[BE
-
CS -
DE -
EN -
ES -
FR -
IT -
HU -
LA -
PT -
SW -
ZH]
Konstitusio juu ya liturujia
SACROSANCTUM
CONCILIUM
Paulo Askofu
Mtumishi wa
Watumishi wa Mungu
pamoja na Mababa wa Mtaguso mkuu
ataka haya
yakumbukwe daima
UTANGULIZI
1. Mtaguso Mkuu (Sacrosanctum Concilium) umeazimu kukuza kila siku
zaidi na zaidi maisha ya kikristo kati ya waamini; kuzilinganisha taratibu
zile zinazobadilika na mahitaji ya siku hizi; kuyahimiza mambo yale yote
yanayosaidia kuleta umoja kati ya wote wanaomwamini Kristo; kuyaimarisha
yale yote yanayofaa kwa kuwaita wote kundini mwa Kanisa. Mtaguso huu Mkuu
unaona ni wajibu wake kujali kwa namna ya pekee kurekebisha na kukuza
Liturujia.
Nafasi ya Liturujia katika fumbo la Kanisa
2. Maana kwa njia ya Liturujia, hasa Sadaka takatifu ya Ekaristi,
“latimizwa tendo la ukombozi wetu”[1].
Liturujia inasaidia kikamilifu waamini waonyeshe katika maisha yao na
kuwadhihirishia wengine fumbo la Kristo na pia maumbile halisi ya Kanisa la
kweli. Kanisa kwa undani kabisa ni la kibinadamu na pia la kimungu,
linaloonekana lakini lenye yasiyoonekana ndani yake, lenye bidii kubwa
katika matendo na uradhi katika kutafakari, lililopo ulimwenguni lakini kama
mwenye kuhiji. Hayo yote yamo ili yale ya kibinadamu ndani yake yaelekezwe
kwa yale ya kimungu, yaonekanayo kwa yasiyoonekana, matendo kwenye
kutafakari, yaliyopo yaelekee mji ujao tunakoelekea[2].
Hivyo Liturujia kila siku inawajenga wale waliomo katika Kanisa wawe hekalu
takatifu la Bwana, makao ya Mungu katika Roho[3],
mpaka kuufikia utimilifu wa Kristo[4].
Wakati huohuo kwa namna ya ajabu Liturujia inaimarisha nguvu za waamini
kumhubiri Kristo; na kwa njia hiyo inawaonyesha wale walio nje [nalo,]
Kanisa lililo ishara iliyoinuliwa juu kati ya mataifa[5],
ambayo chini yake watoto wa Mungu waliotawanyika wakusanyika katika umoja[6],
mpaka liwepo zizi moja na mchungaji mmoja[7].
Hati hii juu ya Liturujia na Riti mbalimbali
3. Kwa hiyo Mtaguso Mkuu unadhamiria kwamba inabidi kukumbusha kanuni
zifuatazo kuhusu ukuzaji na marekebisho ya Liturujia, na kutoa miongozo ya
utekelezaji.
Kati ya kanuni na sheria hizo, zipo nyingi zinazoweza kutumika na
lazima zitumike katika Riti*[, au
madhehebu,] ya Kiroma (Ritum romanum) na pia Riti nyinginezo.
Miongozo ya utekelezaji ifuatayo, lakini, ni kwa ajili ya Riti ya Kiroma tu,
isipokuwa kama ni mambo ambayo, kwa maumbile yake yenyewe, yanahusu pia Riti
nyingine.
Heshima kwa Riti zote zilizo halali
4. Mwishowe, Mtaguso Mkuu, kwa kuheshimu kiaminifu Mapokeo, unathibitisha
kwamba Mama Kanisa anastahi kwa heshima moja Riti zote (omnes Ritus)
zilizokubaliwa kuwa halali. Tena Mtaguso unatamani kwamba [Riti hizo]
zihifadhiwe kwa baadaye na kuendelezwa kwa hali na mali. Aidha, Mtaguso
unatamani zitengenezwe upya, kama ni lazima, kwa utaratibu na kadiri ya
Mapokeo halisi na pia zipewe nguvu mpya kulingana na mazingira ya sasa.
Sura ya Kwanza
KANUNI ZA JUMLA ZA MAREKEBISHO NA UKUZAJI WA LITURUJIA
TAKATIFU
I - MAUMBILE YA LITURUJIA NA UMUHIMU WAKE KATIKA MAISHA YA KANISA
5. Mungu, “ambaye hutaka watu wote waokolewe na kupata kujua yaliyo
kweli” (1Tim 2:4), “ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa
sehemu nyingi na kwa njia nyingi” (Ebr 1:1), ulipofika utimilifu wa nyakati
akamtuma Mwanawe, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, aliyetiwa mafuta kwa
Roho Mtakatifu, ili awahubiri maskini habari njema, awagange waliovunjika
moyo[8], yeye aliye “mganga wa
mwili na wa roho”[9],
Mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu[10].
Maana ubinadamu wake, katika kuungana na Neno, ulikuwa chombo cha wokovu
wetu. Kwa hiyo “katika Kristo ulitokea utimilifu halisi wa upatanisho wetu,
nasi tulipewa ukamilifu wa ibada kwa Mungu”[11].
Tendo hilo la ukombozi wa wanadamu na la kutukuzwa kwake kamili, lenye
utangulizi wake katika miujiza iliyotendeka kwa taifa la Agano la Kale,
lilitimizwa na Bwana Yesu hasa kwa njia ya fumbo la Pasaka ya mateso yake
yenye heri, ufufuko wake kutoka kuzimu, na kupaa kwake mbinguni kwa utukufu;
fumbo ambalo kwa ajili yake “kwa kufa aliangamiza mauti na alipofufuka
akaturudishia uzima”[12].
Maana, kutoka ubavuni mwa Kristo akilala msalabani ilitoka sakramenti ya
ajabu ya Kanisa lote[13].
Tendo la wokovu linaloendelezwa na Kanisa hutimizwa katika Liturujia
6. Kama vile Kristo alivyotumwa na Baba, kadhalika naye aliwatuma Mitume,
waliojaa Roho Mtakatifu.Alifanya hivyo sio tu ili watangaze, kwa kuhubiri
Injili kwa kila kiumbe[14],
kwamba Mwana wa Mungu, kwa kifo na ufufuko wake, ametuokoa kutoka mamlaka ya
shetani[15]na ya mauti na
kutuleta katika ufalme wa Baba yake; bali, pia alitaka kazi hiyo ya
ukombozi, ambayo walikuwa wakiitangaza, waitekeleze kwa njia ya Sadaka na
Sakramenti, ambazo ni kiini cha maisha ya kiliturujia. Hivyo, kwa njia ya
Ubatizo, wanadamu wanaingizwa katika fumbo la Pasaka ya Kristo: wanakufa
pamoja naye, wanazikwa na kufufuka pamoja naye[16],
wanapokea roho ya kufanywa wana “ambayo kwa hiyo twalia: Aba, yaani Baba”
(Rum 8:15); na hivyo wanapata kuwa wale waabuduo halisi ambao Baba awatafuta[17].
Kadhalika, kila wailapo karamu ya Bwana, waitangaza kifo cha Bwana hata
ajapo[18]. Kwa hiyo, siku
ileile ya Pentekoste, ambapo Kanisa lilidhihirishwa ulimwenguni, “wale
waliolipokea neno” la Petro “wakabatizwa”. Nao “wakawa wakidumu katika
fundisho la Mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika
kusali ... wakimsifu Mungu kwa pamoja, na kuwapendeza watu wote” (Mdo
2:41-42.47 Vulg.). Tokea hapo, Kanisa halijaacha kamwe kujumuika
pamoja ili kuliadhimisha fumbo la Pasaka: kwa kuyasoma yote “katika Maandiko
yanayomhusu Yeye [Kristo]” (Lk 24:27), kwa adhimisho la Ekaristi, ambapo
“vimefanyika wazi tena mafanikio na ushindi mkuu wa kifo chake”[19],
na kwa kumshukuru “Mungu kwa sababu ya kipawa chake tusichoweza kukisifu
kama ipasavyo” (2Kor 9:15), katika Yesu Kristo, “kwa sifa ya utukufu wake”
(Efe 1:12), kwa nguvu ya Roho Mtakatifu.
Uwepo wa Kristo katika Liturujia
7. Kusudi kutimiza tendo kubwa namna hii, Kristo yupo daima katika Kanisa
lake, kwa jinsi ya pekee katika maadhimisho ya kiliturujia. Yupo kwenye
Sadaka ya Misa katika nafsi ya kasisi, “Yeye ambaye, akijitoa mara moja
msalabani, anajitoa tena mwenyewe kwa huduma ya mapadre”[20].
Yupo hasa chini ya maumbo ya Ekaristi. Yupo kwa nguvu yake katika
sakramenti, ili kwamba mtu anapobatiza, ni Kristo mwenyewe anayebatiza[21].
Yupo katika Neno lake, kwa kuwa ni Yeye anayesema wakati Maandiko Matakatifu
yanaposomwa katika Kanisa. Yupo, tena, wakati Kanisa linaposali (supplicat)
na kuimba zaburi (psallit), kwa vile aliahidi: “Walipo wawili watatu
wamekusanyika kwa jina langu nami nipo papo hapo katikati yao” (Mt 18:20).
Kwa kweli, katika tendo kubwa namna hii, ambalo kwa njia yake Mungu
hutukuzwa kikamilifu na wanadamu wanatakatifuzwa, Kristo daima
hulishirikisha Kanisa; naye Kanisa ni Bibiarusi yake mpendwa sana, ambaye
anamwomba Bwana wake na kwa njia yake anamwabudu Baba wa milele.
Kumbe, kwa haki Liturujia hutazamwa kama utekelezaji wa kazi ya kikuhani
ya Yesu Kristo. Katika Liturujia, kwa ishara zinazoonekana, huo-nyeshwa na
kutendeka kutakatifuzwa kwake binadamu, kila ishara ikiwa na maana ya pekee.
Katika Liturujia, ibada halisi za hadhara huadhimishwa na Mwili wa fumbo wa
Yesu Kristo, yaani na Kichwa na viungo vyake.
Kwa hiyo kila adhimisho la kiliturujia, kwa kuwa ni tendo la Yesu Kristo
Kuhani na la Mwili wake, ndilo Kanisa, ni tendo takatifu kupita yote na
hakuna tendo jingine la Kanisa linalofanana nalo kwa manufaa kwa kiwango
kilekile na kwa daraja ileile.
Liturujia ya duniani na ile ya mbinguni
8. Katika Liturujia ya hapa duniani sisi tunashiriki, tukiionja,
Liturujia ya mbinguni, iadhimishwayo katika Mji Mtakatifu wa Yerusalemu,
tunaouelekea kama wasafiri, ambako Kristo ameketi mkono wa kuume wa Mungu
kama mhudumu wa patakatifu na wa ile hema ya kweli[22].
Tunaungana na wapiganaji wa jeshi la mbinguni kumwimbia Bwana wimbo wa
utukufu. Tukiwakumbuka kwa heshima watakatifu, twatumaini kupata ushirika
nao; twamngojea kwa shauku Mkombozi, Bwana wetu Yesu Kristo, mpaka
atakapojidhihirisha, Yeye aliye uzima wetu, ndipo na sisi
tutakapodhihirishwa pamoja naye katika utukufu[23].
Liturujia takatifu haimalizi utendaji wote wa Kanisa
9. Liturujia takatifu haimalizi utendaji wote wa Kanisa. Maana, kabla
wanadamu hawajaikaribia Liturujia, yabidi waalikwe kwenye imani na toba:
“Wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena
wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije wasipopelekwa?” (Rum 10:14-15).
Kwa hiyo Kanisa laihubiri habari njema ya wokovu kwa wale
wasioamini, kusudi watu wote wamjue Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo
aliyemtuma, na pia, wakitubu, waongoke kutoka njia zao[24].
Aidha, Kanisa lazima lihubiri daima imani na toba kwa waamini; lazima pia
liwatayarishe kwa Masakramenti, liwafundishe kuyashika yote yaliyoamriwa na
Kristo[25], na pia liwahimize
kwenye matendo yote ya mapendo, ya ibada na ya utume, ambayo huonyesha ya
kuwa waamini wa Kristo si wa ulimwengu huu, lakini wao ni nuru ya ulimwengu
na lazima wamtukuze Baba mbele ya watu.
