Mungu ambazo Kanisa amezikubali kufuatana na mafundisho yenye uzima na halisi, kadiri ya mazingira ya nyakati na mahali, kadiri ya tabia na hali za waamini, zaleta kwamba, Mama anapoheshimiwa, Mwana hupata kujulishwa, kupendwa na kutukuzwa inavyostahili, na amri zake kushikwa, kwa kuwa katika Yeye vitu vyote viliumbwa (taz. Kol 1:15-16) na “katika yeye ilimpendeza Baba wa milele utimilifu wote ukae” (Kol 1:19).

Kanuni za kichungaji

67. Mtaguso Mtakatifu unatoa mafundisho hayo ya kikatoliki baada ya kufikiri sana, na wakati huohuo unawaonya wana wote wa Kanisa wahamasishe kwa moyo mkuu ibada kwa Bikira Mwenye heri, hasa ile ya kiliturujia. Wathamini sana desturi na mazoezi ya ibada kwake, vilivyopendekezwa na Majisterio [ya Kanisa] katika mfululizo wa karne, na washike kwa makini yale yaliyoamriwa zamani juu ya kuziheshimu sanamu (de cultu imaginum) za Kristo, za Bikira Maria na za watakatifu[193]. Tena unawaonya sana wanateolojia na wahubiri wa Neno la Mungu waepukane kwa makini na kila chuku ya uongo (falsa superlatione), pia na choyo ya akili (a nimia mentis angustia) katika kuheshimu hadhi ya pekee ya Mama wa Mungu[194]. Kwa kusoma Maandiko Matakatifu, vitabu vya Mababa na vya Walimu Watakatifu, na kuchunguza Liturujia za Kanisa chini ya uongozi wa Majisterio, waeleze sawa majukumu na majaliwa ya Bikira Mwenye heri, ambayo kikomo chake daima ni Kristo, ambaye ni asili ya ukweli wote, utakatifu wote na utauwa wote. Wajihadhari sana wasije wakawakosesha kwa maneno na kwa matendo ndugu waliojitenga au watu wengine kuhusu mafundisho ya kweli ya Kanisa. Waamini, kwa upande wao, wakumbuke kwamba ibada ya kweli si kuwa na vionjo (affectu) vipitavyo tu visivyo na matunda, wala si wepesi wa kuamini bila ushuhuda, bali hutokana na imani ya kweli ambayo twaongozwa nayo kuutambua ubora wa Mama wa Mungu, na kuhimizwa kumpenda kimwana huyo Mama yetu na kuziiga fadhila zake.

V. MARIA NI ISHARA NA TUMAINI THABITI 

NA YA FARAJA KWA TAIFA LA MUNGU LISAFIRILO

Maria ni ishara ya taifa la Mungu

68. Mama wa Yesu, akiwa amekwisha tukuzwa mbinguni mwili na roho, ni sura na mwanzo wa Kanisa ambalo litapata utimilifu wake katika ulimwengu ujao. Kadhalika anang’aa duniani kama alama ya hakika ya matumaini na ya faraja kwa taifa la Mungu lililo safarini, mpaka siku ya Bwana itakapokuja (taz. 2Pet 3:10).

Maria auombee umoja wa wakristo

69. Mtaguso huu Mkuu unaona furaha kubwa na faraja kwa kuwa hata kati ya ndugu waliojitenga hawakosi kuwapo wanaomtolea Mama wa Bwana na Mwokozi heshima stahili, hasa kati ya wakristo wa Mashariki, wanaoshirikiana nasi katika kumheshimu Mama wa Mungu aliye Bikira daima, kwa bidii ya ari na moyo wa ibada[195]. Waamini wote wakristo wamsihi kwa nguvu Mama wa Mungu na Mama wa wanadamu, ili yeye aliyeusaidia mwanzo wa Kanisa kwa maombezi yake, pia sasa aliyetukuzwa mbinguni, juu ya Wenye heri na Malaika, awaombee kwa Mwanawe katika Ushirika wa Watakatifu wote, mpaka jamaa zote za mataifa zilizopambwa jina la Kristo au zisizomjua bado Mwokozi wao, zikusanyike kwa furaha kuwa Taifa moja la Mungu katika amani na mapatano, kwa utukufu wa Utatu Mtakatifu sana usiogawanyika.

 

Mambo yote yaliyoamuliwa katika konstitusio hii, na kila moja kati yao, yamewapendeza Mababa wa Mtaguso Mkuu. Nasi, kadiri ya mamlaka ya kitume tuliyopewa na Kristo, na pamoja na Mababa waheshimiwa, katika Roho Mtakatifu, tunayakubali, tunayaidhinisha na tunayathibitisha. Na yale yote yaliyoamuliwa kwa pamoja katika Sinodi hii, tunaamuru yawekwe kwa utukufu wa Mungu.

 

Roma, katika Kanisa la Mt. Petro, 21 Novemba 1964

 

Mimi mwenyewe, Paulo, Askofu wa Kanisa Katoliki

(zinafuata sahihi za Mababa)

 

    ______________

Kutoka maandishi ya Mtaguso Mkuu Vatikano II (Taarifa zilizotolewa na Katibu wa Mtaguso katika mkusanyo wa 123, tarehe 16 novemba 1964).

Limeulizwa swali kuhusu maana ya kiteolojia ya mafundisho yaliyotolewa katika kiwatiko (Schemate) juu ya Kanisa yenye kupigiwa kura ya maoni.

Kamati ya kimafundisho, kuhusu swali juu ya utathmini wa Hoja za marekebisho (Modis) zihusuzo Sura ya Tatu ya kiwatiko juu ya Kanisa, imetoa jibu hili lifuatalo:

“Kama ilivyo dhahiri kwa yenyewe, fasuli ya Mtaguso hutakiwa kufasiriwa kulingana na kanuni za kawaida, zinazojulikana kwa wote.

Wakati huohuo kamati ya kimafundisho hurejesha kwenye Tamko lake la tarehe 6 machi 1964, ambalo tunalinukulu hapa chini:

“Kulingana na desturi za Mitaguso na pia na malengo ya kichungaji ya Mtaguso huu wa sasa, Sinodi hii takatifu huagiza kwamba ni yenye nguvu ya faradhi yale tu ambayo, katika nyanja za dini na desturi, au maadili, yenyewe itatamka wazi kuwa na tabia hiyo.

Mambo mengine ambayo Sinodi takatifu inapendekeza na kufundisha, kama mafundisho ya Majisterio kuu ya Kanisa, waamini, wote na kila mmoja, watakiwa kuyapokea na kuyashika kadiri ya nia ya Sinodi takatifu yenyewe, nia ambayo inadhihirishwa katika mada yenyewe inayoongeleka na maneno yenyewe yanayoielezea, kufuatana na kanuni za ufafanuzi wa kiteolojia”.

Kwa agizo la Mamlaka kuu yanatolewa kwa Mababa maelezo mafupi ya utangulizi wa Hoja za marekebisho juu ya Sura ya Tatu ya kiwatiko juu ya Kanisa. Kadiri ya nia na maneno ya maelezo hayo inabidi kufafanua na kuelewa mafundisho yaliyotolewa katika sura hiyo ya tatu.

  Maelezo mafupi ya utangulizi (Nota esplicativa praevia)

Kamati imeamua kutanguliza kabla ya kutazama Hoja za marekebisho, maangalizo haya ya jumla:

1) Neno “Urika” halieleweki kwa maana iliyo “ya kisheria finyufinyu”, kama kundi la walio sawa, ambao kabidhi mamlaka yao kwa mkuu wao, bali kundi la kudumu ambalo muundo wake na mamlaka yake vinatakiwa kukisiwa (deduci debet) kutoka kwa Ufunuo wa kimungu. Kwa hiyo katika jibu kwa Hoja namba 12 inasemwa wazi juu ya Thenashara kwamba Bwana aliwaweka “kama Urika au kundi la kudumu”. Taz. pia Hoja n. 53c. – Kwa sababu hiyohiyo, mintarafu Urika wa Maaskofu hutumika pia maneno kama “Daraja” (Ordo), au “Umoja” (Corpus). Ufanano kati ya Petro na Mitume wengine kwa upande mmoja, na Baba Mtakatifu na Maaskofu kwa upande mwingine, hauleti maana ya kurithishwa mamlaka ya pekee ya Mitume kwa waandamizi wao, wala – kama ilivyo dhahiri – “usawa” (aequalitatem) kati ya Kichwa na viungo vya Urika, ila tu uwiano (proportionalitatem) kati ya uhusiano wa kwanza (Petro - Mitume) na uhusiano mwingine (Baba Mtakatifu - Maaskofu). Kwa hiyo kamati imeamua kuandika katika n. 22 sio jinsi “ileile” (eadem ratione), bali “iliyo sawa” (pari). Taz. Hoja 57.

2) Mmoja anakuwa “mwanaurika” kwa njia ya kupewa uwakfu wa Daraja ya Uaskofu, na ya ushirika wa kihierarkia na Mkuu wa Urika na viungo vyake. Taz. n. 22 § 1, mwishoni.

Katika kuwekwa wakfu, Askofu hupewa ushirikiano halisi katika majukumu “matakatifu”, kama inavyoonekana kutokana na mapokeo, pia ya kiliturujia. Kwa kusudi limetumiwa neno “majukumu” (munerum), wala si “mamlaka” (potestatum), kwa sababu hili la mwisho lingetambulika pengine kama mamlaka “iliyo huru kutumiwa” (ad actum expedita). Lakini, ili kuwepo uhuru huo wa kutumia mamlaka, inatakiwa liwepo “agizo wazi la kisheria”, au la kikanisa (iuridica determinatio) kutoka kwa mamlaka ya kihierarkia. Na agizo hilo juu ya mamlaka laweza kuhusu ama idhini kwa ofisio maalum, ama kukabidhiwa kundi la waamini, nalo linatolewa kadiri ya “miongozo” iliyoidhinishwa na mamlaka ya juu kabisa. Kanuni hii ya nyongeza inadaiwa na hali halisi ya jambo lenyewe (ex natura rei), kwa vile yanaongelewa hapa majukumu ya kutekelezwa na “watendaji wengi wengi”, wanaoshirikiana katika ngazi ya kihierarkia, kwa mapenzi ya Kristo. Ni dhahiri kwamba “ushirika” huo “katika maisha” ya Kanisa umetekelezwa hapo awali kadiri ya mazingira ya nyakati, kabla ya kupangwa katika kanuni na sheria (in iure).

Ndiyo sababu imesemwa wazi kwamba inatakiwa ushirika “wa kihierarkia” na Kichwa cha Kanisa na viungo vyake. “Ushirika” ni neno lenye heshima sana katika Kanisa la zamani (na hata sasa, hasa huko Mashariki). Kwa neno hili halimaanishwi “upendo-hisia” wa juujuu, bali “utaratibu lenye mpangilio” (realitate organica), udaio muundo wa kisheria na vilevile hutendwa na mapendo.

Kwa hiyo, kamati – kwa makubaliano ya wanakamati karibu wote – imeamua iandikwe hivi: “Katika ushirika wa kihierarkia”. Taz. Hoja 40 na pia yale yaliyosemwa juu ya “utume wa kikanisa” (missione canonica), katika n. 24.

Hati za Mababa Watakatifu wa hivi karibuni mintarafu mamlaka ya kisheria ya Maaskofu zinapaswa kufasiriwa kwa kuendana na hilo agizo juu ya mamlaka linalotakiwa.

3) “Urika”, ambao haupo pasipo Kichwa, husemwa kuwa nao una “mamlaka kubwa sana na kamili” juu ya Kanisa lote. Na jambo hilo lazima likubalike, ili usiathiriwe utimilifu wa mamlaka ya Baba Mtakatifu. Maana, Urika daima na kwa maumbile yake, unahusisha pia Kichwa, au Mkuu, wake “ambaye katika Urika ana daima wadhifa wa Wakili wa Kristo na Mchungaji wa Kanisa lote”. Kwa maneno mengine: kumeainishwa kati ya Baba Mtakatifu akiwa peke yake, na Baba Mtakatifu akiwa pamoja na Maaskofu; sio baina ya Baba Mtakatifu peke yake, na Maaskofu wakiwa wao pamoja. Lakini, kwa vile Baba Mtakatifu wa Roma ni “Kichwa” (Caput) cha Urika, anao uwezo wa kutenda matendo (actus) ambayo hayamo katika mamlaka ya Maaskofu, k.v. kuitisha na kuongoza Urika, kuidhinisha kanuni za utendaji, n.k. Taz. Hoja 81. Ni juu ya uamuzi wa Baba Mtakatifu, ambaye amekabidhiwa uangalizi juu ya kundi lote la Kristo, kuelezea, kadiri ya mahitaji ya Kanisa yanayobadilika katika mlolongo wa karne, kanuni za kutekeleza uangalizi huo, ama kwa peke yake, ama kiurika. Baba Mtakatifu, katika kuamuru, kuhimiza, kuidhinisha utendaji wa kiurika, anafuata utambuzi wake (discretionem) akitazamia manufaa ya Kanisa.

4) Baba Mtakatifu, kama Mchungaji Mkuu wa Kanisa, anaweza kutumia mamlaka yake wakati wowote kwa hiari yake, kadiri inavyodaiwa na majukumu yake. Lakini Urika, ungawa daima upo, hata hivyo hautendi daima matendo ya kiurika “kwelikweli” (stricte), kama inavyoonekana katika Mapokeo ya Kanisa. Kwa maneno mengine: haupo daima “katika utendaji timilifu” (in acto pleno); na kwa kweli unatenda kiurika kwelikweli kwa nafasi tu, na “kwa kibali cha Kichwa” (consentiente Capite), inasemwa “kwa kibali cha Kichwa” ili isifikiriwe kuwa ni suala la “kumtegemea mgeni”; neno “kibali” linarejea kwenye maana ya “ushirika” uliopo kati ya Kichwa na viungo, na inamaanisha kuwa “tendo” ambalo kwa asili ni ya Kichwa lahitajika. Jambo hilo liko wazi katika n. 22, § 2, napo mwishoni linaelezwa. Usemi wa kukanusha “isipokuwa” (nonnisi) inaelekea ibara zote, kwa hiyo ni dhahiri kwamba “kanuni” zilizoidhinishwa na mamlaka ya juu zatakiwa kushikwa daima. Taz. Hoja 84.

Lakini inaonekana katika sehemu zote kwamba unaongelewa “muungano” (coniunctionem) wa Maaskofu na Kichwa chao, wala kamwe matendo ya Maaskofu bila ya Baba Mtakatifu. Ingalikuwa hivyo, kwa vile ingekosekana utendaji wa Kichwa, Maaskofu hawawezi kutenda kama Urika, kadiri inavyoeleweka kwa maana yenyewe ya “Urika”. Hakika ushirika huo wa kihierarkia wa Maaskofu wote na Baba Mtakatifu ni wa kawaida katika Mapokeo.