Liturujia ni kilele na chemchemi ya maisha ya Kanisa
10. Hata hivyo Liturujia ni kilele ambapo kazi ya Kanisa inaelekea, na
papo hapo ni chemchemi zinamotoka nguvu zake zote. Maana, bidii zote za kazi
za kitume hukusudiwa ili wote, waliofanywa watoto wa Mungu kwa njia ya imani
na Ubatizo, wakusanyike pamoja, wamtukuze Mungu katika Kanisa, washiriki
sadaka na kuila karamu ya Bwana.
Kwa upande wake, Liturujia huwasukuma waamini, waliolishwa kwa
“sakramenti za kipasaka”, kuishi katika “umoja wa utakatifu”[26].
Tena huwaombea “waonyeshe katika maisha yao yale waliyopewa katika imani”[27].
Aidha, kufanyika upya kwa agano la Bwana na wanadamu katika Ekaristi
kuwavuta na kuwasha ndani ya waamini upendo wenye bidii wa Kristo. Kwa hiyo
kutokana na Liturujia, hasa Ekaristi, humiminwa ndani yetu neema, kama toka
chemchemi, na pia hupatikana kikamilifu lengo la utendaji wote wa Kanisa
ambalo ni utakatifu ule wa wanadamu na tukuzo la Mungu, katika Kristo.
Umuhimu na maelekeo ya kila mtu katika Liturujia
11. Lakini, ili kufikia lengo hilo kamili, sharti waamini washiriki
Liturujia takatifu kwa maelekeo ya moyo mnyofu, walinganishe akili zao na
sauti, wafanye kazi pamoja na neema ya Mungu ili wasiipokee bure[28].
Kwa hiyo wachungaji watukufu wanapaswa kuangalia kuwa katika tendo la
Liturujia zishikwe sheria zifanyazo maadhimisho yawe thabiti na halali.
Wachungaji pia lazima wahakikishe kuwa waamini wanaelewa kinachofanyika na
wanashiriki kikamilifu na kufaidi matunda ya maadhimisho hayo.
Liturujia na sala ya binafsi
12. Lakini maisha ya kiroho hayaishii katika kuishiriki Liturujia
takatifu tu. Maana mkristo, anayealikwa kushiriki sala ya pamoja, anapaswa
pia aingie chumbani mwake kumwomba Baba katika siri[29].
Aidha, kadiri ya mafundisho ya Mtume anapaswa kusali bila kukoma[30].
Naye Mtume mwenyewe hutufundisha kuchukua sikuzote katika mwili wetu mateso
yake Yesu, ili uzima wa Yesu nao hudhihirishwe katika mwili wetu wenye kufa[31].
Kwa sababu hiyo katika sadaka ya Misa twamwomba Bwana kwamba “anapopokea
sadaka ya dhabihu ya kiroho” atufanye sisi wenyewe kuwa kwake “sadaka ya
milele”[32].
Ibada mbalimbali za wakristo zielekee kwenye Liturujia
13. Ibada mbalimbali za watu wakristo, mradi zilingane na kanuni na
taratibu za Kanisa, zinahimizwa sana, hasa zinapofanyika kwa agizo la Kiti
cha Kitume.
Ibada mbalimbali za Makanisa maalum (particularium) zina hadhi ya
pekee, hasa zinapofanyika kwa agizo la Maaskofu, kadiri ya desturi au vitabu
vilivyoidhinishwa kihalali.
Ibada hizo, lakini, sharti zipangwe kwa kulingana vipindi vya mwaka wa
kiliturujia, zilingane na Liturujia takatifu, zitokane nayo kwa namna
fulani, na kuwaelekeza watu kwenye Liturujia yenyewe, kwa sababu, kwa tabia
yake, Liturujia ina hadhi ya juu zaidi kuliko ibada za watu.
II - UMUHIMU WA KUHIMIZA MALEZI YA KILITURUJIA NA KUSHIRIKI HAI KWA WAAMINI
14. Mama Kanisa anatamani sana waamini wote waongozwe kwenye kuyashiriki
maadhimisho ya kiliturujia kwa utimilifu, kwa ufahamu na utendaji. Jambo
hili linadaiwa na tabia ya Liturujia yenyewe na pia – kwa sababu ya Ubatizo
[wao], ni haki na wajibu wa watu wakristo, ambao ni “mzao mteule, ukuhani wa
kifalme, taifa takatifu, watu wa milki wa Mungu” (1Pet 2:9; taz. 2:4-5).
Katika kurekebisha na kukuza Liturujia lazima kujali kwa namna ya pekee
kushiriki huko kwa utimilifu na utendaji kwa waamini wote: maana [Liturujia]
ni chemchemi ya kwanza na ya lazima ambayo toka kwake waamini wanaweza
kuchota roho kweli ya kikristo. Kwa hiyo wachungaji wa roho, katika kazi zao
zote za kitume, wanapaswa kuishughulikia bila kukoma kwa njia ya mafundisho
yafaayo.
Lakini haiwezekani kutumaini kuyatimiza hayo, kama wachungaji wenyewe
hawajawa na roho na nguvu ya Liturujia, na kabla hawajajielimisha ili
wawaelimishe na wengine. Kwa hiyo ni muhimu kabisa, awali ya yote, makleri
wapate mafundisho juu ya Liturujia. Kwa sababu hiyo Mtaguso Mkuu unaagiza
yafuatayo.
Malezi ya maprofesa wa Liturujia
15. Walimu wanaochaguliwa kufundisha Liturujia katika seminari, katika
vituo vya malezi ya kitawa, na katika vyuo vya elimu ya Teolojia, ni lazima
wapate elimu inayoifaa kazi yao katika vyuo vinavyofundisha haya kwa namna
ya pekee.
Ufundishaji wa Liturujia
16. Liturujia takatifu katika seminari na nyumba za malezi ya kitawa,
lazima ihesabiwe kati ya masomo ya lazima na ya muhimu zaidi. Aidha, katika
vyuo vya Teolojia ihesabiwe kati ya masomo ya maana zaidi, na ifundishwe
kadiri ya muono wa kiteolojia, wa kihistoria, wa kiroho, wa kichungaji na wa
kisheria. Aidha, walimu wa masomo mengine, hasa walimu wa Dogma, Maandiko
Matakatifu, Teolojia ya maisha ya kiroho na ya kichungaji, wajitahidi
kusisitiza, kila mmoja kadiri ya matakwa ya masomo yake, fumbo la Kristo na
historia ya wokovu ili uonekane wazi uhusiano wake na Liturujia, na jinsi
masomo hayo yanavyohusiana katika malezi ya kipadre.
Malezi ya waseminari kuhusu Liturujia
17. Waseminari wakubwa, katika seminari na katika nyumba za kitawa,
waelimishwe juu ya Liturujia katika maisha ya kiroho; yaani waingizwe
polepole ili waweze kuelewa maana ya madhehebu takatifu na kushiriki kwa
moyo wote, na pia wapate kuadhimisha mafumbo matakatifu na ibada nyingine
zenye roho ya kiliturujia. Pia wajifunze kuzishika sheria za kiliturujia,
ili maisha katika seminari na katika nyumba za malezi za kitawa zitawaliwe
na roho ya kiliturujia.
Kuwasaidia mapadre mintarafu Liturujia
18. Mapadre, wanajimbo na pia watawa, wanaofanya kazi tayari katika
shamba la mzabibu la Bwana, wasaidiwe kwa kila namna ifaayo ili waelewe
zaidi na zaidi yale watendayo katika ibada takatifu, tena wasaidiwe kuishi
maisha ya kiliturujia na kuwashirikisha waamini waliokabidhiwa.
Kuwaelimisha waamini juu ya Liturujia
19. Wachungaji wa roho wajitahidi, kwa bidii na saburi, ili waamini
waelimishwe juu ya Liturujia na pia waweze kuishiriki kikamilifu, katika
mwili na katika roho, kulingana na umri wao, hali yao, aina ya maisha yao na
elimu yao ya kidini. Kwa njia hii wachungaji hawa watatimiza moja ya
majukumu yao ya kwanza, yaani kuwa wagawaji waaminifu wa mafumbo ya Mungu.
Aidha, waliongoze kundi lao katika mambo hayo, si kwa maneno tu, bali pia
kwa mifano.
Vyombo vya upashanaji habari na Liturujia
20. Kama zinatumiwa redio na televisheni kutangaza ibada takatifu, hasa
Misa, matumizi ya vyombo hivyo yawe ya heshima na utaratibu, chini ya
uongozi na udhamini wa mtu mwenye ujuzi, ambaye ameteuliwa na Maaskofu kwa
kazi hiyo.
III - MAREKEBISHO YA LITURUJIA TAKATIFU
21. Mama Kanisa anatamani kufanya kwa uangalifu marekebisho ya Liturujia
yenyewe, ili kuhakikisha kuwa wakristo wanapata wingi wa neema katika
Liturujia takatifu. Katika Liturujia ipo sehemu isiyobadilika, kwa sababu
imewekwa na Mungu; na pia zipo sehemu zinazoweza kubadilika, nazo ni zile
ambazo, kufuatana na mwenendo wa nyakati, zinaweza au pia zinapaswa
kubadilika, endapo ndani yake yameingia mambo yasiyolingana na maumbile
halisi ya Liturujia yenyewe, au inapoonekana kutofaa tena.
Katika marekebisho hayo, inabidi kuratibu matini na madhehebu za ibada
ili zionyeshe kinaganaga zaidi mambo matakatifu zinayoisharisha, nao
wakristo waweze kuyaelewa kwa urahisi iwezekanavyo na kuyashiriki
kikamilifu, kwa bidii na kama jumuiya.
Kwa sababu hiyo, Mtaguso Mkuu unaweka kanuni za jumla zifuatazo.
A) Kanuni za jumla
Kuratibu Liturujia ni juu ya Hierarkia
22. § 1. Kuratibu Liturujia takatifu ni juu ya mamlaka ya Kanisa tu,
ambayo ipo katika Kiti Kitakatifu na, kadiri ya sheria, kwa Maaskofu.
§ 2. Kwa uwezo unaotokana na sheria, kuratibu Liturujia, kadiri ya mipaka
iliyokubaliwa, ni juu ya Mabaraza mbalimbali ya Maaskofu ya nchi fulani
yaliyoundwa kwa mujibu wa sheria kusimamia nchi hizo.
§ 3. Kwa hiyo, mtu mwingine yeyote yule, hata akiwa padre, hawezi
kuongeza, kuondoa au kubadili jambo lolote kwa uamuzi wake mintarafu
Liturujia.
Mapokeo na maendeleo
23. Ili kuyahifadhi mapokeo mema, na hapohapo lakini kufanyiza maendeleo
ya halali yasitawi, marekebisho ya kila sehemu ya Liturujia lazima
yatanguliwe na uchunguzi wa kina wa kiteolojia, wa kihistoria na wa
kichungaji. Aidha, marekebisho hayo yazijali kanuni za jumla zinazohusu
muundo na roho ya Liturujia. Tena yajali mang’amuzi yatokanayo na
marekebisho ya Liturujia ya hivi karibuni na ruhusa (indultis)
zilizokubaliwa mahali mbalimbali. Mwishowe, mabadiliko yasifanywe isipokuwa
inapodaiwa na manufaa ya kweli ya Kanisa, kwa uangalifu ili mambo mapya
yatokane kwa mpangilio na yale yaliyopo.
Pia, kadiri iwezekanavyo, kusiwe na tofauti kubwa kati ya ibada katika
nchi zilizo jirani.
Biblia na Liturujia
24. Jambo muhimu kuliko yote katika adhimisho la Liturujia ni Maandiko
Matakatifu, maana katika hayo huchukuliwa masomo ya kusomwa na kufafanuliwa
katika mahubiri, na pia zaburi zinazoimbwa. Sala, maombi na nyimbo hupata
uvuvio toka Maandiko, kama vile toka Maandiko matendo na ishara hupata
maana. Kwa hiyo, ili kufaulu kufanya marekebisho na maendeleo na
malinganisho ya Liturujia, ni lazima kuhimiza ule upendo mtamu na hai wa
Maandiko Matakatifu, ambao unashuhudiwa na mapokeo mastahiki ya Makanisa ya
Mashariki na ya Magharibi.