N.B. Bila ushirika wa kihierarkia majukumu ambayo yanaendana na sakramenti na maumbile (munus sacramentale-ontologicum), ambayo ni kitu kingine na maana ya kikanuni na kisheria (ab aspectu canonico-iuridico), “hayawezi” kutekelezwa. Kamati imeona vema kutokuingia katika masuala ya “uhalali” na “uthabiti” ambayo yameachwa kwa majadiliano ya wanateolojia, hasa kwa ambo yale yahusuyo mamlaka ambayo yakini inatumiwa na ndugu wa Mashariki waliojitenga, na ambayo kuna maelezo mbalimbali ya ufasiri wake.

+ Pericle Felici
Askofu Mkuu wa Samosata
Katibu mkuu wa Mtaguso

  

[1]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 64,4: PL 3, 1017; CSEL (Hartel), III B, uk. 720. – Mt. Hilarius Pict., In Mt. 23,6: PL 9, 1047. – Mt. Augustinus, passim. – Mt. Cyrillus Alex., Glaph. in Gen. 2,10: PG 69, 110A.
[2]Mt. Gregorius M., Hom. in Evang. 19,1: PL 76, 1154B. – Taz. Mt. Augustinus, Serm. 341,9,11: PL 39, 1499 s. – Mt. Ioannes Dam., Adv. Iconocl. 11: PG 96, 1357.
[3] Taz. Mt. Irenaeus, Adv. Haer.III,24,1: PG 7, 966B; Harvey 2,131; ed.Sagnard, Sources Chr., uk. 398
[4]Mt. Cyprianus, De Orat. Dom. 23: PL 4, 553; Hartel, III A, uk. 285. – Mt. Augustinus, Serm. 71,20,33: PL 38, 463 s. – Mt. Ioannes Dam., Adv. Iconocl. 12: PG 96, 1358D.
[5]Taz. Origenes, In Mt. 16,21: PG 13, 1443C. – Tertullianus, Adv. Marc. 3,7: PL 2, 357C; CSEL 47,3, uk. 386. – Kuhusu matini za kiliturujia, taz. Sacramentarium Gregorianum: PL 78, 160B; au C. Moehlberg, Liber Sacramentorum Romanae Ecclesiae, Romae 1960, uk. 111, XC: “Ee Mungu, ujijengaye makao ya milele kwa tangamano lote la watakatifu....”. Utenzi Urbs Ierusalem baeata katika Breviari ya kimonaki, na Coelestis urbs Ierusalem, katika Breviari ya Kiroma (Sala ya Kanisa).
[6]Taz. Mt. Thomas, Summa Theol.III, q.62, a.5, ad i.
[7]Taz. Pius XII, Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 208.
[8]Taz. Leo XIII, Enc. Divinum illud, 9 mei 1897: AAS 29 (1896-97) uk. 650. – Pius XII, Enc. Mystici Corporis, l.c., uk. 219-220; Denz. 2288 (3808). – Mt. Augustinus, Serm. 268,2: PL 38, 1232 na nyingine. – Mt. Ioannes Chrys., In Eph., Hom. 9, 3: PG 62, 72. – Didymus Alex., Trin. 2, 1: PG 39, 449 s. – Mt. Thomas, In Col. 1, 18, lect. 5: Ed. Marietti, II, n. 46: “Kama ulivyowekwa mwili mmoja kutoka kwa umoja wa roho ( animae), vivyo hivyo Kanisa kutoka kwa umoja wa Roho...”.
[9]Taz. Leo XIII, Enc. Sapientiae Christianae, 10 jenuari 1890: AAS 22 (1889-90) uk. 392. Id., Epist. Enc. Satis cognitum, 29 juni 1896: AAS 28 (1895-96) uk. 710 na 724 ss. – Pius XII, Enc. Mystici Corporis, l.c., uk. 199-200.
[10]Taz. Pius XII, Enc. Mystici Corporis, l.c., uk. 221 ss. Id., Enc. Humani generis, 12 agosti 1950: AAS 42 (1950) uk. 571.
[11]Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Satis cognitum, 29 juni 1896: AAS 28 (1895-96) uk. 713.
[12]Taz. Symbolum Ap.: Denz. 6-9 (10-30); Symb. Nic.Const.: Denz. 86 (150); coll. Prof. fidei Trid.: Denz. 994 na 999 (1862 na 1868).
[13] Laitwa “Kanisa la kiroma, takatifu (katoliki, la Mitume)”, katika Prof. fidei Trid., l.c. na katika Conc. Vat. I, Sess. III, Const. dogm. Dei Filius: Denz. 1782 (3001).
[14]Taz. Mt. Augustinus, De Civ.Dei XVIII, 51, 2: PL 41, 614.
[15]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 69,6: PL 3, 1142B; CSEL (Hartel), III B, uk. 754: “Sakramenti ya umoja isiyotengeka”.
[16] Taz. Pius XII, Alloc. Magnificate Dominum, 2 novemba 1954: AAS 46 (1954) uk. 669. Id., Litt. Enc. Mediator Dei, 20 novemba 1947: AAS 39 (1947) uk. 555.
[17] Taz. Pius XI, Litt. Enc. Miserentissimus Redemptor, 8 mei 1928: AAS 20 (1928) uk. 171 s. – Pius XII, Alloc. Vous nous avez, 22 septemba 1956: AAS 48 (1956) uk. 714.
[18]Taz. Mt. Thomas, Summa Theol. III, q.63, a.2.
[19]Taz. Mt. Cyrillus Hieros., Catech. 17, kuhusu Roho Mtakatifu, II, 35-37: PG 33, 1009-1012. – Nic.Cabasilas, De vita in Christo, lib. III, kuhusu manufaa ya Krisma (Mpako mtakatifu, au kipaimara): PG 150, 569-580. – Mt. Thomas, Summa Theol. III, q.65, a.3 na q.72, a.1 na 5.
[20]Taz. Pius XII, Litt. Enc. Mediator Dei, 20 novemba 1947: AAS 39 (1947) hasa uk. 552 s.
[21]Taz. 1Kor 7:7: “Kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi”. – Mt. Augustinus, De Dono Persev. 14, 37: PL 45, 1015s.: “Ni kipaji cha Mungu si kutawala tamaa tu, bali pia usafi wa moyo wa watu wa ndoa”.
[22]Taz. Mt. Augustinus, De Praed.Sanct.14, 27: PL 44, 980.
[23]Taz. Mt. Ioannes Chrys., In Io., Hom. 65, 1: PG 59, 361.
[24]Taz. Mt. Irenaeus, Adv.Haer.III,16,6; III,22,1-3: PG 7, 925C-926A na 955C-958A; Harvey 2,87 s. na 120-123; ed. Sagnard, Sources Chr., uk. 290-92 na 372 ss.
[25]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Rom., Praef.: ed. Funk, I, uk. 252.
[26]Taz. Mt. Augustinus, Bapt. c. Donat., V,28, 39: PL 43, 197: “Hakika ni dhahiri kwamba liitwalo katika Kanisa ndani na nje, lazima lifikiriwe moyoni, wala si mwilini”. – Id., ib.III,19,26: col. 152; V,18,24: col. 189; In Io., Tr. 61,2: PL 35, 1800, na mara nyingi mahali pengine.
[27] Lk 12:48: “Kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi”. Taz. Mt 5:19-20; 7:21-22; 25:41-46; Yak 2:14.