Marekebisho ya vitabu vya Liturujia
25. Vitabu vya kiliturujia virekebishwe upesi iwezekanavyo; kazi hiyo
ifanywe na watu wenye ujuzi, na maoni ya Maaskofu wa nchi mbalimbali
yasikilizwe.
B) Kanuni zitokanazo na tabia ya kidaraja na ya kijumuiya ya Liturujia
26. Matendo ya kiliturujia si matendo ya kila mmoja peke yake, bali ni
maadhimisho ya Kanisa, ambalo ni “sakramenti ya umoja”, yaani taifa takatifu
linalokusanywa na kuratibishwa chini ya uongozi wa Maaskofu[33].
Kwa sababu hiyo matendo hayo ni ya mwili wote kabisa wa Kanisa, nayo
huudhihirisha na kuuimarisha. Aidha, kila mmoja wa wanakanisa anahusika kwa
namna tofauti, kadiri ya utofauti wa daraja, wa majukumu, na wa ushiriki
kiutendaji
Ubora wa adhimisho la pamoja
27. Kila mara ibada, kulingana na maumbile ya kila moja, zinapodai
adhimisho la pamoja kwa mahudhurio ya waamini wanaoshiriki kimatendo,
ihimizwe kwamba adhimisho hilo ni la kupendelewa zaidi, kadiri
inavyowezekana, kuliko adhimisho la mtu peke yake, kana kwamba lingekuwa
ibada ya binafsi.
Hayo yanahusu hasa adhimisho la Misa – hata kama kila Misa ni daima tendo
la hadhara na la kijumuiya – na pia maadhimisho ya sakramenti.
Nafasi ya kila mmoja katika adhimisho la Liturujia
28. Katika maadhimisho ya liturujia kila mmoja, mhudumu au mwamini, aliye
na kazi ya kufanya, atekeleze yote na sehemu zile tu zinazohusu wajibu wake,
kulingana na maumbile ya ibada na kanuni za Liturujia.
29. Pia watumishi wa altare, wasomaji, wenye kueleza ibada na wanakwaya
wote, wanatekeleza huduma kweli ya kiliturujia. Kwa hiyo inawapasa
watekeleze kazi yao kwa ule uchaji wa kweli na adabu inayofaa huduma muhimu
namna hii, na ambayo taifa la Mungu kwa haki linadai kwao.
Hivyo inabidi wajawe kwa makini na roho ya kiliturujia, kila mmoja kadiri
ya hali yake; na pia wafundishwe kutenda yote kufuatana na kanuni za
utaratibu zilizowekwa.
Kushiriki kikamilifu kwa waamini
30. Ili kuwawezesha waamini washiriki kimatendo, mashangilio ya waamini,
maitikio, kuimba zaburi, antifona, nyimbo, vitendo, ishara na mkao wa mwili
vitiliwe maanani. Unyamavu mtakatifu utumike pia, wakati unapodaiwa.
31. Katika marekebisho ya vitabu vya kiliturujia, iangaliwe kwa makini
kwamba maelekezo (rubricae) yanayowahusu waamini pia yawekwe wazi
kabisa.
Liturujia na usawa wa waamini
32. Katika Liturujia usiwepo upendeleo wowote kwa watu binafsi ama cheo,
iwe katika maadhimisho au katika fahari ya nje, isipokuwa kwa cheo
kitokanacho na kazi ya kiliturujia na Daraja takatifu; au pia heshima
zinazowapasa viongozi wa serikali kwa kadiri ya sheria za kiliturujia.
C) Kanuni zitokanazo na tabia ya kiliturujia ya kuelimisha na kuwalea
waamini
33. Ingawa Liturujia takatifu ni hasa ibada kwa Mungu Mkuu, yamo pia
ndani yake mafundisho tele kwa waamini[34].
Maana katika Liturujia Mungu anaongea na watu wake; naye Kristo anaendelea
kuhubiri Injili. Waamini kwa upande wao wanamwitikia Mungu kwa nyimbo na
sala.
Sala zinazoinuliwa kwa Mungu na padre, aongozaye ibada katika nafsi ya
Kristo, zinasemwa kwa niaba ya taifa zima takatifu na wote waliopo. Na zile
ishara zinazoonekana, ambazo Liturujia huzitumia kwa kuyaashiria yale mambo
ya kimungu yasiyoonekana, zilichaguliwa na Kristo au na Kanisa. Kwa hiyo si
yanaposomwa tu “yaliyoandikwa kwa kutufundisha sisi” (Rum 15:4), lakini pia
Kanisa linaposali au kuimba au kutenda, imani ya wale wanaoshiriki
inalishwa, akili zao zinainuliwa kwa Mungu, ili kumtolea heshima ipasayo na
kupokea kwa wingi zaidi neema yake.
Kwa hiyo, katika kufanya marekebisho ya Liturujia kanuni za jumla
zifuatazo hazina budi kuzingatiwa.
Ukamilifu na kueleweka kwa ibada
34. Ibada zing’ae kwa heshima na urahisi, ziwe fupi, wazi na bila marudio
ya bure. Zilingane na uwezo wa ufahamu wa waamini, bila kuhitaji, kwa
kawaida, maelezo mengi.
Biblia, homilia na katekesi kuhusu Liturujia
35. Ili ionekane wazi kwamba katika Liturujia matendo ya ibada na
Neno vimeunganika kiundani:
1) Katika ibada takatifu, masomo ya Maandiko Matakatifu yapangwe
kwa wingi zaidi, kutoka sehemu mbalimbali na kwa jinsi inayofaa zaidi.
2) Wakati ufaao zaidi kwa mahubiri, kama sehemu ya adhimisho la
Liturujia, kwa kadiri ya ibada yenyewe inavyoruhusu, uwekwe na kutajwa pia
katika rubrika (maelekezo). Huduma ya kuhubiri itimizwe kwa uaminifu kamili
na jinsi ifaavyo. Aidha, mahubiri yachotwe hasa kutoka chemchemi ya Maandiko
Matakatifu na ya Liturujia, kwani ni tangazo la matendo makuu ya Mungu
katika historia ya wokovu, iliyo fumbo la Kristo, fumbo ambalo daima lipo na
linatenda kazi ndani yetu, hasa katika maadhimisho ya kiliturujia.
3) Mafundisho kuhusu Liturujia yenyewe yatolewe kwa njia
mbalimbali. Katika ibada zenyewe yatolewe maelezo mafupi, ikiwa ni lazima.
Hayo yafanywe kwa maneno yaliyotayarishwa au kwa mengine yanayofanana nayo,
na padre au mhudumu mwenye uwezo. Lakini hayo yote yafanywe tu katika nafasi
zifaazo zaidi.
4) Ibada ya Neno la Mungu ihimizwe, hasa katika makesha ya sherehe, au
siku za Majilio na Kwaresima, siku za Dominika na sikukuu, hasa pale
asipokuwepo padre. Ikiwa ni hivyo, ibada iongozwe na shemasi au mtu mwingine
aliyeruhusiwa na Askofu.
Lugha ya Liturujia
36. § 1. Matumizi ya lugha ya kilatini yahifadhiwe katika
madhehebu za ibada za kilatini, licha ya sheria za pekee zikiwemo.
§ 2. Lakini, mara nyingi zaidi itumike lugha ya nchi kwani yaweza
kuwafaa sana waamini, iwe katika Misa, katika kuadhimisha Sakramenti, na pia
katika sehemu nyingine za Liturujia. Katika masomo na maelekezo, katika
baadhi ya sala na nyimbo, lugha ya nchi ipate nafasi zaidi. Kanuni
zinazohusu jambo hili zimetolewa peke yake katika sura zifuatazo.
§ 3. Kadiri ya kanuni hizo, kutoa uamuzi mintarafu matumizi ya
lugha ya nchi ni juu ya mamlaka ya kikanisa husika ya kila nchi, kama
ilivyoandikwa katika ibara 22 § 2. Na ikiwa inafaa, maoni ya Maaskofu wa
nchi jirani zinazotumia lugha hiyo yasikilizwe. Maamuzi hayo lazima yapate
kibali, yaani idhini, cha Kiti cha Kitume.
§ 4. Tafsiri ya vitabu vya Liturujia vya kilatini lazima ikubaliwe na
mamlaka ya kikanisa husika ya nchi ile, kama yalivyotajwa hapo juu.
D) Kanuni za marekebisho ya Liturujia kulingana na hali za watu na mapokeo
yao
37. Kanisa, katika yale yasiyogusa imani au manufaa ya jumuiya
nzima ya waamini, halipendi kuwabana wote kwa mtindo moja, wala katika
Liturujia. Kanisa huheshimu na kuhimiza vipawa na tunu za mila za kila taifa
na jamii. Katika tamaduni za mataifa, yale ambayo hayafungamani kabisa na
ushirikina au makosa, Kanisa huyachunguza kwa wema na pia, kama inawezekana,
huyahifadhi yalivyo. Na mara nyingine huyaingiza hata katika Liturujia
yenyewe, iwapo tu yanalingana na roho ya kweli na halisi ya kiliturujia.
38. Pasipo kuvunja umoja wa Riti ya Kiroma, katika marekebisho ya
vitabu vya Liturujia, iachwe nafasi kwa ajili ya tofauti zilizo halali na
kwa marekebisho yanayoweza kufanywa na jamii, nchi na mataifa mbalimbali,
hasa katika nchi za misioni. Hayo yatiliwe maanani katika mipangilio ya
ibada na katika kuandaa maelekezo (rubricis) ya jinsi ibada
zinavyofanyika.
39. Kadiri ya maagizo yaliyomo katika matoleo halisi (editionibus
typicis) ya vitabu vya kiliturujia, mamlaka ya kufanya marekebisho ni
juu ya Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali, kama ilivyoelezwa katika ibara
22 § 2; marekebisho hayo yahusu hasa utoaji wa Sakramenti, visakramenti,
maandamano, lugha na muziki na sanaa za kiliturujia kadiri ya kanuni za
msingi zilizomo katika hati hii.
Jinsi ya kufanya marekebisho ya Liturujia
40. Kwa kuwa katika nchi mbalimbali marekebisho ya kina ya
Liturujia yanatakiwa upesi, nayo yanaleta ugumu zaidi, basi, kwa sababu
hiyo:
1) Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali, kama ilivyoelezwa katika
ibara 22 § 2, yachunguze kwa makini na busara mambo yaliyomo katika mila na
desturi ya kila jamii ambayo yanaweza kuingizwa, kwa namna ifaayo, katika
ibada kwa Mungu. Hatimaye, marekebisho yanayodhaniwa kuwa ni ya kufaa au ya
lazima, yapelekwe kwa Baba Mtakatifu kusudi yaingizwe kwa idhini yake.
2) Kusudi marekebisho hayo yafanyike kwa tahadhari inayotakiwa,
Baba Mtakatifu atatoa idhini kwa Mabaraza ya Maaskofu ili yaruhusu na
kuongoza, ikiwa inafaa, majaribio ya kwanza yatakiwayo katika vikundi
vilivyoandaliwa kwa kusudi hilo na kwa muda wa kupangwa.
3) Kwa vile sheria za kiliturujia mara nyingi huleta matatizo mintarafu
marekebisho, hasa katika misioni, ni lazima wataalamu wahusishwe katika
kuzitunga sheria hizo.
IV - KUKUZA MAISHA YA KILITURUJIA JIMBONI NA PAROKIANI
41. Askofu lazima atazamwe kama kuhani mkuu wa kundi lake na
ambaye maisha ya waamini wake katika Kristo kwa namna fulani yanatoka kwake
na yanamtegemea.
Kwa hiyo ni lazima waamini wote wakaze sana umuhimu wa maisha ya
kiliturujia ya jimbo pamoja na Askofu, hasa katika kanisa katedrali (cathedrali):
wote waelewe kwamba Kanisa ladhihirika hasa katika ushirikiano kamili na wa
kimatendo wa taifa lote takatifu la Mungu katika maadhimisho yaleyale ya
kiliturujia, hasa katika Ekaristi ileile moja, sala ileile na altare ileile
anapoongoza Askofu pamoja na mapadre wake na watumishi[35].
Maisha ya kiliturujia katika parokia
42. Maadam Askofu hawezi mwenyewe kuongoza daima na popote kundi
lake zima katika Kanisa lake, basi Askofu hana budi kuwagawanya waamini
katika makundi mbalimbali, na kati ya hayo yana umuhimu wa maana sana
maparokia yanayoundwa kila mahali chini ya uongozi wa mchungaji
amwakilishaye Askofu; maana, hayo yanawakilisha kwa namna fulani Kanisa
lionekanalo ambalo limewekwa katika dunia nzima.
Kwa hiyo maisha ya kiliturujia ya parokia na uhusiano wake na Askofu
lazima visitawishwe katika roho na matendo ya waamini na wakleri; pia lazima
kufanya jitihada ili hisia ya jumuiya katika parokia ichanue hasa katika
kuadhimisha pamoja Misa ya Dominika.
V - KUKUZA KAZI YA KICHUNGAJI MINTARAFU LITURUJIA
43. Hamasa ya kukuza na kurekebisha Liturujia inatazamwa kwa haki
kama ishara ya Maongozi ya Mungu katika nyakati zetu, na pia kama mpito wa
Roho Mtakatifu katika Kanisa lake; tena inapiga chapa mahsusi kwa maisha ya
Kanisa na pia kwa mwelekeo mzima wa dini kimawazo na kimatendo kwa wakati
huu.
Kwa sababu hiyo, kwa lengo la kuongeza zaidi na zaidi katika Kanisa kazi
hiyo ya kichungaji mintarafu Liturujia, Mtaguso Mkuu unaamua yafuatayo:
Kamati ya Liturujia kitaifa
44. Yafaa Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali, kama ilivyoelezwa katika
ibara 22 § 2, yaunde kamati ya Liturujia ambayo itafanya kazi ikisaidiwa na
wataalamu wa Liturujia, muziki, sanaa takatifu pamoja na uchungaji. Kama
inawezekana, kamati hiyo isaidiwe na aina ya taasisi ya kichungaji ya
Liturujia yenye wataalamu katika uwanja huo, bila kuwatenga walei pale
inapotakiwa. Itakuwa ni wajibu wa kamati yenyewe, chini ya uongozi wa
Mabaraza ya Maaskofu, kama ilivyoelezwa hapo juu, kuratibu kazi ya
kichungaji mintarafu Liturujia katika sehemu yake iliyokabidhiwa, na pia
kuhimiza utafiti na majaribio yanayotakiwa kila panapokuwa na suala la
kupeleka kwa Baba Mtakatifu.
Kamati ya Liturujia ya jimbo
45. Vilevile katika kila jimbo iundwe kamati ya Liturujia kwa
lengo la kuhimiza, chini ya uongozi wa Askofu, utume wa kiliturujia.
Ikiwa inafaa, majimbo kadhaa yaunde kamati moja ili kuhimiza Liturujia
kwa makubaliano ya pamoja.
Kamati nyinginezo
46. Licha ya kamati ya Liturujia, kadiri iwezekanavyo, katika kila
jimbo iundwe pia kamati ya muziki na ya sanaa takatifu.
Kamati hizo tatu lazima zishirikiane katika kazi zao, na, ionekanapo kuwa
inafaa, ziunganike na kuunda kamati moja.
Sura ya Pili
FUMBO TAKATIFU LA EKARISTI
Misa na fumbo la Pasaka
47. Mwokozi wetu, katika Karamu ya mwisho, usiku alipotolewa, aliweka
sadaka ya Ekaristi ya Mwili wake na Damu yake. Alifanya hivyo ili kuendeleza
Sadaka ya Msalaba siku zote mpaka atakaporudi, kusudi amwachie Bibiarusi
mpendwa, yaani Kanisa, ukumbusho wa kifo chake na ufufuko wake: sakramenti
ya utakatifu (sacramentum pietatis), ishara ya umoja, kifungo cha
mapendo[36], karamu ya Pasaka
“ambamo Kristo huliwa, na roho hujazwa neema, na hutolewa amana ya uzima wa
milele”[37].
Kushiriki kiutendaji kwa waamini katika Misa
48. Kwa sababu hiyo, Kanisa anajibidisha kwa namna nyingi kusudi
waamini wasihudhurie fumbo hilo la imani kama wageni au watazamaji bubu,
bali waishiriki ibada takatifu kwa akili, kwa moyo na kwa matendo, wakielewa
vizuri fumbo hilo kwa njia ya matendo ya kiliturujia na sala. Waamini
waelimishwe katika Neno la Mungu; walishwe katika karamu ya Mwili wa Bwana;
wamtolee Mungu shukrani; wakitolea hostia isiyo na doa, siyo kwa mikono ya
padre tu, bali pia pamoja naye, wajifunze kujitolea wenyewe. Tena, siku kwa
siku, kwa njia ya Kristo mshenga, wakamilishwe katika umoja na Mungu na kati
yao[38], ili hatimaye Mungu awe
yote katika wote.
49. Kwa hiyo, ili sadaka ya Misa ilete manufaa kamili ya kichungaji pia
kwa njia ya umbo la ibada, Mtaguso Mkuu unaagiza yafuatayo kwa ajili ya Misa
ziadhimishwazo pamoja na waamini, hasa Dominika na Sikukuu.
Marekebisho ya kanuni ya Misa
50. Kanuni ya ibada ya Misa itengenezwe upya ili kiini halisi cha
kila sehemu ya ibada na uhusiano kati ya sehemu mbalimbali vionekane wazi
zaidi, na kuwawezesha waamini kushiriki kwa moyo na kwa matendo.
Kwa sababu hiyo madhehebu za ibada zirahisishwe, lakini kiini chake
kihifadhiwe; yaachwe mambo yale ambayo yalifanyika maradufu na yale
yaliyoongezwa bila umuhimu, kadiri nyakati zilivyopita; na mengine
yaliyoachwa bila haki yaingizwe tena, kadiri ya kanuni ya kale ya Mababa
watakatifu, kadiri itakavyoonekana kufaa au kuwa lazima.
Masomo ya Biblia katika Misa yaongezeke
51. Ili meza ya Neno la Mungu iandaliwe kwa wingi zaidi kwa ajili ya
waamini, hazina za Biblia zizidi kufunguliwa, kusudi katika muda wa miaka
kadhaa ya kuagizwa waamini wasomewe sehemu kubwa zaidi ya Maandiko
Matakatifu.
Homilia
52. Inatiliwa sana maanani homilia, kama sehemu ya Liturujia yenyewe;
kwani, kwa njia yake, katika mwaka wa kiliturujia, mafumbo ya imani na
miongozo ya maisha ya kikristo vinafafanuliwa kutoka Maandiko Matakatifu.
Katika Misa ziadhimishwazo pamoja na waamini siku ya Dominika na Sikukuu
zilizoamriwa, homilia isiachwe isipokuwa kwa sababu nzito.
Sala ya waamini
53. “Sala za pamoja” au “sala za waamini” ziingizwe tena baada ya Injili
na homilia, hasa Dominika na Sikukuu zilizoamriwa, kusudi, kwa ushirikiano
na waamini, yatolewe maombi kwa ajili ya Kanisa takatifu, wale
wanaotuongoza, wanaosongwa na mahitaji mbalimbali, kwa ajili ya watu wote na
ukombozi wa ulimwengu mzima[39].
Matumizi ya kilatini na lugha ya mahali katika Misa
54. Katika Misa zinazoadhimishwa pamoja na waamini, matumizi ya
lugha ya nchi inayohusika yaruhusiwe kwa jinsi ifaavyo, hasa katika masomo
na “sala za waamini”, na pia katika sehemu ziwahusuzo waamini, kufuatana na
mazingira ya kila nchi, kadiri ya ibara 36 ya hati hii.
Lakini bidii ifanyike ili waamini waweze kusali na kuimba pamoja
sehemu za ibada ya Misa ziwahusuzo wao pia katika lugha ya kilatini.
Aidha, ikionekana kwamba inafaa katika nchi nyingine kutumia zaidi lugha
ya nchi ile katika Misa, yafuatwe maagizo yaliyotolewa katika ibara 40 ya
hati hii.
Komunyo katika maumbo yote mawili
55. Njia kamilifu zaidi ya kushiriki Misa inakazwa sana: nayo ni
pale waamini wanapopokea Mwili wa Bwana Yesu, baada ya komunyo ya Padre,
kutoka katika sadaka ileile.
Bila kupingana na maagizo ya kidogma ya Mtaguso Mkuu wa Trento[40],
inaruhusiwa komunyo katika maumbo mawili kwa makleri na watawa, na pia
walei, katika nafasi zinazopangwa na Baba Mtakatifu na kufuatana na maoni ya
Askofu, kama vile wanaopewa Daraja takatifu, katika Misa ya kupewa Daraja;
wanaoweka nadhiri za kitawa, katika Misa ya kuweka nadhiri; na wanaobatizwa
(neophytis), katika Misa ya Ubatizo wao.
Umoja wa Misa
56. Ibada ya Misa ina sehemu mbili, yaani Liturujia ya Neno na Liturujia
ya Ekaristi; hizo zote zimeunganika sana kati yake kiasi kwamba zinafanya
ibada moja tu. Kwa hiyo Mtaguso Mkuu unawasihi kwa dhati wachungaji wa roho
wawaelimishe kwa makini waamini wao, katika katekesi, ili washiriki Misa
nzima, hasa siku ya Dominika na Sikukuu zilizoamriwa.
Konselebrasio
57. § 1. Misa ya kushirikiana mapadre wengi pamoja, au
‘Konselebrasio’, ambayo huonyesha vizuri umoja wa upadre, imebaki mpaka leo
katika desturi ya Kanisa la Mashariki na pia la Magharibi. Kwa sababu hiyo
Mtaguso Mkuu umependa kutoa kibali chake kwa konselebrasio katika nafasi
zifuatazo:
1° a) Siku ya Alhamisi Kuu ya Karamu ya Mwisho, katika Misa ya
Krisma na pia katika Misa ya jioni;
b) katika Misa wakati wa Mitaguso, mikutano ya Maaskofu na Sinodi;
c) katika Misa ya kumbariki Abate.
2° Aidha, kwa idhini ya Mkuu wa mahali anayehusika, ambaye tu
anaweza kuamua kuhusu kufaa kwa konselebrasio, [basi idhini inatolewa kwa
nafasi hizi]:
a) katika Misa “ya shirikani” (conventualem) na katika Misa
kubwa makanisani, ikiwa manufaa ya waamini hayahitaji mapadre wote waliopo
waadhimishe Misa kila mmoja peke yake;
b) katika Misa wakati wa mikutano mbalimbali ya Mapadre wa jimbo
na pia wa mashirika.
§ 2. 1° Ni juu ya Askofu kupanga utaratibu wa konselebrasio katika
jimbo.
2° Lakini kila padre anaweza kuadhimisha Misa bila mapadre
wengine, ila si wakati uleule na mahali palepale [konselebrasio
inapofanyika]; wala Alhamisi Kuu.
58. Ibada mpya ya konselebrasio itungwe na kuingizwa katika Pontifikale
na katika Misale ya Kiroma.
Sura ya Tatu
SAKRAMENTI NYINGINE NA VISAKRAMENTI
Maana ya Sakramenti
59. Sakramenti zimewekwa ili kuwatakatifuza wanadamu, kuujenga Mwili wa
Kristo, na mwishowe kumtolea Mungu ibada. Kwa kuwa ni ishara
zinazowafundisha waamini, kwa upande moja zinadai imani, na kwa upande
mwingine zinalisha imani yenyewe kwa maneno na matendo ya ibada; tena
zinaimarisha na kuidhihirisha imani hiyo. Ndiyo sababu zinaitwa “Sakramenti
za imani”. Ni kweli kwamba zinawapatia waamini neema, lakini pia maadhimisho
yake yanawaandaa kikamilifu ili neema yenyewe wanayoipokea itoe matunda; pia
yawawezeshe kumheshimu Mungu jinsi ipasavyo na kufanya matendo ya huruma.