[28] Taz. Leo XIII, Epist. Apost. Praeclare gratulationis, 20 juni 1894: AAS 26 (1893-94) uk. 707.
[29]Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Satis cognitum, 29 juni 1896: AAS 28 (1895-96) uk. 738. – Id. Epist. Enc. Caritatis studium, 25 julai 1898: AAS 31 (1898-99) uk. 11. – Pius XII, Nuntius radioph. Nell’alba, 24 desemba 1941: AAS 34 (1942) uk.21.
[30]Taz. Pius XI, Litt. Enc. Rerum Orientalium, 8 septemba 1928: AAS 20 (1928) uk. 287. – Pius XII, Litt. Enc. Orientalis Ecclesiae, 9 aprili 1944: AAS 36 (1944) uk. 137.
[31]Taz. Instr. S.S.C.S. Officii, 20 desemba 1949: AAS 42 (1950) uk. 142.
[32]Taz. Mt. Thomas, Summa Theol.III, q.8, a.3, ad l.
[33] Taz. Epist. S.S.C.S. Officii kwa Askofu Mkuu wa Boston: Denz. 3869-72.
[34] Taz. Eusebius Caes., Praeparatio Evangelica. 1,1: PG 21, 28AB.
[35]Taz. Benedictus XV, Epist. Apost. Maximum illud, 30 novemba 1919: AAS 11 (1919) uk. 440, hasa 451 ss. – Pius XI, Litt. Enc. Rerum Ecclesiae, 28 februari 1926: AAS 18 (1926) uk. 68-69. – Pius XII, Litt. Enc. Fidei Donum, 21 aprile 1957: AAS 49 (1957) uk. 236-237.
[36] Taz. Didachè, 14: ed. Funk, I, uk. 32 – Mt. Iustinus, Dial 41: PG 6, 564. – Mt. Irenaeus, Adv. Haer.IV,17,5: PG 7, 1023; Harvey 2,199 s. – Conc. Trid., Sess. 22, cap. 1: Denz. 939 (1742).
[37]Taz. Conc. Vat.I, Const. dogm.De Ecclesia Christi, Pastor aeternus: Denz. 1821 (3050 s.).
[38] Taz. Conc. Flor., Decretum pro Graecis: Denz. 694 (1307) na Conc. Vat. I, ib.: Denz. 1826 (3059).
[39] Taz. Liber sacramentorum Mt. Gregorii, Praef. in natali Mt. Matthiae et Mt. Thomae: PL 78, 51 na 152; taz. Cod. Vat. lat. 3548, f.18 – Mt. Hilarius Pict., In Ps. 67,10: PL 9, 450; CSEL 22, uk.286. – Mt. Hieronymus, Adv. Iovin. 1,26: PL 23, 247A.-S. – Mt. Augustinus, In Ps. 86,4: PL 37, 1103. – Mt. Gregorius M., Mor. in Iob XXVIII,V: PL 76, 455-456. – Primatius, Comm. in Apoc. V: PL 66, 924BC. – Paschasius Radb., In Mt. L.8, cap.16: PL 120, 561C. – Taz.Leo XIII, Epist. Et sane, 17 desemba 1888: AAS 21 (1888) uk. 321.
[40]Taz. Mdo 6:2-6; 11:30; 13:1; 14:23; 20:17; 1The 5:12-13; Flp 1:1; Kol 4:11 na sehemu nyingine.
[41]Taz. Mdo 20:25-27; 2Tim 4:6s. pamoja na 1Tim 5:22; 2Tim 2:2; Tit 1:5; Mt. Clem. Rom., Ad Cor. 44,3: Ed. Funk, I, uk. 156.
[42]Taz. Mt. Clem. Rom., Ad Cor. 44,2: Ed. Funk, I, uk. 154 s.
[43]Taz. Tertullianus, Praescr. Haer. 32: PL 2, 52 s. – Mt. Ignatius M., sehemu mbalimbali.
[44]Taz. Tertullianus, Praescr. Haer. 32: PL 2, 53.
[45]Taz. Mt. Irenaeus, Adv. Haer. III,3,1: PG 7, 848A; Harvey 2,8; ed. Sagnard, Sources Chr., uk. 100 s.: “manifestatam” (= hudhihirishwa).
[46]Taz. Mt. Irenaeus, Adv. Haer. III,2,2: PG 7, 847; Harvey 2,7; ed. Sagnard, Sources Chr., uk. 100: “custoditur” (= hutunzwa), taz. hiyohiyo IV,26,2; coll. 1053; Harvey 2,236, na IV,33,8 coll. 1077; Harvey 2,262.
[47]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Philad., Praef.: ed. Funk, I, uk. 264.
[48]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Philad. 1,1; Ad Magn. 6,1: ed. Funk, I, uk. 264 na 234.
[49] Taz. Mt. Clem. Rom., l.c. 42,3-4; 44,3-4; 57,1-2: Ed. Funk, I, uk. 152, 156, 171 s. – Mt. Ignatius M., Ad Philad. 2; Ad Smyrn. 8; Ad Magn. 3; Ad Trall. 7: ed. Funk, I, uk. 265 s.; 282; 232; 246 s. n.k. – Mt. Iustinus, Apol., 1,65: PG 6, 428. – Mt. Cyprianus, Epist., sehemu mbalimbali.
[50] Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Satis cognitum, 29 juni 1896: AAS 28 (1895-96) uk. 732.
[51]Taz. Conc. Trid., Decr. De sacr. Ordinis, cap. 4: Denz. 960 (1768); Conc. Vat.I, Const. dogm.De Ecclesia Christi, Pastor aeternus, cap. 3: Denz. 1828 (3061). Pius XII, Litt. Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 209 na 212. CIC, can. 329 §1.
[52]Taz. Leo XIII, Epist. Et sane, 17 desemba 1888: AAS 21 (1888) uk. 321 s.
[53]Taz. Mt. Leo M., Serm. 5,3: PL 54, 154.
[54]Taz. Conc. Trid., Sess. 23, cap. 3. hutaja maneno ya 2Tim 1:6-7, ili kuonyesha kuwa Daraja takatifu ndiyo sakramenti ya kweli: Denz. 959 (1766).
[55]Katika Trad. Apost. 3: ed. Botte, Source Chret., uk. 27-30, Askofu hupewa “primatus sacerdotii = ukuu wa ukuhani”. Taz. Sacramentarium Leonianum, ed. C. Moehlberg, Sacramentarium Veronense, Romae, 1955, uk. 119: “hadi huduma ya ukuhani mkuu... kamilisha ndani ya makuhani wako fumbo lako”; vilevile Liber Sacramentorum Romanae Ecclesiae, Romae, 1960, uk. 121-122: “Uwape, Ee Bwana, kiti cha Uaskofu, walichunge Kanisa lako na watu wote”.Taz. PL 78, 224.
[56] Taz. Trad. Apost. 2: ed. Botte, uk. 27.
[57] Taz. Conc. Trid., Sess. 23, cap. 4, hufundisha kwamba Daraja takatifu hutia alama isiyofutika ( characterem): Denz. 960 (1767). Taz. Ioannes XXIII, Alloc. Iubilate Deo, 8 mei 1960: AAS 52 (1960) uk. 466.Paulus VI, Homilia in Bas. Vaticana, 20 oktoba 1963: AAS 55 (1963), uk. 1014.
[58]Mt. Cyprianus, Epist. 63,14: PL 4, 386; Hartel, III B, uk. 713: “Kuhani hutenda kweli mahali pa Kristo”. – Mt. Ioannes Chrys., In 2 Tim., Hom. 2, 4: PG 62, 612: Kuhani ndiye “sumbolon” ya Kristo. – Mt. Ambrosius, In Ps. 38,25-26: PL 14, 1051-52: CSEL 64,203-204. – Ambrosiaster, In 1 Tim. 5,19: PL 17, 479C na In Eph. 4,11-12: col. 387C. – Theodorus Mops., Hom. Katech. XV,21 na 24: ed. Tonneau, uk. 497 na 503. – Hesychius Hieros., In Lev. L. 2,9,23: PG 93, 894B.
[59]Taz. Eusebius Caes., Hist.Eccl., V,24,10: GCS II,1, uk. 495; ed. Bardy, Sources Chret. II, uk. 69. – Dionysius, kufuata Eusebius Caes., ib. VII,5,2: GCS II,2, uk. 638 s.; ed. Bardy, Sources Chret. II, uk. 168 s.
[60]Taz. kuhusu Mitaguso ya zamani, Eusebius Caes., Hist.Eccl., V,23-24: GCS II,1, uk. 488 ss.; ed. Bardy, Sources Chret. II, uk. 66 ss. na sehemu nyingine. Conc. Nicaenum, can. 5: COD uk. 7.
[61]Taz. Tertullianus, De Ieiunio, 13: PL 2, 972B; CSEL 20, uk. 292, lin. 13-16.
[62]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 56,3: Hartel, III B, uk. 650; Bayard, uk. 154.
[63]Taz. Relatio officialis Zinelli, katika Conc. Vat.I: Mansi 52, 1109C.
[64]Taz. Conc. Vat.I, Schema Const. Dogm. II, de Ecclesia Christi, c. 4: Mansi 53, 310. Taz. Relatio Kleutgen kuhusu Schemate reformato: Mansi 53, 321B-322B na declaratio Zinelli: Mansi 52, 1110A. Taz. pia Mt. Leo M., Serm. 4,3: PL 54, 151A.
[65]Taz. CIC, can. 222 na 227.
[66]Taz. Conc. Vat.I, Const. dogm.De Ecclesia Christi, Pastor aeternus: Denz. 1821 (3050 s.).
[67]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 66,8: Hartel, III,2, uk. 733: “Askofu katika Kanisa, na Kanisa katika Askofu”.
[68]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 55,24: Hartel, uk. 642, lin. 13: “Kanisa lililo moja hugawanyika katika viungo vingi ulimwenguni mwote”. Epist. 36,4: Hartel, uk. 575, lin. 20-21.
[69]Taz. Pius XII, Litt. Enc. Fidei Donum, 21 aprile 1957: AAS 49 (1957) uk. 237.
[70]Taz. Mt. Hilarius Pict., In Ps. 14,3: PL 9, 206; CSEL 22, uk.86. – Mt. Gregorius M., Moral. IV,7,12: PL 75, 643C. – Ps. Basilius, In Is. 15,296: PG 30, 637C.
[71]Taz. Mt. Coelestinus, Epist. 18,1-2, ad Conc. Eph.: PL 50, 505AB; Schwartz, Acta Conc. Oec. I,1,1, uk.22. Taz. Benedictus XV, Epist. Apost. Maximum illud, 30 novemba 1919: AAS 11 (1919) uk. 440. – Pius XI, Litt. Enc. Rerum Ecclesiae, 28 februari 1926: AAS 18 (1926) uk. 69. – Pius XII, Litt. Enc. Fidei Donum, l.c.
[72] Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Grande munus, 30 septemba 1880: AAS 13 (1880) uk. 145. Taz. CIC, c. 1327; c. 1350 §2.
[73]Kuhusu haki za Upatriarka, taz. Conc. Nicaenum, can. 6 kwa habari ya Alexandria na Antiochia, na can. 7 kwa habari ya Hierosolymis: COD, uk. 8. – Conc.Later. IV, mwaka 1215, Constit.V: De dignitate Patriarcharum: COD, uk. 212. – Conc.Ferr.-Flor.: COD, uk. 504.
[74]Taz. Cod. Iuris Can. pro Eccl. Orient., c. 216-314: kuhusu Mapatriarka; c. 324-339: kuhusu Maaskofu wakuu; c. 362-391: kuhusu wenye madaraka wengine; hasa c. 238 §3; 216; 240; 251; 255: kuhusu Mapatriarka kuwateua Maaskofu.*Tunaona vema kueleza hivi dondoo hili: Taz. Pius XII, Motu proprio Cleri sanctitati, 2 juni 1957: AAS 49 (1957) uk. 497-527 (cc. 216-314: kuhusu Mapatriarka), uk. 530-534 (cc. 324-339: kuhusu Maaskofu wakuu), uk. 540-547 (cc. 362-391: kuhusu wenye madaraka wengine); hasa uk. 497-510 (cc. 238 §3; 216; 240; 251; 255: kuhusu Mapatriarka kuwateua Maaskofu). ( N.d.R.)
[75]Taz. Conc. Trid., Decr. de reform., Sess. V, c. 2, n. 9 na Sess. XXIV, can. 4; COD, uk 645 na 739).
[76]Taz. Conc. Vat.I, Const. dogm. Dei Filius, 3: Denz. 1792 (3011). Taz. maelezo yaliyomo katika kiwatiko (=“Schema”) (yaliyochukuliwa kutoka kwa Mt. Roberto Bellarmino): Mansi 51, 579C; na pia kiwatiko kilichosahishwa Const. II De Ecclesia Christi, pamoja na maelezo yake Kleutgen: Mansi 53, 313AB. – Pius IX, Epist. Tuas libenter: Denz. 1683 (2879).
[77]Taz. CIC, c. 1322-1323.
[78]Taz. Conc. Vat. I, Const. dogm., Pastor aeternus: Denz. 1839 (3074).
[79]Taz. ufafanuzi wa Gasser katika Conc. Vat.I: Mansi 52, 1213AC.
[80]Taz. Gasser, ib.: Mansi 1214A.
[81]Taz. Gasser, ib.: Mansi 1215CD, 1216-1217A.
[82]Taz. Gasser, ib.: Mansi 1213.
[83]Taz. Conc. Vat. I, Const. dogm., Pastor aeternus, 4: Denz. 1836 (3070).
[84]Sala ya kuweka wakfu Askofu katika riti ya kigriki: Euchologion to mega, Romae, 1873, uk. 139.
[85]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Smyrn.8,1: ed. Funk, I, uk. 282.
[86] Taz. Mdo 8:1; 14:22-23; 20:17 na sehemu nyingine.
[87] Sala ya kimozarabi: PL 96, 759B.
[88]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Smyrn.8,1: ed. Funk, I, uk. 282.
[89]Mt. Thomas, Summa Theol. III, q.73, a.3.
[90]Taz. Mt. Augustinus, C. Faustum, 12,20: PL 42, 265; Serm. 57,7: PL 38,89, n.k.
[91]Mt. Leo M., Serm. 63,7: PL 54, 357C.
[92] Taz. Trad. Apost. Hippolyti, 2-3: ed. Botte, uk. 26-30.
[93] Taz. fasulu ya uchunguzi mwanzoni mwa kumweka wakfu Askofu, na sala mwishoni mwa Misa hiyo ya kumweka wakfu, baada ya Ta Deum.
[94]Benedictus XIV, Br. Romana Ecclesia, 5 oktoba 1752, §1: Bullarium Benedicti XIV, t. IV, Romae, 1758, 21: “Askofu ni mfano wa Kristo, hutekeleza jukumu lake”. – Pius XII, Enc. Mystici Corporis, l.c.; uk. 211: “Wanalisha na kuchunga kwa jina la Kristo makundi waliyokabidhiwa, kila mmoja kundi lake”.