Kwa sababu hiyo ni muhimu sana waamini wazielewe kwa urahisi
ishara za Sakramenti, nao wazikaribie kwa makini sana Sakramenti zile
zilizowekwa ili kuyalisha maisha ya kikristo. Visakramenti
60. Mama Kanisa takatifu aliweka pia visakramenti, ambavyo ni
alama takatifu ambazo kwazo, kutokana na kufanana kwa namna fulani na
Sakramenti, vinaashiria matunda, hasa ya kiroho, ambayo hupatikana kwa
maombi ya Kanisa. Kwa njia ya visakramenti hivi watu hutayarishwa kupokea
tunda la msingi la Sakramenti, na mazingira mbalimbali ya maisha hutakaswa.
61. Hivyo liturujia ya Sakramenti na Visakramenti inawawezesha waamini
wenye moyo mnyofu kuyatakatifuza matukio karibu yote ya maisha kwa njia ya
ile neema ya kimungu inayobubujika toka fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo
na ufufuko wa Kristo. Kutokana na fumbo hilo Sakramenti na Visakramenti
hupata nguvu yao; na kwa msaada wa nguvu hiyo matumizi manyofu ya mambo ya
kidunia yaweza kuelekezwa katika kumtakatifuza binadamu na kumsifu Mungu.
Umuhimu wa marekebisho ya adhimisho ya Sakramenti
62. Katika mwenendo wa nyakati katika ibada ya Sakramenti na Visakramenti
yameingizwa mambo kadhaa yaletayo ugumu katika kuelewa maumbile na lengo la
ibada hizo. Kwa hiyo marekebisho, ili kulinganisha ibada na matakwa ya siku
hizi, ni ya lazima. Kwa kusudi hilo Mtaguso unaagiza yafuatayo.
Lugha katika ibada
63. Mara nyingi katika kutoa Sakramenti na Visakramenti, kwa manufaa ya
waamini, lugha ya nchi husika inaweza kutumiwa katika nafasi kubwa zaidi
kadiri ya mwongozo ufuatao:
a) Katika utoaji wa Sakramenti na Visakramenti inawezekana kutumia
lugha ya nchi husika kufuatana na ibara 36.
b) Kufuatana na toleo jipya la Rituale ya Kiroma, Mabaraza ya
Maaskofu ya kila mahali, kama ilivyoelezwa katika ibara 22 § 2 ya hati hii,
yatayarishe upesi iwezekanavyo Rituale faridi zinazolinganishwa na mahitaji
ya kila nchi, pia kuhusu lugha; kisha Rituale hizo zitatumika katika nchi
zinazohusika baada ya kuchunguzwa na Kiti cha Kitume. Katika kutunga Rituale
hizo, au mikusanyo maalum mingine ya ibada, yasiachwe maelezo yaliyomo kabla
ya kila madhehebu katika Rituale ya Kiroma, yale yenye tabia ya kichungaji
au ya maelekezo (rubricis), na yale yenye umuhimu wa pekee wa kijamii
pia.
Ukatekumeni
64. Uwekwe tena ukatekumeni kwa watu wazima, uliogawanywa katika hatua
nyingi, wa kutekeleza kadiri ya mwongozo wa Mkuu wa mahali. Hivyo, muda wa
ukatekumeni, uliowekwa kwa ajili ya mafundisho yafaayo, uweze kutakatifuzwa
kwa njia ya ibada takatifu zitakazoadhimishwa kwa nyakati mbalimbali.
Marekebisho ya adhimisho la Ubatizo
65. Katika nchi za misioni iruhusiwe kuyapokea, sambamba na mambo
yote ya mapokeo ya kikristo, pia yale ya unyago ulivyo katika mila za kila
taifa kwa kiasi kiwezekanacho kufungamana na ibada ya kikristo, kadiri ya
ibara 37-40 za hati hii.
66. Ibada zote mbili za Ubatizo wa wakubwa zitengenezwe, ile ya
kawaida na ile ya Ubatizo wa sherehe zaidi, kwa kuzingatia kuwekwa tena kwa
ukatekumeni. Katika Misale ya Kiroma Misa maalum “katika utoaji wa Ubatizo”
iingizwe.
67. Ibada ya Ubatizo wa watoto itengenezwe upya, nayo izingatie
hali halisi ya watoto. Katika ibada hiyo jukumu na wajibu wa wazazi na
wasimamizi vitiliwe mkazo zaidi.
68. Katika ibada ya Ubatizo iwepo pia mibadala fulani ya
utaratibu, ya kutumia wakati wanaobatizwa ni wengi, kadiri ya mwongozo wa
Mkuu wa mahali. Itungwe pia ibada iliyo fupi zaidi ambayo wanaweza kutumia,
hasa katika nchi za misioni, makatekista au pia, katika hatari ya kufa,
waamini, ikiwa anakosekana Padre au Shemasi.
69. Badala ya “Ibada ya
kukamilisha yaliyoachwa katika Ubatizo wa watoto”, itungwe ibada mpya ambayo
nayo ionyeshe waziwazi zaidi kwamba mtoto, aliyekwisha kubatizwa kwa ibada fupi,
ameshapokelewa katika Kanisa.
Itungwe pia ibada maalum kwa wale ambao wameshabatizwa kwa halali na baadaye
wanaliongokea Kanisa Katoliki. Katika ibada hiyo kusisitizwe kupokelewa kwao
katika ushirika wa Kanisa.
70. Nje ya kipindi cha Pasaka, maji ya Ubatizo yaweza kubarikiwa katika
ibada yenyewe ya Ubatizo kwa formula fupi maalum iliyoidhinishwa.
Marekebisho ya adhimisho la Kipaimara
71. Ibada ya Kipaimara itengenezwe upya ili ionyeshe vizuri zaidi
uhusiano wa ndani wa Sakramenti hii na zingine za kumwingiza mtu katika
ukristo. Kwa hiyo, kurudia ahadi za Ubatizo kutangulie kupokea Sakramenti
hii.
Ikiwa inafaa, Sakramenti ya Kipaimara inaweza kutolewa wakati wa Misa.
Kama ibada itaadhimishwa nje ya Misa, itayarishwe formula ya kutumia kama
utangulizi.
Marekebisho ya adhimisho la Kitubio
72. Ibada na formula za Kitubio zitengenezwe upya ili zionyeshe waziwazi
zaidi maumbile na matokeo ya Sakramenti hii.
Sakramenti ya Mpako wa wagonjwa
73. Sakramenti ya “Mpako wa Mwisho”, ambayo inaweza kuitwa vizuri
zaidi “Mpako wa wagonjwa”, si Sakramenti kwa wale tu walio katika hali ya
kuaga dunia. Kwa hiyo, wakati ufaao kwa kuipokea ni ule mwamini aanzapo kuwa
katika hatari ya kufa kwa sababu ya ugonjwa na uzee.
74. Licha ya ibada mbili tofauti, yaani ya Mpako wa wagonjwa na ya
Komunyopamba, itungwe pia utaratibu wenye mfululizo, ambamo Mpako utatolewa
kwa mgonjwa baada ya Kitubio na kabla ya kuipokea Komunyopamba.
75. Idadi ya mipako irekebishwe, kadiri inavyoonekana inafaa; pia sala za
ibada ya Mpako wa wagonjwa zirekebishwe ili zilingane na hali tofauti ya
kila mgonjwa anayepewa Sakramenti.
Marekebisho ya adhimisho la Daraja
76. Ibada na matini yanayohusu Sakramenti ya Daraja yarekebishwe.
Mawaidha (Allocutiones) ya Askofu mwanzoni mwa kila ibada ya Daraja
yaweza kutolewa katika lugha ya nchi.
Katika ibada ya kumweka wakfu Askofu, Maaskofu wote waliopo waweza
kumwekea mikono yao juu yake.
Marekebisho ya adhimisho la Ndoa
77. Ibada ya Sakramenti ya Ndoa, iliyomo katika Rituale ya Kiroma,
irekebishwe na itajirishwe zaidi ili neema ya Sakramenti iashirishwe
waziwazi zaidi, na pia majukumu ya wafunga ndoa yakazwe sana.
Katika adhimisho la Sakramenti ya Ndoa, “kama katika mila na
desturi za taifa zipo mila na sherehe nyingine za kufaa, Mtaguso unatamani
kabisa hizo zihifadhiwe”[41].
Aidha, Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali, kama ilivyoelezwa
katika ibara 22 § 2 ya hati hii, yanaweza kutayarisha kwa mujibu wa ibara
63, ibada maalum, nayo ilingane na mila za taifa; lakini kwa sharti itunzwe
sheria ya kwamba Padre anayesimamia Ndoa aombe na kupokea ukubaliano wa
wafunga ndoa.
78. Kawaida Ndoa iadhimishwe wakati wa Misa, baada ya Injili na
homilia, kabla ya “sala za waamini”. Sala ya kumwombea bibiarusi irekebishwe
ili iwaeleze vizuri wanaarusi wote wawili wajibu wao wa kuwa waaminifu wao
kwa wao; lugha ya nchi inaweza kutumika katika sala hii.
Lakini, ikiwa Sakramenti ya Ndoa inaadhimishwa bila Misa, mwanzoni mwa
ibada usomwe waraka na Injili ya Misa ya Ndoa; vilevile kila mara baraka ya
wanandoa itolewe.
Marekebisho ya Visakramenti
79. Visakramenti virekebishwe, kadiri ya kanuni ya msingi kwamba
waamini wawezeshwe kushiriki kwa ufahamu, matendo, na kwa urahisi. Tena
vilinganishwe na mahitaji ya siku hizi. Katika kurekebisha miongozo yao,
kadiri ya ibara 63, kama ikifaa, yawezekana kuongeza pia Visakramenti vipya.
Baraka za pekee ziwe chache sana, na kwa ajili ya Maaskofu na
Wakuu [wa mahali] tu.
Jitihada zifanyike ili Visakramenti vingine vitolewe na walei wenye uwezo
na sifa zinazotakiwa, walau katika nafasi za pekee na kwa uamuzi wa Mkuu
anayehusika.
Nadhiri za kitawa
80. Ibada ya kuweka wakfu mabikira iliyomo katika Pontifikale ya Kiroma
irekebishwe.
Itungwe pia ibada ya kuweka nadhiri, au uprofesi (professionis religiosae),
na ya kurejea nadhiri (renovationis votorum), yenye kuonyesha kwa
wazi zaidi umoja, usahili na heshima. Nayo itumiwe na wale wanaoweka nadhiri
za maisha au za muda wakati wa Misa, isipokuwa kwa nafasi ya pekee.
Ni vema nadhiri ziwekwe wakati wa Misa.
Marekebisho ya ibada ya Mazishi
81. Ibada ya Mazishi ionyeshe kinaganaga zaidi tabia ya kipasaka
ya kifo cha kikristo. Pia mintarafu rangi ya kiliturujia hiyo, na ilingane
zaidi na mazingira na mapokeo ya kila kanda.
82. Irekebishwe pia ibada ya Mazishi ya watoto na itungwe Misa maalum kwa
ajili ya hiyo.
Sura ya Nne
LITURUJIA YA VIPINDI
Liturujia ya Vipindi ni tendo la Kristo na la Kanisa
83. Kuhani Mkuu wa Agano Jipya na la milele, Yesu Kristo, kwa
kutwaa maumbile ya kibinadamu, ameingiza katika ugeni huu wa hapa duniani
wimbo ule unaoimbwa daima katika makao ya mbinguni. Yeye anaunganisha naye
jumuiya ya wanadamu wote mpaka washiriki naye katika kuuinua wimbo huo wa
kimungu na wa sifa.
Kwa kweli, Yesu huendeleza tendo hili la kikuhani kwa njia ya
Kanisa lake, ambalo humsifu Bwana Mungu bila kukoma na kumwomba kwa ajili ya
ukombozi wa ulimwengu mzima, si kwa njia ya kuadhimisha Ekaristi tu, bali
pia kwa namna nyingine, na hasa kwa kusali “Kazi ya Mungu” (Officio
divino), yaani Liturujia ya Vipindi.