[95] Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Satis cognitum, 29 juni 1896: AAS 28 (1895-96) uk. 732. Idem, Epist. Officio sanctissimo, 22 desemba 1887: AAS 20 (1887) uk. 264. – Pius IX, Litt. Apost. ad Episcopos Germaniae, 12 machi 1875, na Alloc. Consist. 15 machi 1875: Denz. 3112-3117, katika toleo jipya tu.
[96]Taz. Conc. Vat. I, Const. dogm., Pastor aeternus, 3: Denz. 1828 (3061). Taz. Relatio Zinelli: Mansi 52, 1114D.
[97]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Ephes.5,1: ed. Funk, I, uk. 216.
[98]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Ephes.6,1: ed. Funk, I, uk. 218.
[99]Taz. Conc. Trid., Decr. De sacr. Ordinis, cap. 2: Denz. 958 (1765), na can. 6: Denz. 966 (1776).
[100]Taz. Innocentius I, Epist. ad Decentium: PL 20, 554A; Mansi 3, 1029; Denz. 98 (215): “Mapadre, ingawa ni makuhani wa Daraja ya pili, lakini hawana kilele cha ukuhani”. – Mt. Cyprianus, Epist. 61,3: ed. Hartel, uk. 696.
[101]Taz. Conc. Trid., l.c.: Denz. 956a-968 (1763-1778), na hasa can. 7: Denz. 967 (1777). – Pius XII, Const. Apost. Sacramentum Ordinis: Denz. 2301 (3857-61).
[102]Taz. Innocentius I, l.c. – Mt. Gregorius Naz., Apol. II,22: PG 35, 432B. – Ps.Dionysius, Eccl. Hier., 1,2: PG 3, 372D.
[103]Taz. Conc. Trid., Sess. 22: Denz. 940 (1743). – Pius XII, Litt. Enc. Mediator Dei, 20 novemba 1947: AAS 39 (1947) uk. 553: Denz. 2300 (3850).
[104]Taz. Conc. Trid., Sess. 22: Denz. 938 (1739-40). – Conc. Vat. II, Const. de Sacra Liturgia, Sacrosanctum Concilium, n.7 na n.47: AAS 56 (1964) uk. 100-113.
[105]Taz. Pius XII, Litt. Enc. Mediator Dei, l.c., kwenye dondoo n. 103.
[106]Taz. Mt. Cyprianus, Epist. 11,3: PL 4, 242B; Hartel, II, 2, uk. 497.
[107]Taz. Pontificale romanum, katika kuweka wakfu Mapadre, wakati wa kuvalisha mavazi ya ibada.
[108]Taz. Pontificale romanum, katika kuweka wakfu Mapadre; utangulizi.
[109]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Philad., 4: ed. Funk, I, uk. 266. – Mt. Cornelius I, kufuata Mt. Cyprianus, Epist. 48,2; Hartel, III, 2, uk. 610.
[110] Constitutiones Ecclesiae aegyptiacae, III,2: ed. Funk, Didascalia, II, uk. 103 . Statuta Eccl. Ant. 37-41: Mansi 3, 954.
[111] Taz. Mt. Polycarpus, Ad Phil., 5,2: ed. Funk, I, uk. 300: Kristo aitwa “aliyejifanya mtumishi wa wote”. – Taz. Didachè, 15,1: ed. Funk, I, uk. 32. – Mt. Ignatius M., Ad Trall. 2,3: ed. Funk, I, uk. 242. – Constitutiones Apostolorum, 8,28,4: ed. Funk, Didascalia, I, uk. 530 .
[112]Taz. Mt. Augustinus, Serm. 340,1: PL 38, 1483.
[113]Taz. Pius XI, Litt. Enc. Quadragesimo anno, 15 mei 1931: AAS 23 (1931) uk. 221 s. – Pius XII, Alloc. De quelle consolation, 14 oktoba 1951: AAS 43 (1951) uk. 790 s.
[114] Taz. Pius XII, Alloc. Six ans se sont écouléss, 5 oktoba 1957: AAS 49 (1957) uk. 927.
[115] Missale romanum, kutoka Utangulizi wa Sherehe ya Yesu Kristo Mfalme.
[116] Taz. Leo XIII, Epist. Enc. Immortale Dei, 1 novemba 1885: AAS 18 (1885) uk. 166 ss. – Id. Litt. Encicl. Sapientiae christianae, 10 jenuari 1890: AAS 22 (1889-90) uk. 397 ss. – Pius XII, Alloc. Alla vostra filiale, 23 machi 1958: AAS 50 (1958) uk. 220: “Hali ya ulei safi na wa halali ya serikali”.
[117]Taz. CIC, can. 682.
[118] Taz. Pius XII, Alloc. De quelle consolation, l.c., uk. 789: “Katika mapigano mkataa katika vita, mara nyingi juhudi zenye mafanikio zatoka kwa upande wa mbele wa jeshi...”. Id., Alloc. L’importance de la presse catholique, 17 februari 1950: AAS 42 (1950) uk. 256.
[119]Taz. 1The 5:19 na 1Yoh 4:1.
[120] Epist. Ad Diognetum, 6: ed. Funk, I, uk. 400 – Taz. Mt. Ioannes Chrys., In Mt., Hom. 46(47), 2: PG 58, 478, kwa mfano wa chachu katika donge.
[121] Missale romanum, Gloria in excelsis. Taz. Lk 1:35; Mk 1:24; Lk 4:34; Yn 6:69 (Ð §gioj toà Qeoà); Mdo 3:14; 4:27 na 30; Ebr 7:26; 1Yoh 2:20; Ufu 3:7.
[122] Taz. Origenes, Comm. Rom. 7,7: PG 14, 1122B. – Ps. Macarius, De Oratione 11: PL 34, 861AB. – Mt. Thomas, Summa Theol. II-II, q.184, a.3.
[123]Taz. Mt. Augustinus, Retract. II, 18: PL 32, 637 s. – Pius XII, Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 225.
[124]Taz. Pius XI, Litt. Enc. Rerum omnium, 26 jenuari 1923: AAS 15 (1923) uk. 50 na 59-60. – Id., Litt. Enc. Casti Connubii, 31 desemba 1930: AAS 22 (1930) uk. 548. – Pius XII, Const. Apost. Provida Mater, 2 februari 1947: AAS 39 (1947) uk. 117. – Id., Alloc. Annus sacer, 8 desemba 1950: AAS 43 (1951) uk. 27-28. – Id., Alloc. Nel darvi, 1 julai 1956: AAS 48 (1956) uk. 574 s.
[125]Taz. Mt. Thomas, Summa Theol. II-II, q.184, a.5 na 6. – Id., Perf. vitae spir. c. 18. – Origenes, In Is. Hom. 6,1: PG 13, 239.
[126] Taz. Mt. Ignatius M., Ad Magn. 13,1: ed. Funk, I, uk. 241.
[127]Taz. Mt. Pius X, Exort. Haerent animo, 4 agosti 1908: ASS 41 (1908) uk 560 s.. – CIC can. 124. – Pius XI, Litt. Enc. Ad catholici sacerdotii, 20 desemba 1935: AAS 28 (1936) uk. 22.
[128]Taz. Pontificale romanum, katika kuweka wakfu Mapadre; katika mawaidha ya mwanzoni.
[129]Taz. Mt. Ignatius M., Ad Trall. 2,3: ed. Funk, I, uk. 244.