84. Liturujia ya Vipindi, kadiri ya mapokeo ya zamani ya kikristo,
imewekwa ili mfululizo wa mchana na usiku utakatifuzwe kwa njia ya sifa ya
Mungu. Wakati wenye kuadhimisha wimbo ule wa sifa na wa ajabu ni mapadre, au
wengine waliowekwa kwa ajili hiyo na sheria ya Kanisa, au pia waamini
wanaosali pamoja na Padre kwa jinsi inavyokubalika, hapo kweli ni sauti ya
Bibiarusi mwenyewe anayeongea na Bwanaarusi. Kwa kweli ni sala ya Kristo
ambaye, pamoja na Mwili wake, humwomba Baba.
85. Wote wanaotimiza tendo hilo wanatekeleza wajibu wa Kanisa, na pia
wanashiriki heshima kubwa sana ya Bibiarusi wa Kristo kwa sababu,
wanapomsifu Mungu, hukaa mbele ya kiti cha enzi cha Mungu kwa niaba ya Mama
Kanisa.
Umuhimu wa Liturujia ya Vipindi katika uchungaji
86. Mapadre wanaotekeleza huduma takatifu ya kichungaji watasali
masifu ya Vipindi kwa juhudi kubwa zaidi kiasi ambacho kitawasukuma kushika
onyo la Mtume Paulo: “Ombeni bila kukoma” (1The 5:17). Kwa maana Bwana peke
yake tu anaweza kuleta na kukuza matunda ya kazi wanayofanya, yeye
aliyesema: “Bila mimi hamwezi kufanya lolote” (Yn 15:5). Kwa sababu hiyo
Mitume, walipowawekea mikono mashemasi, walisema: “Na sisi tutadumu katika
kuomba na kulihudumia lile Neno” (Mdo 6:4).
87. Ili mapadre na waamini wengine waweze kusali vizuri na kikamilifu
zaidi Liturujia ya Vipindi katika nafasi mbalimbali, Mtaguso Mkuu,
ukiendeleza marekebisho yaliyoanzishwa na Kiti cha Kitume, unapenda kuagiza
yafuatayo kuhusu Liturujia ya Vipindi, kufuatana na Riti ya Kiroma.
Marekebisho ya utaratibu wa Liturujia ya Vipindi
88. Kwa vile lengo la Liturujia ya Vipindi ni kutakatifuza siku nzima,
utaratibu wa kimapokeo wa vipindi urekebishwe ili Sala za Vipindi zifanywe
kwa wakati wake, kadiri inavyowezekana. Vilevile hali ya maisha ya siku
hizi, na hasa ya wale wanaojibidisha katika matendo ya kitume, iangaliwe.
Mwongozo kwa marekebisho ya Liturujia ya Vipindi
89. Kwa hiyo, katika kurekebisha Liturujia ya Vipindi, ufuatwe
mwongozo huu:
a) Masifu ya Asubuhi (Laudes), kama sala ya asubuhi, na
Masifu ya Jioni (Vesperae), kama sala ya jioni, kadiri ya mapokeo
yenye heshima ya Kanisa lote ni bawaba maradufu ya Liturujia ya Vipindi ya
kila siku. Hivyo yatazamwe kama Vipindi muhimu zaidi na yaadhimishwe
kufuatana na umuhimu wake;
b) Utaratibu wa Sala ya Usiku, au Kompleto (Completorium),
urekebishwe ili ulingane inavyofaa na mwisho wa siku;
c) Sala ya Kipindi kiitwacho Mikesha (Matutinum), ingawa
kinaendelea kuwa kipindi cha sala kwa ajili ya usiku kisaliwapo pamoja
katika kwaya (in choro), irekebishwe ili iweze kutumika wakati wowote
wa siku, tena iwe na zaburi chache na masomo marefu zaidi;
d) Kipindi cha Kwanza (Prima) kifutwe;
e) Katika kwaya Vipindi vidogo vya Kabla ya Adhuhuri au Tersia (Tertia),
Adhuhuri au Sesta (Sexta) na Baada ya Adhuhuri au Nona (Nona)
vihifadhiwe. Nje ya kwaya inaruhusiwa kuchagua kimoja kati ya hivyo vitatu,
kadiri ya majira ya siku.
Liturujia ya Vipindi ni chemchemi ya uchaji
90. Licha ya hayo, Liturujia ya Vipindi ni sala ya hadhara ya
Kanisa na chemchemi ya uchaji na chakula cha sala ya binafsi. Kwa hiyo,
mapadre na waamini wengine wote wanaoshiriki Liturujia ya Vipindi tunawasihi
ili, katika kusali, akili na sauti zao viungane; kwa kufikia lengo hilo
wahusika wajipatie ufahamu wa kina zaidi wa Liturujia na wa Biblia hasa
kuhusu zaburi.
Katika kufanya marekebisho hayo, hazina yenye heshima na ya zamani
iliyomo katika Breviari ya Kiroma irekebishwe ili waliokabidhiwa waweze
kuitumia zaidi na kwa urahisi.
Mgawanyo wa Zaburi
91. Ili utaratibu wa Vipindi uliopendekezwa katika ibara 89 uweze
kutekelezwa kweli, zaburi zigawanywe sio tena katika juma moja, bali katika
muda mrefu zaidi.
Kazi hii ya kurekebisha mgawanyo wa zaburi, iliyoanzishwa vizuri,
imalizwe kwa haraka, bila kusahau Kilatini kinachotumiwa na wakristo, na
matumizi yake ya kiliturujia katika nyimbo. Vivyo hivyo mapokeo yote ya
Kanisa la Kiroma yasisahauliwe.
Utaratibu wa masomo
92. Kuhusu masomo, mwongozo ufuatao uzingatiwe:
a) Usomaji wa Maandiko Matakatifu upangwe ili hazina za Neno la
Mungu zipatikane katika wingi wake kwa urahisi zaidi;
b) Masomo yachukuliwayo kutoka maandiko ya Mababa, Waalimu na
Waandishi wa Kanisa, yachaguliwe vizuri zaidi;
c) Masimulizi ya mateso ya watakatifu, yaani maisha yao, yarudishwe
katika ukweli wa kihistoria.
Marekebisho ya tenzi
93. Pia tenzi zirudishwe katika mtindo wao wa asili, kwa kiasi kifaacho;
na yale yaliyo katika hali ya visasili (mythologiam) au yasiyofaa kwa
uchaji wa Mungu yaondolewe au yabadilishwe. Aidha, zichukuliwe tena tenzi
nyingine, kadiri ifaavyo, zilizomo katika mikusanyo mbalimbali.
Wakati wa kusali kila Kipindi
94. Ili kutakatifuza kweli siku na kusali Vipindi vyenyewe kwa matunda ya
kiroho, Sala za Vipindi zifanywe kulingana na majira yake, yaani sambamba na
wakati halisi wa kila Kipindi.
Ulazima wa Liturujia ya Vipindi
95. Jumuiya zenye sharti la kusali pamoja zinatakiwa kusali katika
kwaya Liturujia ya Vipindi kila siku, zaidi ya Misa ya shirikani; na hasa:
a) Jumuiya za Wakanoniki, Mashirika ya Wamonaki wa kike na wa
kiume na wale watawa wote (Regularium) wanaotakiwa kusali pamoja
katika kwaya, kadiri ya sheria na katiba zao, wanapaswa kusali Vipindi
vyote.
b) Kapitulo za Makanisa Makuu na za Kolejata zinapaswa kusali
sehemu zile za Ofisyo zinazoamriwa katika sheria za kawaida au za pekee.
c) Wanashirika wote waliotajwa juu, ambao wamepewa Daraja kuu (Ordinibus
maioribus) au wameweka nadhiri za maisha, isipokuwa ndugu watawa walei (conversis),
wanapaswa kusali peke yao Vipindi vile wasivyosali katika kwaya.
96. Makleri wasiopasika kusali katika kwaya, kama wamepewa Daraja
kuu, wanapaswa kusali sala zote za Vipindi kila siku peke yao au kwa pamoja,
kadiri ya ibara 89.
97. Mwongozo wa kushiriki ibada nyingine kama mibadala ya kufaa ya
Liturujia ya Vipindi uratibiwe.
Katika nafasi za pekee na kwa sababu halali, Wakuu wa mahali
wanaweza kuwaruhusu wale walio chini yao kutofungwa na ulazima wa kusali
Liturujia ya Vipindi, ama kufanya ibada nyingine badala yake.
98. Wanashirika wa taasisi yoyote ya kitawa ambao kwa mujibu wa
Katiba husali sehemu kadhaa za Liturujia ya Vipindi, huonyesha sala ya
hadhara ya Kanisa.
Vilevile wanaonyesha sala ya hadhara ya Kanisa kama, kwa mujibu wa
Katiba, wakisali “Ofisyo fupi”, mradi zimetungwa kulingana na mpango wa
Liturujia ya Vipindi ya kawaida na kuidhinishwa inavyotakiwa.
Kusali pamoja Liturujia ya Vipindi99. Liturujia ya Vipindi ni
sauti ya Kanisa, yaani ya Mwili wote wa fumbo unaomsifu Mungu hadharani. Kwa
hiyo, Mtaguso unawasihi makleri wasiopasika kusali katika kwaya na hasa mapadre
wanaoishi au kukutana pamoja, wasali pamoja walau sehemu kadhaa za Liturujia ya
Vipindi.
Aidha, wale wote wanaosali Liturujia ya Vipindi kwa pamoja au katika kwaya,
watimize, kikamilifu iwezekanavyo, wajibu waliokabidhiwa kwa uchaji wa
rohoni na pia kwa vitendo vya nje.
Pia ni vema, kama inawezekana, Liturujia ya Vipindi katika kwaya au kwa
pamoja iimbwe.
Kushiriki kwa waamini katika Liturujia ya Vipindi
100. Wachungaji wa roho wajitahidi kwamba Vipindi vikuu vya sala, hasa
Masifu ya Jioni (Vesperae), viadhimishwe kanisani pamoja na waamini
siku ya Dominika na Sikukuu kubwa zaidi. Walei pia wanahimizwa wasali
Liturujia ya Vipindi au pamoja na mapadre, au wakiungana kati yao, au kila
mmoja peke yake.
Lugha katika Liturujia ya Vipindi
101. § 1. Kadiri ya mapokeo ya zamani ya riti ya kilatini, wakleri
wanapaswa kuhifadhi lugha ya kilatini katika Liturujia ya Vipindi. Lakini
Mkuu wao ana uwezo wa kuruhusu matumizi ya tafsiri katika lugha ya nchi,
iliyoandaliwa kadiri ya ibara 36, kwa wale wakleri mmoja mmoja (singulis
pro casibus) ambao kwao matumizi ya lugha ya kilatini ni kizuio kikubwa
kwa kusali Liturujia ya Vipindi ipasavyo.
§ 2. Kwa wamonaki wa kike (monialibus) na wanajumuiya wa
mashirika ya kitawa, au wasio wakleri, au wa kike, Mkuu wao anayehusika
anaweza kuruhusu matumizi ya lugha ya nchi katika Liturujia ya Vipindi, hata
ikiadhimishwa katika kwaya, lakini tafsiri iidhinishwe.
§ 3. Kila mkleri anayepaswa kusali Liturujia ya Vipindi, akisali katika
lugha ya nchi pamoja na waamini, au pamoja na wale waliotajwa katika § 2,
anatimiza wajibu wake. Hata hivyo, tafsiri inayotumika iwe imeidhinishwa.
Sura ya Tano
MWAKA WA LITURUJIA
Maana ya Mwaka wa Liturujia102. Mama Kanisa takatifu huchukulia
wajibu wake kuadhimisha kwa kumbukumbu takatifu kazi ya ukombozi ya Bwanaarusi
wake aliye Mungu, katika siku zilizopangwa katika mwenendo wa mwaka mzima. Kila
juma Kanisa, katika siku aliyoiita “Dominika”, yaani “Siku ya Bwana”,
anaadhimisha kumbukumbu ya ufufuko wa Bwana. Kwa namna ya pekee anauadhimisha
ufufuko huo pamoja na mateso yake yenye heri mara moja kwa mwaka katika Sikukuu
ya Pasaka, iliyo kubwa kuliko Sherehe zote.