[130] Taz. Pius XII, Alloc. Sous la maternelle protection, 9 desemba 1957: AAS 50 (1958) uk. 36.
[131]Taz. Pius XI, Litt. Enc. Casti Connubii, 31 desemba 1930: AAS 22 (1930) uk. 548 s. – Mt. Ioannes Chrys., In Eph., Hom. 20, 2: PG 62, 136 ss.
[132]Taz. Mt. Augustinus, Enchir. 121, 32: PL 40, 288. – Mt. Thomas, Summa Theol. II-II, q.184, a.1. – Pius XII, Adhort. Apost. Menti nostrae, 23 septemba 1950: AAS 42 (1950) uk. 660.
[133]Kuhusu mashauri kwa ujumla, taz.Origenes, Comm. Rom. X,14: PG 14, 1275B. – Mt. Augustinus, De S. Virginitate, . 15, 15: PL 40, 403. – Mt. Thomas, Summa Theol.I-II, q.100, a.2C (mwishoni); II-II, q.44, a.4, ad 3.
[134] Kuhusu ubora wa ubikira mtakatifu, taz. Tertullianus, Exhort. Cast. 10: PL 2, 925C. – Mt. Cyprianus, Hab. Virg. 3 na 22: PL 4, 443B na 461A s..– Mt. Athanasius (?), De Virg.: PG 28, 252 ss. – Mt. Io. Chrys., De Virg.: PG 48, 533 ss.
[135]Kuhusu umaskini wa kiroho, taz. Mt 5:3 na 19:21; Mk 10:21; Lk 18:22; kuhusu utii, hutolewa mfano wa Kristo: Yn 4:34 na 6:38; Flp 2:8-10¸Ebr 10:5-7. Maandishi ya Mababa na ya waanzilishi wa mashirika yapo mengi.
[136]Kuhusu kutekeleza mashauri ya kiinjili kusikowalazimisha watu wote, taz. Mt. Ioannes Chrys., In Mt., Hom. 7(7), 2: PG 57, 81 s. – Mt. Ambrosius, De Viduis, 4,23: PL 16, 241 s.
[137]Taz. Rosweydus, Vitae Patrum, Antwerpias, 1628. – Apophtegmata Patrum: PG 65. – Palladius, Historia Lausiaca: PG 34, 995ss.: ed.C. Butler, Cambridge, 1898 (1904). – Pius XI, Const. Apost. Umbratilem, 8 julai 1924: AAS 16 (1924) uk. 386-387. – Pius XII, Alloc. Nous sommes heusereux, 11 aprili 1958: AAS 50 (1958) uk. 283.
[138] Taz. Paulus VI, Alloc. Magno gaudio, 23 mei 1964: AAS 56 (1964) uk. 566.
[139] Taz. CIC, c. 487 na 488, 4 °. – Pius XII, Alloc. Annus sacer, 8 desemba 1950: AAS 43 (1951) uk. 27 s. – Id., Const. Apost. Provida Mater, 2 februari 1947: AAS 39 (1947) uk. 120 ss.
[140] Taz. Paulus VI, l.c., uk. 567.
[141]Taz. Mt. Thomas, Summa Theol.II-II, q.184, a.3 na q.188, a.2. – Mt. Bonaventura, Opusc . XI, Apologia Pauperum, c. 3,3: ed. Opera, Quaracchi, t. 8, 1898, uk. 245 a.
[142]Taz. Conc. Vat.I, Schema De Ecclesia Christi, cap. XV na dondoo n.48: Mansi 51, 549 s. na 619 s. – Taz. Leo XIII, Epist. Au milieu des consolations, 23 desemba 1900: AAS 33 (1900-01) uk. 361. – Pius XII, Const.Apost. Provida Mater, l.c., uk. 114 s.
[143] Taz. Leo XIII, Const. Romanus Pontefices, 8 mei 1881: ASS 13 (1880-81) uk. 483. – Pius XII, Alloc. Annus sacer, 8 desemba 1950: AAS 43 (1951) uk. 28 s.
[144] Taz. Pius XII, Alloc. Annus sacer, l.c., uk. 28. – Id., Const. Apost. Sede Sapientiae, 31 mei 1956: AAS 48 (1956) uk. 355. – Paulus VI, Alloc. Magno gaudio, 23 mei 1964: AAS 56 (1964) uk. 570-571.
[145]Taz. Pius XII, Litt. Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 214 s.
[146] Taz. Pius XII, Alloc. Annus sacer, l.c., uk. 30. – Id., Alloc. Sous la maternelle protection, 9 desemba 1957: AAS 50 (1958) uk. 39 s..
[147]Taz. Conc. Flor., Decretum pro Graecis: Denz. 693 (1305).
[148]Licha ya hati za zamani dhidi ya aina yoyote ya kuwapandisha pepo, tangu wakati wa Iskanda IV (27 septemba 1258), taz. Encicl. S.S.C.S. Officii, De magnetismi abusu, 4 agosti 1856: ASS (1856) uk. 177-178, Denz. 1653-54 (2823-2825); jibu S.S.C.S. Officii, 24 aprile 1917: AAS (1917) uk. 268, Denz. 2182 (3642).
[149]Muhtasari wa mafundisho ya Mt. Paulo Mtume hupatikana katika: Pius XII, Litt. Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 200, na nyingine.
[150]Taz. k.m. Mt. Augustinus, Enarr. in Ps. 85,24: PL 37, 1099. – Mt. Hieronymus, Liber contra Vigilantium, 6: PL 23, 344. – Mt. Thomas, In quattrom Sent., d. 45, q. 3, a. 2. – Mt. Bonaventura, In quattrom Sent., d. 45, a. 3, q.2; n.k.
[151]Taz. Pius XII, Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 245.
[152]Taz. miandiko mingi iliyomo katika makatakombi huko Roma.
[153]Taz. Gelasius I, Decretalis De libris recipiendis, 3: PL 59, 160, Denz. 165 (353).
[154]Taz. Mt. Methodius, Symposion, VII, 3: GCS (Bonwetsch) uk. 74.
[155]Taz. Benedictus XV, Decretum approbationis virtutum in Causa beatificationis et canonizationis Servi Dei Ioannis Nepomuceni Neumann: AAS 14 (1922) uk. 23 – Hotuba nyingi za Pius XII juu ya watakatifu: Inviti all’eroismo, katika Discorsi e Radiomessaggi, tt.I-III, Romae, 1941-42, sehemu nyingi; Id., Discorsi e Radiomessaggi, t. 10, 1949, uk. 37-43.
[156]Taz. Pius XII, Litt. Enc. Mediator Dei, 20 novemba 1947: AAS 39 (1947) uk. 581.
[157] Taz. Ebr 13:7; YbS 44-50; Ebr 11:3-40. Taz. pia Pius XII, Litt. Enc. Mediator Dei, 20 novemba 1947: AAS 39 (1947) uk. 582 s.
[158]Taz. Conc. Vat.I, Const. dogm. De fide catholica, Dei Filius, cap. 3: Denz. 1794 (3013).
[159]Taz. Pius XII, Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 216.
[160]Kuhusu ushukrani kwa ajili ya watakatifu, taz. E. Diehl, Inscriptiones latinae christianae veteres, I, Berolini, 1925, nn. 2008, 2382 na nyingine.
[161]Taz. Conc. Trid., Decr. De invocatione...Sanctorum: Denz. 984 (1821).
[162] Breviarum romanum, mwaliko katika sherehe ya Watakatifu Wote.
[163]Taz. k.m. 2The 1:10.
[164]Conc. Vat. II, Const. de Sacra Liturgia, Sacrosanctum Concilium, cap. 5, n. 104: AAS 56 (1964) uk. 125-126.
[165] Missale romanum, Kanuni ya Misa.
[166]Conc. Nicaenum II, Act. VII: Denz. 302 (600).
[167]Conc. Flor., Decretum pro Graecis: Denz. 693 (1304).
[168]Conc.Trid., Decr. De invocatione, veneratione et reliquiis Sanctorum et sacris imaginibus: Denz. 984-988 (1821-1824). – Id., Decr. De Purgatorio: Denz 983 (1820). – Id., Decr. De Iustificatione, can. 30: Denz 840 (1580).
[169] Missale romanum, katika Utangulizi wa sherehe ya Watakatifu, uliotolewa kwa idhini kwa ajili ya majimbo kadha wa kadha (ya Ufaransa).
[170] Taz. Mt. Petrus Canisius, Catechismus Maior seu Summa Doctrinae christianae, cap. III (ed. crit. F. Streicher), sehemu ya I, uk. 15-16, n. 44 na uk. 100-101, n. 49.
[171]Taz. Conc. Vat. II, Const. de Sacra Liturgia, Sacrosanctum Concilium, cap. 1, n. 8: AAS 56 (1964) uk. 401.
[172] Symbolum Constantinopolitanum: Mansi 3, 566. Taz. Conc.Ephesinum, ibid. 4, 1130 (na pia ibid. 2, 665 na 4, 1071); Conc. Chalcedonense, ibid. 7, 111-116; Conc.Constantinopolitanum II, ibid. 9, 375-396; Missale romanum, katika “Nasadiki”.
[173] Missale romanum, Kanuni ya Misa.
[174]Mt. Augustinus, De S. Virginitate, . 6: PL 40, 399.
[175] Taz. Paulus VI, Allocutio in Concilio, 4 desemba 1963: AAS 56 (1964) uk. 37.
[176]Taz. Mt. Germanus Const., Hom. in Annunt. Deiparae: PG 98, 328A – Id., In Dorm. 2: col. 357 – Anastasius Anthioc., Serm. 2 de Annunt., 2: PG 89, 1377AB – Id., Serm. 3,2: col. 1388C. – Mt. Andreas Cret., Can. in B.V. Nat. 4: PG 97, 1321B. – Id., In B.V. Nat., 1: col. 812A. – Id., Hom. in Dorm. 1: col. 1068C. – Mt. Sophronius, Hor. 2 in Annunt., 18: PG 87 (3), 3237BD.
[177]Mt. Irenaeus, Adv.Haer.III, 22,4: PG 7, 959A; Harvey 2,123.
[178]Mt. Irenaeus, ibid.; Harvey 2,124.
[179]Mt. Epiphanius, Haer. 78, 18: PG 42, 728CD-729AB.
[180]Mt. Hieronymus, Epist. 22, 21: PL 22, 408. – Taz. Taz. Mt. Augustinus, Serm. 51,2,3: PL 38, 335. – Id., Serm. 232,2: 1108. – Mt. Cyrillus Hieros., Catech. 12, 15: PG 33, 741AB. – Mt. Ioannes Chrys., In Ps. 44, 7: PG 55, 193. – Mt. Ioannes Dam., Hom. 2 in Dorm. B. M. V., 3: PG 96, 728.
[181]Taz. Conc. Lateranense (mwaka 649), can. 3: Mansi 10, 1151. – Mt. Leo M., Epist. ad Flav.: PL 54, 759. – Conc.Chalcedonense: Mansi 7, 462. – Mt. Ambrosius, De instit. Virg.: PL 16, 320.
[182]Taz. Pius XII, Enc. Mystici Corporis, 29 juni 1943: AAS 35 (1943) uk. 247-248.
[183] Taz. Pius IX, Bulla Ineffabilis, 8 desemba 1854: Acta Pii IX, 1, I, uk. 616; Denz. 1641 (2803).
[184]Taz. Pius XII, Const. Apost. Munificentissimus, 1 novemba 1950: AAS 42 (1950); Denz. 2333 (3903). – Mt. Ioannes Dam., Enc. in Dorm.Dei genitricis, Hom. 2 na 3: PG 96, 721-761, hasa col. 728B. – Mt. Germanus Const., In. S. Dei gen. Dorm., Serm. 1: PG 98 (6), 340-348; ibid., Serm. 3: col. 361. – Mt. Modestus Hier., In Dorm. SS. Deiparae: PG 86 (2), 3277-3312.
[185] Taz. Pius XII, Litt. Enc. Ad coeli Reginam, 11 oktoba 1954: AAS 46 (1954) uk. 633-636; Denz. 3913 ss. – Taz. Mt. Andreas Cret., Hom 3 in Dorm. SS.Deiparae: PG 97, 1089-1109. – Mt. Ioannes Dam., De fide orth., IV, 14: PG 94, 1153-1161.
[186]Taz. Kleutgen, fasuli iliyorekebishwa De mystero Verbi incarnati, cap.IV: Mansi 53, 290. – Taz. Mt. Andreas Cret., In nat. Mariae, sermo 4: PG 97, 865A. – Mt. Germanus Const., In Annunt. Deiparae: PG 98, 321BC. – Id., In Dorm. Deiparae, III: col. 361D. – Mt. Ioannes Dam., In Dorm. B. M. V., Hom. 1, 8: PG 96, 712BC-713A.
[187]Taz. Leo XIII, Litt. Enc. Adiutricem populi, 5 septemba 1895: AAS 28 (1895-96) uk. 129. – Mt. Pius X, Litt.Encicl. Ad diem illum, 2 februari 1904: Acta, I, uk. 154; Denz. 1978a (3370). – Pius XI, Litt. Enc. Miserentissimus Redemptor, 8 mei 1928: AAS 20 (1928) uk. 178. – Pius XII, Nuntius radioph., 13 mei 1946: AAS 38 (1946) uk. 266.
[188] Taz. Mt. Ambrosius, Epist. 63: PL 16, 1218.
[189]Taz. Mt. Ambrosius, Expos. Lc., II, 7: PL 15, 1555.
[190]Taz. Ps. Petrus Dam., Serm. 63: PL 144, 861AB. – Godefridus wa Mt. Victore, In nat. B.M., Ms. Paris, Mazarine, 1002, fol. 109r. – Gerhohus Reich., De gloria et honore Filii hominis, 10: PL 194, 1105AB.
[191]Taz. Mt. Ambrosius, Expos.Lc., II, 7 na X, 24-25: PL 15, 1555 na 1810. – Mt. Augustinus, In Io., Tr. 13,12: PL 35, 1499. – Id., Serm. 191,2,3: PL 38, 1010; na nyingine. – Taz. pia Ven. Beda, In Lc. Expos. I, cap. 2: PL 92, 330. – Isaac de Stella, Serm. 51: PL 194, 1863A.
[192]Taz. Breviarium romanum, ant. “Sub tuum praesidium”, ya Vesperi I ya Ofisyo Ndogo ya Bikira Maria.
[193] Taz. Conc. Nicaenum II, anno 787: Mansi 13, 378-379; Denz. 302 (600-601). – Conc. Trid., Sess. 25: Mansi 33, 171-172.
[194]Taz. Pius XII, Nuntius radioph., 24 oktoba 1954: AAS 46 (1954) uk. 679. – Id., Litt. Enc. Ad coeli Reginam, 11 oktoba 1954: AAS 46 (1954) uk. 637.
[195]Taz. Pius XI, Litt. Enc. Ecclesiam Dei, 12 novemba 1923: AAS 15 (1923) uk. 581. – Pius XII, Litt. Enc. Fulgens corona, 8 septemba 1953: AAS 45 (1953) uk. 590-591.