Katika mzunguko wa mwaka mzima, [Mama Kanisa] analikunjua fumbo la Kristo,
tangu umwilisho na kuzaliwa, hadi kupaa mbinguni, mpaka siku ya Pentekoste
na kungojea kwa tumaini lenye heri kurudi kwake Bwana.
Anapokumbuka namna hii mafumbo ya ukombozi, Kanisa huwafungulia
waamini utajiri wa uweza na mastahili ya Bwana wake. Kwa njia hii, uwepo wa
mafumbo haya unakuwapo kwa nyakati zote, ili kutoka humo waamini waweze
kuchota na kujazwa neema ya wokovu.
103. Kwa kuadhimisha katika mzunguko huo wa [kila] mwaka mafumbo ya
Kristo, Kanisa humheshimu kwa upendo wa pekee Maria mwenye heri, Mama wa
Mungu, ambaye ameunganika na Mwana wake kwa namna isiyoweza kutengwa, katika
kazi ya wokovu. Tena, ndani ya Maria, Kanisa hustahi na kutukuza tunda bora
kuliko yote la ukombozi, na pia hutazama kwa furaha, kama katika mfano usio
na doa, yale anayoyatamani na kuyatumaini kwa ajili yake lote.
Kumbukumbu za Mashahidi na za Watakatifu
104. Kanisa limeingiza pia katika mwaka wa Liturujia kumbukumbu za
Mashahidi na za Watakatifu wengine ambao, baada ya kufikia ukamilifu
kutokana na neema ya Mungu iliyo ya namna nyingi, na wakishapata ukombozi wa
milete, wanaimba sifa kamili ya Mungu kule mbinguni na kutuombea.
Kwa kuadhimisha siku za kuzaliwa [mbinguni] kwa Watakatifu Kanisa
latangaza fumbo la Pasaka lionekanalo katika Watakatifu walioteswa pamoja na
Kristo na kutukuzwa pamoja naye, na lawaonyesha waamini mifano yao
inayowavutia wote kwa Baba kwa njia ya Kristo. Pia linawaombea fadhili za
Mungu kwa njia ya mastahili yao.
105. Kanisa, katika vipindi mbalimbali vya mwaka na kadiri ya
utaratibu wa kimapokeo, linatimiza wajibu wake wa kuwakomaza waamini kwa
njia ya matendo ya kiroho na kimwili, mafundisho, sala pamoja na matendo ya
toba na ya huruma.
Kwa sababu hiyo Mtaguso Mkuu kwa dhati unaamua yafuatayo.
Umuhimu wa Dominika
106. Kadiri ya mapokeo ya Mitume, yanayopata asili yake katika siku ya
ufufuko wa Kristo, Kanisa huadhimisha fumbo la Pasaka kila siku ya nane,
katika siku ile iitwayo kwa haki kabisa Siku ya Bwana au Dominika. Katika
siku hii waamini wanapaswa kujumuika pamoja ili, wanaposikiliza Neno la
Mungu na kushiriki Ekaristi, wafanye ukumbusho wa mateso, ufufuko na utukufu
wa Bwana Yesu. Na pia watoe shukrani kwa Mungu “aliyewazaa upya katika
tumaini lenye uhai kwa njia ya ufufuko wa Yesu Kristo katika wafu” (1Pet
1:3). Kwa hiyo, siku ya Dominika ni Sikukuu ya kwanza ambayo ni lazima
ielezwe vizuri na kuingizwa, kwa kadiri inavyowezekana, katika maisha ya
kidini ya wakristo, ili iweze kuwa pia siku ya furaha na ya kuacha kazi.
Sherehe nyingine zisitiliwe mkazo sana, isipokuwa zile zenye umuhimu zaidi,
kwa sababu siku ya Dominika ni msingi na kiini cha mwaka mzima wa Liturujia.
Marekebisho ya Mwaka wa Liturujia
107. Mwaka wa Liturujia urekebishwe ili zihifadhiwe au ziingizwe
tena desturi na taratibu za vipindi vitakatifu kadiri ya hali ya nyakati
zetu. Pia maana yao ya asili ihifadhiwe ili kulisha ipasavyo uchaji wa
waamini katika kuadhimisha mafumbo ya ukombozi wa Kristo, na hasa fumbo la
Pasaka. Aidha, ikiwa ni lazima, marekebisho yafanywe kulingana na hali ya
kila mahali kadiri ya ibara 39 na 40.
108. Roho za waamini zielekezwe kwanza kabisa kwenye sikukuu za Bwana,
ambamo, katika mwaka, yanaadhimishwa mafumbo ya wokovu. Kwa hiyo Vipindi vya
Mwaka (Proprium de Tempore) vipewe umuhimu wake kuliko sikukuu za
Watakatifu, ili mfululizo mzima wa mafumbo ya wokovu uadhimishwe ipasavyo.
Kwaresima
109. Maana mbili zinazofanya kipekee Kipindi cha Kwaresima,
ukumbusho wa Ubatizo au matayarisho yake, na toba, zitiliwe mkazo wa pekee
katika Liturujia na katekesi ya Liturujia. Nazo zinasaidia kuwaandaa waamini
kuadhimisha fumbo la Pasaka, wakisikiliza mara nyingi zaidi Neno la Mungu na
kujibidisha katika kusali. Kwa hiyo:
a) Mambo yote yadokezayo Ubatizo yaliyomo katika Liturujia ya
Kwaresima yapewe nafasi kubwa zaidi, na pia, kama inafaa, yaingizwe tena
mengine yatokanayo na mapokeo ya zamani;
b) Vivyo hivyo ifanywe kuhusu mambo ya toba. Mintarafu katekesi, juhudi
ifanywe ili iweze kuingizwa rohoni mwa waamini, pamoja na matokeo ya kijamii
ya dhambi, maumbile halisi ya toba yenye kuchukia dhambi kwa sababu ni
kumtukana Mungu; nafasi ya Kanisa katika tendo la toba isisahauliwe kamwe,
na pia sala kwa ajili ya wakosefu ihimizwe.
110. Toba ya wakati wa Kwaresima isiwe ni tendo la ndani na la binafsi tu,
bali pia lionekanalo kwa nje na katika maisha ya jamii. Matendo ya toba na
kujinyima, kadiri ya uwezekano wa nyakati zetu na mahali mbalimbali, na pia
kadiri ya hali ya waamini, yasisitizwe na kuhimizwa na wale wenye mamlaka,
kama ilivyoelezwa katika ibara 22.
Lakini tendo la kufunga chakula wakati wa Pasaka litakuwa takatifu, nalo
liadhimishwe popote siku ya Ijumaa ya Mateso na Kifo cha Bwana na kuendelea,
kama inawezekana, siku nzima ya Jumamosi Kuu, ili kufikia furaha na shangwe
ya Dominika ya Ufufuko kwa moyo wazi na ulioinuliwa.
Sherehe za Watakatifu
111. Katika Kanisa, kadiri ya mapokeo, Watakatifu huheshimiwa;
vivyo hivyo masalia yao halisi na picha zao huhifadhiwa kwa heshima. Maana
sherehe za Watakatifu zinatangaza matendo ya ajabu ya Kristo ndani ya
watumishi wake, na pia zinawaonyesha waamini mifano bora ya kuiga.
Ili sikukuu za Watakatifu zisipewe umuhimu zaidi kuliko zile
zinazokumbusha mafumbo ya wokovu, nyingi kati ya sikukuu hizo [za
Watakatifu] ziadhimishwe tu katika Kanisa faridi, au Taifa au Shirika.
Sikukuu zile tu zinazowakumbuka Watakatifu wenye umuhimu kwa wote
ziadhimishwe katika Kanisa zima.
Sura ya Sita
MUZIKI MTAKATIFU
Umuhimu wa muziki wa kiliturujia
112. Mapokeo ya kimuziki ya Kanisa lote ni hazina yenye thamani
isiyopimika, inayozidi aina nyingine ya sanaa, hasa kwa sababu kuimba
kutakatifu, kukiunganika na maneno, ni sehemu ya lazima na ya ndani ya
Liturujia ya sherehe.
Hakika kuimba kutakatifu kumesifiwa katika Maandiko Matakatifu[42]na
pia na Mababa wa Kanisa na Mapapa wa Kanisa la Kiroma, ambao nyakati hizi
kwanzia na Mt. Pius X, wamesisitiza kwa dhati karama na huduma ya kuimba
kutakatifu katika ibada ya Liturujia.
Kwa hiyo, muziki mtakatifu utazidi kuwa mtakatifu pale uunganikapo na tendo
la Liturujia; maana utafanya sala kuwa tamu zaidi na kuonyesha umoja wa
mioyo, pia utaleta heshima zaidi katika maadhimisho matakatifu. Tena Kanisa
linakubali na kuingiza katika ibada kwa Mungu mitindo yote ya sanaa ya
kweli, lakini yenye sifa zinazotakiwa.
Kwa hiyo, Mtaguso Mkuu unahifadhi kanuni na sheria zilizokubalika na za
mapokeo ya Kanisa, na pia unalenga shabaha ya muziki mtakatifu, ambayo ni
utukufu wa Mungu na kutakatifuzwa kwa waamini. Ili kutekeleza kusudi hilo,
Mtaguso Mkuu unaamua yafuatayo.
Liturujia ya Sikukuu
113. Tendo la Liturujia hupata kuwa na heshima zaidi wakati
linapoadhimishwa katika sherehe kwa kuimba, wakiwepo makasisi na kwa
ushirikiano hai wa waamini.
Kuhusu matumizi ya lugha, ibara 36 izingatiwe; juu ya Misa, kama
ilivyoelezwa katika ibara 54; kwa Sakramenti, ifuatwe ibara 63, na mintarafu
Liturujia ya Vipindi, ifanywe kama isemavyo ibara 101.
114. Hazina ya mapokeo ya muziki mtakatifu ihifadhiwe na kukuzwa kwa
uangalifu sana. Shule za Kwaya (Scholae cantorum) zihimizwe, hasa
katika Makanisa Makuu. Aidha, Maaskofu na wachungaji wengine wa roho wafanye
jitihada ili katika kila ibada iadhimishwayo kwa kuimba, waamini wote waweze
kushiriki kikamilifu, kadiri ya ibara 28 na 30.
Uandaaji wa wanamuziki
115. Jitihada kubwa ifanyike ili kuhamasisha elimu na mazoezi ya
muziki katika seminari, katika nyumba za unovisi za mashirika ya kiume na ya
kike, katika nyumba za wanafunzi, kama vile vyuo na shule za kikatoliki; ili
kupata elimu hii, walimu waandaliwe kwa bidii kubwa, kisha watumwe
kufundisha muziki mtakatifu.
Ikiwa inafaa, uundaji wa Taasisi za Juu za muziki mtakatifu
uhimizwe.
Wanamuziki, wanakwaya, na juu ya wote watoto, wapewe elimu halisi ya
kiliturujia.
Nyimbo za kigregoriani na nyinginezo
116. Kanisa anautambua uimbaji wa mtindo wa kigregoriani kuwa ndio ulio
rasmi wa Liturujia ya Kiroma: kwa hiyo, katika matendo ya Liturujia ushike
nafasi ya kwanza, isipokuwa kwa sababu maalum.
Mitindo mingine ya muziki mtakatifu, hasa ile itumiayo sauti nyingi (polyphonia),
isiondolewe katika maadhimisho ya ibada kwa Mungu, lakini ilingane na roho
ya tendo la Liturujia, kadiri ya ibara 30.
117. Toleo halisi (Editio typica) la vitabu vya nyimbo za
kigregoriani lichapwe; tena ni afadhali litayarishwe toleo halisi zaidi
kuliko vitabu vilivyochapwa baada ya matengenezo ya Mt. Pius X.
Licha ya toleo hilo, bora litayarishwe toleo jingine lenye tuni zilizo
rahisi zaidi, la kutumia katika makanisa madogo.
Nyimbo za kidini za mahali
118. Nyimbo za kidini za [wakristo] wenyeji zihimizwe kwa bidii, ili
katika ibada mbalimbali za watu na pia katika matendo ya Liturujia sauti za
waamini ziweze kusikika vizuri, kadiri ya utaratibu na madai ya miongozo.
Muziki ya kiliturujia katika misioni
119. Katika nchi kadha wa kadha, hasa zile za Misioni, yapo
mataifa yenye mapokeo yao ya muziki ambayo yana maana kubwa katika maisha
yao ya kidini na ya kijamii. Muziki huu upewe heshima na nafasi inayofaa
katika kuyaelimisha mataifa hayo kidini, na pia katika kutengeneza ibada kwa
kulingana na tabia yao, kadiri ya ibara 39 na 40.
Kwa hiyo, katika kuwaelimisha wamisionari juu ya muziki, jitihada
ifanyike ili, kadiri inavyowezekana, waweze kuendeleza muziki wa kimapokeo
wa mataifa yanayohusika, katika mashule na katika ibada takatifu.
Organi na ala nyingine za muziki
120. Katika Kanisa la Kiroma, organi ya mianzi ipewe nafasi ya
heshima, kama ala ya kimapokeo ya muziki ambayo kwayo muziki huongeza fahari
ya ajabu kwa ibada za Kanisa, na pia huinua roho za waamini kwa Mungu na kwa
mambo ya mbinguni.
Ala nyingine za muziki pia zinaweza kutumika katika ibada kwa Mungu, kwa
uamuzi na kibali cha Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali, kadiri ya ibara 22
§ 2, 37 na 40. Lakini sharti ziwe za kufaa kwa matumizi matakatifu au
zigeuzwe ili zifae kwa lengo hili. Tena, zilingane na heshima ya hekalu na
zisaidie kujenga [uchaji wa] waamini.
Wajibu wa watunga muziki
121. Watunga muziki, wakisukumwa na roho ya kikristo, wajione kuwa
wameitwa kuustawisha muziki mtakatifu na kukuza hazina yake.
Pia watunge melodia zinazolingana na sifa za muziki mtakatifu na
ambao unaweza kuimbwa si tu na kwaya kubwa, bali pia na kwaya ndogo. Tena
ziwasaidie waamini wote kushiriki kikamilifu.
Maneno yaliyomo katika nyimbo yalingane na mafundisho ya Kanisa katoliki,
zaidi yachukuliwe hasa katika Maandiko Matakatifu na vitabu vya liturujia.
Sura ya Saba
SANAA TAKATIFU NA VIFAA VITAKATIFU
Hadhi ya sanaa takatifu
122. Mambo ya sanaa (artes ingenuae) yanahesabika kwa haki
kati ya kazi za maarifa ya kibinadamu zenye heshima zaidi. Kati ya hizo,
sanaa ya kidini na kilele chake ambacho ni sanaa takatifu zinaheshimiwa kwa
namna ya pekee. Hizo, kwa maumbile yao, huhusiana na uzuri usiopimika wa
Mungu, ambao lazima udhihirishwe kwa namna fulani katika kazi za mwanadamu.
Tena, huelekea kwa Mungu na kwa kukuza sifa na utukufu wake, kwa sababu
hazina lengo jingine isipokuwa kuzielekeza kwa nguvu na kikamilifu, kwa njia
ya matunda yao, akili za wanadamu kwa Mungu.
Kwa sababu hizo, Mama Kanisa takatifu daima amependelea sanaa na
kutafuta huduma yao yenye heshima, ili mambo yahusuyo ibada takatifu yapewe
kweli heshima na uzuri, kwani hayo ni alama na ishara za yale ya mbinguni.
Kwa hiyo, Kanisa pia amejitahidi kuwalea wanasanaa. Tena Kanisa, tangu awali
na kwa haki, amejiona kuwa mwamuzi juu ya mambo ya sanaa, akichagua kati ya
kazi za wanasanaa zile zilinganazo na imani, uchaji na kanuni za mapokeo,
ili zifae kwa matumizi ya kidini.
Kwa bidii ya pekee Kanisa amejitahidi ili vifaa vitakatifu
vitumike kadiri ya heshima na uzuri wa ibada; na pia amekubali mabadiliko
yale ya malighafi, ya maumbo na ya madoido yaliyoingizwa na maendeleo ya
mbinu za sanaa katika mwenendo wa karne.
Kwa hiyo, Mababa wamependa kuamua yafuatayo.
Matumizi ya mitindo mbalimbali ya sanaa
123. Kanisa hana mtindo wake maalum wa sanaa, lakini amekubali mitindo ya
sanaa ya kila karne, kadiri ya tabia na mila za mataifa, na pia kufuatana na
matakwa ya kila ibada. Hivyo, katika mwenendo wa karne, Kanisa ameandaa
hazina ya sanaa ambayo lazima kuhifadhi kwa uangalifu mkubwa. Sanaa ya siku
hizi na ya mataifa yote na ya nchi zote ipate uhuru wa kujionyesha katika
Kanisa, mradi tu iwe kwa ajili ya heshima na matakwa ya majengo matakatifu
na maadhimisho ya kiliturujia. Kwa njia hii, [sanaa takatifu ya siku hizi]
iwezeshwe kuunganisha sauti yake na kwaya ile ya ajabu [ya masifu kwa ajili]
ya utukufu ambayo wanasanaa maarufu katika karne zilizopita waliimba kwa
imani katoliki.
124. Katika kuhimiza na kuhamasisha sanaa takatifu halisi, wenye mamlaka
katika Kanisa watafute uzuri wenye heshima kuliko fahari tupu. Vivyo hivyo
ifanywe mintarafu mavazi na vifaa vitakatifu.
Maaskofu wasikubali kamwe matendo ya sanaa yapinganayo na imani na
maadili na uchaji wa kikristo katika nyumba ya Mungu na mahali pengine
patakatifu. Pia wakatae yale yanayovunja heshima halisi ya kidini kwa sababu
ni mapotovu kwa upande wa maumbo au kwa sababu ya utovu wa uzuri wa kisanaa,
au ya uhafifu wake au hila.
Katika kujenga majengo matakatifu jitihada ifanyike ili yafae kwa
ajili ya kuadhimisha Liturujia na kwa kuwawezesha waamini kushiriki
kikamilifu.
125. Desturi ya kuonyesha picha na sanaa takatifu katika makanisa, kusudi
waamini waweze kuziheshimu, iimarishwe. Hata hivyo, idadi yake iwe ya kiasi
kifaacho, na mahali zinapowekwa pafuate utaratibu unaotakiwa, ili
kutowakwaza baadhi ya waamini na kutohimiza uchaji usio halali.
Sanamu takatifu
126. Katika kuhakiki kazi za sanaa, Wakuu wa mahali wasikilize
mapendekezo ya Kamati ya Sanaa takatifu ya Jimbo; na pia, kama inatakiwa,
wapokee mapendekezo kutoka kwa wale wenye ujuzi maalum, na kwa zile kamati
zilizotajwa katika ibara 44, 45 na 46.
Wenye mamlaka wakae macho ili vifaa vitakatifu au vitu vya thamani, kwa
vile ni urembo wa nyumba ya Mungu, visichukuliwe au kuharibiwa.
Malezi ya wanasanaa
127. Maaskofu, wenyewe au kwa njia ya mapadre wanaofaa ambao
wanajua na kupenda sanaa, wawaangalie wanasanaa kwa namna ya pekee, ili
kuwaelimisha juu ya roho ya sanaa takatifu na ya Liturujia takatifu.
Pia inatamaniwa kuanzisha shule au idara za sanaa takatifu katika nchi
zile ambazo inaonekana inafaa, ili kuwalea wanasanaa.
Wanasanaa wote ambao, wakiongozwa na maarifa yao, wanataka
kutumikia utukufu wa Mungu katika Kanisa takatifu, daima wakumbuke kwamba
wanafanya kazi ambayo ni mtindo wa igizo takatifu la Mungu Mwumbaji. Na pia
matunda ya kazi yao yatakuwa kwa ajili ya ibada katoliki, kukuza imani na
uchaji na malezi ya kidini ya waamini. Marekebisho ya sheria za sanaa
takatifu
128. Sheria za Kanisa na miongozo ya Kanisa inayohusu mambo ya nje
yahusuyo ibada takatifu, pamoja na vitabu vya Liturujia, vitengenezwe upya
upesi iwezekanavyo, kadiri ya ibara 25. Hasa yatazamwe tena mambo yafuatayo:
ujenzi unaostahili na wa kufaa wa majengo matakatifu; umbo na utengenezaji
wa altare; heshima, mahali na usalama wa tabernakulo ya Ekaristi; kufaa kwa
mahali pa kubatizia na heshima yake; sehemu ifaayo kwa kuweka sanamu, picha
takatifu na mapambo yote. Kutokana na msingi huo, sheria zile zisizolingana
na marekebisho ya Liturujia zisahihishwe au kufutwa; lakini zile
zinazoinufaisha zitunzwe au kuingizwa tena vipya.
Kwa jambo hilo, na hasa kuhusu malighafi na mitindo ya vifaa vitakatifu
na mavazi, Mabaraza ya Maaskofu ya kila mahali yanaruhusiwa kufanya
marekebisho yanayotakiwa kadiri ya mahitaji na mila za mahali panapohusika
na kufuatana na ibara 22 ya hati hii.
Uandaaji wa makleri mintarafu sanaa
129. Makleri, wakati wa masomo ya falsafa na teolojia, waelimishwe pia
kuhusu historia na maendeleo ya sanaa takatifu, kama vile kanuni halisi
zinazoongoza utengenezaji wa vitu vya sanaa na hivyo waweze kuheshimu na
kulinda majengo na matendo matakatifu (venerabilia monumenta) na pia
kutoa ushauri kwa wanasanaa, ili watimize vema kazi yao.
Zana za kiaskofu
130. Inafaa ishara za kiaskofu zitumiwe na watu wa Kanisa tu wenye Daraja
ya kiaskofu au mamlaka ya pekee.
Nyongeza
TANGAZO LA MTAGUSO MKUU VATIKANO II KUHUSU
MATENGENEZO YA
KALENDA
Mtaguso Mkuu Vatikano II hutilia maanani sana matakwa ya wengi, yaani ya
kutaka Sikukuu ya Pasaka iangukie daima Dominika fulani na hivyo kudai
matumizi ya kalenda isiyobadilika. Kwa sababu hiyo, baada ya kuchunguza kwa
makini yale yanayoweza kutokana na matumizi ya kalenda mpya ya namna hii,
Mtaguso Mkuu unatangaza yafuatayo:
1. Mtaguso Mkuu hauna kizuizi chochote kwa kuichagua Dominika fulani ya
Kalenda ya Kigregoriani kuwa Sikukuu ya Pasaka. Ila kiwepo kibali cha wale
wanaohusika, hasa ndugu zetu waliojitenga na Kiti cha Kitume.
2. Vilevile Mtaguso Mkuu hauwapingi wale ambao wangependa kuingiza
aina tofauti ya kalenda ya kudumu katika maisha ya kijamii.
Lakini, kati ya aina hizo mbalimbali za kalenda za kudumu
zinazopendekezwa ili ziingizwe katika maisha ya kijamii, Kanisa linadai juma
moja liendelee kuwa na jumla ya siku saba pamoja na Dominika. Kwa hiyo,
zisiongezwe siku nyingine zaidi ya zile saba za juma, ili mfululizo wa
majuma usibadilike; isipokuwa kama zipo sababu nzito mno. Nazo hazina budi
kukubaliwa na Kiti cha Kitume.
Mambo yote yaliyoamuliwa katika konstitusio hii, na kila moja kati
yao, yamewapendeza Mababa wa Mtaguso Mkuu. Nasi, kadiri ya mamlaka ya kitume
tuliyopewa na Kristo, na pamoja na Mababa waheshimiwa, katika Roho
Mtakatifu, tunayakubali, tunayaidhinisha na tunayathibitisha. Na yale yote
yaliyoamuliwa kwa pamoja katika Sinodi hii, tunaamuru yawekwe kwa utukufu wa
Mungu.
Roma, katika Kanisa la Mtakatifu Petro, 4 Desemba 1963
Mimi mwenyewe Paulo, Askofu wa Kanisa Katoliki
(zinafuata sahihi za Mababa)